Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) yaombwa kufikisha uelewa wa magonjwa ya moyo mashuleni
Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Winnie Masakuya akitoa uelewa wa jinsi ya kutunza moyo ili uwe na afya njema kwa walimu wakuu wa shule za Sekondari nchini waliofika katika banda la Taasisi hiyo kwa ajili ya kupima viashiria vya magojwa ya moyo wakati wa mkutano wa walimu hao unaomalizika hivi karibuni jijini Dodoma.
Walimu wakuu wa shule za Sekondari nchini wameiomba Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) kuhakikisha uelewa wa magonjwa ya moyo unatolewa kwa wanafunzi
wa shule za msingi na sekondari na siyo kwa watu wazima peke yao.
Wamesema uelewa
wa magonjwa hayo ukiwafikia wanafunzi utawasaidia kuitunza mioyo yao na hivyo
kuweza kuishi maisha marefu zaidi tofauti na inavyofanyika kwa sasa ambapo
uelewa unatolewa kwa watu wazima wengi wao wakiwa na umri wa kuanzia miaka 35
na kuendelea.
Ombi hilo limetolewa
hivi karibuni na baadhi ya walimu waliohudhuria mkutano wa 15 wa walimu wakuu wa
shule za sekondari nchini uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Jakaya
Kikwete uliopo jijini Dodoma.
Walimu hao
walisema ili kuwa na Taifa lenye afya njema ni vyema uelewa ukatolewa kwa
makundi yote kwenye jamii wakiwemo vijana walioko shule za msingi na sekondari
kwani wao ni wepesi wa kuelewa na kuyafanyia kazi maelekezo wanayopewa.
Akizungumza
na waandishi wa habari, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Kabugaro iliyopo
mkoani Kagera, Lucas Kajuna alisema wataalamu wa afya wanajitahidi kuelimisha
wananchi lakini bado uelewa wa magonjwa hayo ni mdogo nchini.
“Hasa kwa
wengi waishio vijijini ambao hawawezi kupata taarifa hizo kupitia vyombo vya
habari ikiwemo mitandao ya kijamii, redio na Televisheni,”alisema.
Mwalimu
Kajuna aliongeza “Hivi sasa maisha yetu Watanzania wengi yamebadilika tuna magari
hata wale ambao hawana wanatumia usafiri wa umma, bodaboda au bajaji, wengi
hatufanyi mazoezi hata ya kutembea, tunakula
vizuri ila siyo vyakula vyenye afya.
“Je, kutokana
na hali hii watanzania wangapi wanapata uelewa (awareness) wa magonjwa ya moyo
ili waweze kuepukana nayo?”, alihoji Mwalimu Kajuna.
Kwa upande wake, Mwalimu Mkuu wa Shule ya Sekondari Mnolela iliyopo mkoani Lindi, Adelfina Mbonde, alisema hii ni mara ya pili kushiriki katika mkutano huo na ameshuhudia tofauti kubwa.
“Mkutano wa
sasa umekuwa na mada nzuri ikiwemo ya jinsi ya kuepukana na magonjwa ya moyo
iliyotolewa na Profesa Janabi (Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI) pamoja na kufanyiwa
uchunguzi wa afya,”alisema.
Mwalimu huyo alisema
kwa hatua hiyo imewasaidia kupata uelewa jinsi ya kujikinga na magonjwa hayo
kwani mtu anapougua matibabu yake ni gharama kubwa.
“Ninaiomba
Serikali itoe uelewa wa magonjwa haya kwa kuwafikia wananchi wengi zaidi,
binafsi nitakaporudi Lindi, nimekusudia kila mwaka kuhakikisha walimu na
wanafunzi wa shule ninayoisimamia wanafikishiwa elimu hii kuhusu magonjwa
yasiyoambukiza, ili wapate uelewa,”alisisitiza.
Aliongeza
“Katika shule yetu wamekuwa wakija wataalamu wanaotoa elimu kuhusu namna ya
kuepuka magonjwa ya kuambukiza na hata malaria lakini kwa upande wa magonjwa yasiyoambukiza
hawajawahi kutufikia,”.
Mkutano huo umeandaliwa na Taasisi isiyo ya Kiserikali ya Global Education Link, ambapo JKCI imeshiriki kutoa uelewa (awareness) kuhusu magonjwa yasiyoambukiza pamoja na kufanya uchunguzi wa viashiria vya magonjwa ya moyo kwa walimu 700.
Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Winnie Masakuya akimwelekeza mwalimu mkuu wa shule ya sekondari Kyamulaile iliyopo mkoani Kagera Gerac Henerico madhara ya mafuta katika mishipa ya damu ya moyo wakati wa mkutano wa walimu hao uliofanyika jijini Dodoma ambapo JKCI ilishiriki kwa kufanya upimaji wa viashiria vya magonjwa ya moyo pamoja na kutoa uelewa (awareness) wa magojwa hayo kwa walimu 700.
Afisa Uuguzi
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Wamara akimweleza mwalimu mkuu
wa shule ya sekondari Kabugaro iliyopo mkoani Kagera Lucas Kajuna madhara ya
uzito mkubwa katika afya ya moyo wakati wa mkutano wa walimu hao unaofanyika
jijini Dodoma. JKCI ilishiriki
katika mkutano huo kwa kufanya
upimaji wa viashiria vya magonjwa ya moyo pamoja na kutoa uelewa (awareness) wa magonjwa hayo
kwa walimu 700.
Mwandishi wa
kujitegemea wa habari za afya Veronica Mrema akimpima urefu mwalimu mkuu wa
shule ya sekondari aliyehudhuria mkutano wa walimu wakuu wa shule za sekondari
nchini uliofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Jakaya Kikwete uliopo jijini
Dodoma. JKCI imeshiriki katika mkutano huo kwa kufanya upimaji wa viashiria vya
magonjwa ya moyo pamoja na kutoa uelewa (awareness) wa magojwa hayo kwa walimu 700.
Comments
Post a Comment