Walimu nchini wapewa mbinu zitakazowawezesha kufaidi matunda ya uchumi wa kati katika miaka ijayo

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akitoa mada kuhusu magonjwa ya moyo na jinsi ya kuyaepuka kwa walimu waliohudhuria mkutano wa walimu wakuu wa shule za sekondari nchini uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Jakaya Kikwete uliopo jijini Dodoma. JKCI imeshiriki katika mkutano huo kwa kufanya upimaji wa viashiria vya magonjwa ya moyo  pamoja na kutoa uelewa (awareness) wa magojwa hayo.


Na Veronica Mrema – Dodoma

Walimu nchini wamepewa mbinu zitakazowawezesha kufaidi matunda ya uchumi wa kati katika miaka ijayo, miongoni mwa mambo muhimu waliyohimizwa kuyazingatia ni kutunza afya zao.

Wamehimizwa pia kuepuka uzito uliokithiri na kufanya mara kwa mara uchunguzi wa afya ili kujua hali zao na kutibiwa mapema ikiwa watagundulika tayari wameanza kushambuliwa na magonjwa mbalimbali hususan yasiyoambukiza ambayo hivi sasa ni janga la dunia.

Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Profesa. Mohamed Janabi, alipowasilisha mada wakati wa ufunguzi wa Mkutano Mkuu wa 15 wa Walimu Wakuu wa Shule za Sekondari Tanzania (TAHOSSA).

Mkutano huo unaofanyika jijini hapa kwa muda wa siku tatu tangu jana (Desemba 20) ukitarajiwa kuhitimika Desemba  22, mwaka huu umepewa kauli mbiu isemayo ‘Elimu Bora na Umuhimu Wake katika Maendeleo ya Uchumi wa Kati’

“JKCI tumealikwa katika mkutano huu kuwasilisha mada kuhusu magonjwa yasiyoambukiza na kutoa huduma ya uchunguzi wa magonjwa ya moyo, hatukusita kuja.

“Tangu tulipoanza leo (jana) asubuhi hadi sasa (saa tano) ambapo mimi pia nimewaona walimu kadhaa, tumeona walimu 40, asilimia 37 ya walimu hawa tumewakuta wana uzito mkubwa (obesity) na asilimia 37.5 wana shinikizo kubwa la damu na hawakuwa wanajua hali zao kwamba ni wagonjwa.

“Kwa hali hii, tunapenda kutoa tahadhari kubwa kwa walimu wetu kwamba wanapaswa kuchukua hatua, nchi yetu ipo uchumi wa kati, kufaidi matunda yake lazima tutunze, watunze afya zao,” alisisitiza.

Aliongeza “‘Presha’ ni ugonjwa ambao hauna dalili na wengi hapa tumewakuta wanaugua tayari lakini walikuwa hawajui kwa sababu hawakuwa na dalili zozote.

“Wengine huwa wanasema kuumwa kichwa ni dalili ya ‘presha’, sikubaliani nao sana kwa sababu, kwa mfano nikiwa sina hela kichwa, wengine wakiwa na njaa kichwa kinauma.

“Hatari yake ni kwamba kitu chochote kikitokea, kikampa msongo wa mawazo mtu mwenye ‘presha’ na hajui hali yake, zile ‘stress’ zitaongezeka na itaweza kupasua mishipa yote ya damu,” alisema.

Prof. Janabi aliwahimiza kwamba kinga ni muhimu kuliko tiba katika kukabiliana na magonjwa hayo kwani gharama zake za matibabu ni kubwa.

“Matibabu dhidi ya magonjwa haya ni ghali na ndiyo maana nimesisitiza kwamba wakate bima ya afya kama ambavyo Serikali inaelekeza na inavyoelekea huko,” alisema.

Aliongeza “Imani yetu, walimu hawa ni wakuu wa shule, watakaporudi kule kwenye shule zao, watakwenda kuwaeleza walimu wao na walimu watawaeleza wanafunzi wao na wanafunzi watakwenda kueleza nyumbani kwao, elimu sahihi itaifikia jamii.

Aliongeza “Wazingatie wanatembea ‘steps’ (hatua) 10,000 kwa siku, wachunguze afya zao mara kwa mara, wazingatie ulaji unaofaa, ili kuepuka magonjwa haya.

“Lakini kwa wale ambao ni wagonjwa ni muhimu wazingatie matumizi ya dawa kama walivyoelekezwa na madaktari wao, shinikizo la damu ni tatizo lililopewa jina ‘silent killer’ (unaua taratibu).

“Dalili zake huchelewa kujitokeza kwa walio wengi, na ndiyo maana kitaalamu tunazungumzia moja ya tatu, kwa maana kwamba ukiwa na wagonjwa 90, yaani 30 kati yao huwa hawajijui, kundi jingine la watu 30 hawatumii dawa ipasavyo na kundi jingine la watu 30 wanatumia dawa.

“Tunaelimisha kwamba dhumuni letu, ni kuongeza hii idadi ya wagonjwa wa shinikizo la damu wanaotumia dawa kwa usahihi katika kukabiliana na tatizo hili,” alisema Prof. Janabi.


  

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari