Mkutano wa CardioTan Imaging 2026, WHO yaeleza maendeleo ya JKCI
Meneja wa Program
Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania Dkt. Sisay Tegegne akizungumza na
wataalamu wa afya alipokuwa akimwakilisha Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika,
Shirika la Afya Duniani (WHO) Prof. Mohame Janabi wakati wa ufunguzi wa Mkutano
wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 unaofanyika
katika ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akielezea mafanikio ya taasisi hiyo wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 unaofanyika katika ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Katibu Mkuu Msaidizi wa Ligi ya Arab
kutoka nchini Misri Balozi Mohanad Legouzi wakisaini mkataba wa mashirikiano
katika kujali afya za wanamichezo, kubadilishana ujuzi na kushiriki katika
huduma za jamii kupitia shirika la Heart
to Heart Association for sustainable development wakati wa ufunguzi wa Mkutano
wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 unaofanyika
katika ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam.
Baadhi ya wataalamu wa afya kutoka ndani na nje ya nchi wakifuatilia mada zilizokuwa zikiendelea wakati wa ufunguzi wa Mkutano wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 unaofanyika katika ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa bodi ya
wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hassan Mahmoud Mshinda
akimpatia tuzo ya mdhamini mkuu wa mkutano nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo
– CardioTan Imaging 2026 Mkuu wa Kitengo cha Biashara Benki ya Azania Samson
Mahimbi wakati wa ufunguzi wa Mkutano huo unaofanyika katika ukumbi wa Blue
Sapphire jijini Dar es Salaam.
Meneja wa Program
Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania Dkt. Sisay Tegegne akiwa katika
picha ya pamoja na viongozi kutoka Wizara ya Afya na Taasisi zake pamoja na
wajumbe wa kamati ya maandalizi ya Mkutano wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo
– CardioTan Imaging 2026 baada ya ufunguzi wa mkutano huo leo jijini Dar es
Salaam.
Na JKCI
***************************************************************************************************
Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) yatajwa kuwa moja ya taasisi za afya nchini yenye ubunifu na
kuleta mafanikio katika sekta ya afya huku ikizidi kujijengea sifa katika Bara
la Afrika.
Hayo yamesemwa na
Meneja wa Program Shirika la Afya Duniani (WHO) nchini Tanzania Dkt. Sisay
Tegegne wakati akimuwakilisha Mkurugenzi wa Kanda ya Afrika, Shirika la Afya
Duniani (WHO) Prof. Mohame Janabi kufungua mkutano wa nne wa Kimataifa wa
Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 unaofanyika katika ukumbi wa Blue
Sapphire jijini Dar es Salaam.
Dkt. Tegegne alisema ni
jambo la kufurahisha kuona mkutano huo muhimu unawakutanisha wataalamu wa afya kutoka
nchi mbalimbali ukiwa na lengo la kuimarisha huduma za uchunguzi, utambuzi wa
haraka wa vipimo vya moyo na matibabu ya magonjwa hayo huku ukionesha maendeleo
yanayopatikana katika sekta ya afya nchini Tanzania.
“Tanzania ipo katika
nafasi nzuri katika huduma za matibabu ya moyo kutokana na historia yake ya
maendeleo, upanuzi wa huduma umekuwa ukiendelea ndani na nje ya mipaka ya nchi jambo
ambalo ni la kujivunia”, alisema Tegegne
Dkt. Tgegne alisema mustakabali
wa huduma za matibabu ya moyo nchini una matumaini makubwa kutokana na
kuongezeka kwa utaalamu, ubunifu na matumizi ya teknolojia mpya, pia huduma za
upandikizaji wa moyo zinazotarajiwa kuanza kutolewa Tanzania baada ya miaka
mitano zitaongeza maendeleo katika sekta ya afya.
Kwa upande wake Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema
kupitia mkutano huo JKCI imeweza kuwakutanisha wataalamu kutoka nchi mbalimbali
duniani ili kwapamoja waweze kushirikiana na kubadilishana mawazo ya jinsi ya
kuwahudumia wagonjwa wa moyo.
“Uwekezaji uliofanywa
na Serikali yetu katika sekta ya afya ni mkubwa, hivyo tumetaka kuionesha dunia
ni jinsi gani Tanzania imewekeza vya kutosha katika huduma za afya hasa upande
wa matibabu ya moyo”, alisema Dkt. Kisenge
Dkt. Kisenge alisema
magonjwa ya moyo na yale yasiyoambukiza yanazidi kuongezeka na kuchangia vifo
vya watu wengi ambapo jumla ya watu milioni 17 duniani hupoteza maisha kutokana
na magonjwa hayo.
“Kwa hapa Tanzania
magonjwa ya moyo yanafikia asilimia 25 kwa sasa, hivyo ni lazima tuwe na vifaa
vya kugundua magonjwa haya ili tuweze kuwatibu vizuri wagonjwa wetu”, alisema
Dkt. Kisenge
Wakielezea mafanikio ya
mkutano huo washiriki wa mkutano walisema Tanzania ipo katika mwelekeo sahihi
wa kuwa kinara wa huduma za matibabu ya moyo si tu ndani ya nchi bali pia
kusini mwa jangwa la Sahara.
Daktari bingwa wa
magonjwa ya moyo na mwanzilishi wa huduma za moyo Tanzania Johnson Rwakatare alisema
huduma walizoanzisha kipindi hicho na mafanikio yaliyopo sasa yanawatia moyo
waanzilishi wa huduma hizo nchini.
“Nakumbuka wakati
tunaanza huduma za matibabu ya moyo hapa nchini tulikuwa watatu lakini sasa
hivi wataalamu wa magonjwa ya moyo ni wengi na wameweza kuendeleza huduma hizi
kwa kujifunza mbinu mbalimbali za kuyatibu magonjwa ya moyo”, alisema Dkt.
Rwakatare
Dkt. Rwakatare alisema
baada ya Serikali kuonesha dhamira kubwa ya kuinua huduma za matibabu ya moyo
nchini, huduma hizo zimeboreshwa na kuifanya Tanzania kujivunia kuwa kinara wa
matibabu ya moyo ikilinganishwa na nchi zilizoendelea.
Mkutano wa nne wa
Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 wenye kauli mbiu
uchunguzi mahiri kwa moyo imara unafanyika kwa siku tatu na kuwakutanisha
wataalamu wa afya kutoka nchi za Chile, Kenya, Marekani, Uganda, Misri, na
Afrika ya Kusini.





Comments
Post a Comment