Serikali yawashukuru wataalamu wa afya nchini kwa kutoa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa - Dkt. Mollel


Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Godwin Mollel akizungumza na wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa ziara yake ya kikazi katika Taasisi hiyo Jana Jijini Dar es Salaam


Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Godwin Mollel akizungumza na madaktari wa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) waliokuwa wakiwaudumia wagonjwa waliolazwa wodini wakati wa ziara yake ya kikazi katika Taasisi hiyo Jana Jijini Dar es Salaam.

Na: JKCI

Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Godwin Mollel amewashukuru wataalamu wa afya nchini kwa moyo wao wa uzalendo wa kutoa huduma bora za matibabu kwa wagonjwa.

Mhe. Mollel ameyasema hayo alipokuwa akizungumza na wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaja Kikwete (JKCI) aliowakuta wanawatibu wagonjwa wodini na kliniki wakati wa ziara yake ya kikazi aliyoifanya leo katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.

Dkt. Mollel alisema katika kipindi hiki ambacho kumekuwa na changamoto nyingi za maradhi wataalamu hao wa afya wamekuwa mkono wa Serikali kwa kuhakikisha wananchi wanakuwa salama kwa kutoa huduma bora za afya bila ya kuchoka.

“Kuna wakati mnafanya kazi katika mazingira magumu bila ya kuwa na hofu yoyote ile jambo la muhimu ni kuchukuwa tahadhari za msingi”, alisema Dkt. Mollel.

Alisema katika Hospitali nyingi alizotembelea asilimia 78 ya matatizo yaliyopo ni kutokana na viongozi wa maeneo husika kutokufanya kazi vizuri au kutokujua majukumu yao ya kazi na hivyo kuwakatisha tamaa watumishi wengine ambao pamoja na mazingira hayo magumu waliweza kufanya kazi zao kwa weledi.

Dkt. Mollel alipongeza , “Hapa JKCI ninawapongeza kwa juhudi zenu za kuhakikisha dawa zinapatikana kwa wagonjwa mnaowatibu. Katika maeneo mengine siyo kama dawa hakuna bali kuna udokozi pia wanatenga fedha kidogo za kununulia dawa ukilinganisha na bajeti husika”,.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi alisema kwa mwaka 2020 walitumia  kiasi cha shilingi milioni 158 kutoka mapato  ya ndani kwa ajili ya kuwasomesha wafanyakazi 20 wa kada mbalimbali ndani na nje ya nchi.

“Mwaka 2020 wafanyakazi 11 waliokuwa masomoni  ndani na nje ya nchi walimaliza masomo yao na kurudi kazini na kwa mwaka wa fedha 2020/21 wafanyakazi 13wameanza masomo”, alisema Prof.Janabi.

Prof. Janabi alisema Taasisi kwa kuwasomesha wafanyakazi hao imeweza kuzalisha wataalamu wa fani mbalimbali ambao baada ya kumaliza masomo yao wameweza kuongeza idadi ya mabingwa na hivyo kutoa huduma bora kwa wagonjwa.

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari