Mkutano wa CardioTan Imaging 2026 Kujadili Matumizi ya Akili Unde matibabu ya moyo

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na waandishi wa habari leo kuhusu Mkutano wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 utakaofanyika tarehe 4 hadi 6 mwezi Juni mwaka huu katika ukumbi wa Blue Sapphire Jijini Dar es Salaam. 

Mwenyekiti wa Mkutano wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026, Iddi Lemah akizungumza na waandishi wa habari leo kuelekea mkutano huo utakaofanyika tarehe 4 hadi 6 mwezi Juni mwaka huu katika Ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam.

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Engerasia Kifai akizungumza na waandishi wa habari kuhusu umuhimu wa Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 utakaofanyika tarehe 4 hadi 6 mwezi Juni mwaka huu katika Ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Idara ya magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane akizungumza na waandishi wa habari kuhusu ubora wa Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 utakaofanyika tarehe 4 hadi 6 mwezi Juni mwaka huu katika Ukumbi wa Blue Sapphire, Dar es Salaam.

Baadhi ya wajumbe wa kamati ya maandalizi ya Mkutano wa nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo – CardioTan Imaging 2026 wakifuatilia mada zilizokuwa zikiendelea katika mkutano na waandishi  wa habari kuelekea mkutano huo utakaofanyika tarehe 4 hadi 6 mwezi Juni mwaka huu katika Ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam.

Na JKCI

***************************************************************************************************

Mkutano wa nne wa kimataifa wa magonjwa ya moyo (CardioTan Imaging 2026) kuwakutanisha wataalamu wa afya kutoka nchi mbalimbali duniani kujadili matumizi ya teknolojia za kisasa katika utambuzi na matibabu ya magonjwa ya moyo.

Mkutano huo unaofanyika katika Ukumbi wa Blue Sapphire jijini Dar es Salaam utafanyika kwa siku tatu kuanzia tarehe 4 hadi 6, 2026 kwa lengo la kubadilishana ujuzi, kuboresha huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo pamoja na kuongeza ushirikiano wa wataalamu kutoka nchi washiriki wa mkutano huo.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema mkutano huo ni sehemu ya jukwaa la wataalamu wa afya kubadilishana uzoefu na kujadili mbinu mpya za utambuzi na matibabu ya magonjwa ya moyo kwa kutumia akili unde.

“Katika mkutano huu tutajadiliana njia mbalimbali za kutibu magonjwa ya moyo na miongoni mwa mada zitakazojadiliwa ni pamoja na matumizi ya teknolojia ya kisasa hususani akili unde (Artificial Intelligence) katika kutibu magonjwa ya moyo”, alisema Dkt. Kisenge.

“Tunategemea madaktari wa moyo pamoja na wataalamu wa radiolojia kuanzia ngazi ya diploma hadi wale wenye utaalamu wa hali ya juu watakaa pamoja kujadili njia mbalimbali za kutumia teknolojia za kisasa kuwasaidia wagonjwa wa moyo”, alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge alisema mkutano huo utatumika pia kama sehemu ya kuitangaza Tanzania kimataifa lakini pia kutangaza utalii tiba unaofanya na Taasisi hiyo.

“Mkutano huu vilevile unaenda kuchangia katika masuala ya tiba utalii kwa sababu kutakuwa na wawakilishi kutoka nchi mbalimbali za Afrika watakaokuja kujionea uwezo wa JKCI na maendeleo makubwa yaliyofanyika katika Taasisi yetu”, alisema Dkt. Kisenge.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Mkutano wa Nne wa Kimataifa wa Magonjwa ya Moyo (CardioTan Imaging 2026) Iddi Lemah alisema mkutano huo ni mwendelezo wa jitihada za JKCI kutoa mafunzo kwa wataalamu wa afya na wadau wengine wa sekta ya afya.

“Mkutano huu ni wa nne tangu tulipoanzisha mpango huu wa kutoa mafunzo mbalimbali kwa wataalamu wa afya, watunga sera na wadau wengine, tunawakaribisha wataalamu na wadau mbalimbali kushiriki mkutano huu na kujionea mafanikio tuliyoyapata”, alisema Lemah.

Akielezea namna mkutano huo utakavyokuwa Mkurugenzi wa Idara ya Magonjwa ya Moyo wa kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Tatizo Waane alisema mkutano huo pia utawawezesha wataalamu wa afya kujadili umuhimu wa kugundua magonjwa ya moyo katika hatua za awali.

“Moja ya mada zitakazojadiliwa katika mkutano  huu ni ile ya namna ya kufanya utambuzi wa magonjwa ya moyo katika hatua za awali na jinsi vipimo mbalimbali vinavyoweza kusaidia matibabu ya wagonjwa wa moyo”, alisema Dkt. Waane.

Naye Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Engerasia Kifai alisema kupitia mkutano huo kutafanyika uzinduzi wa chama cha umoja wa upimaji moyo kuwaunganisha wataalamu hao na kubadilishana uzoefu.

“Siku hiyo pia kutakuwa na uzinduzi wa chama cha umoja wa upimaji moyo Tanzania (Echocardiography Society) tukiwa na lengo la kuwajumuisha na kuwasajili wataalamu wote wanaofanya vipimo vya moyo na kusaidia kutoa mafunzo endelevu, kuongeza wigo wa tafiti ili kuboresha huduma za utambuzi wa magonjwa ya moyo”, alisema Dkt. Kifai.

Mkutano wa CardioTan Imaging 2026 unatarajiwa kuwa jukwaa muhimu la kuimarisha ushirikiano, kujadili, kuendeleza matumizi ya teknolojia za kisasa katika kutoa huduma bingwa bobezi za matibabu ya moyo na kuitangaza Tanzania kama kitovu cha huduma bingwa za magonjwa ya moyo barani Afrika.

Comments

Popular posts from this blog

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi