TAKUKURU yachangia milioni 20.89 matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akipokea hundi ya shilingi milioni 20.89 kutoka kwa Mkuu wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Ilala Faustine Maijo kwaajili ya kusaidia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Msimamizi wa Wodi ya
watoto wenye magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Tedy
Tarimo akielezea namna wodi hiyo inavyotoa huduma wakati Mkuu wa Taasisi ya
Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Ilala Faustine Maijo
alipotembelea wodi hiyo mara baada ya kukabidhi hundi ya shilingi milioni 20.89
kuchangia gharama za matibabu ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa
katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.Taasisi ya Kuzuia na
Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) imechangia shilingi milioni 20.89 kusaidia matibabu
ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI).
Fedha hizo
zimekabidhiwa katika Shirika lisilo la kiserikali la Heart Team Africa
Foundation (HTAF) linalounga mkono juhudi zinazofanywa na Serikali kwa
kuchangisha fedha za matibabu ya moyo kwa watu wasiokuwa na uwezo wa kugharamia
matibabu hayo hasa watoto wenye magonjwa ya moyo.
Akizungumza wakati wa
hafla fupi ya kupokea hundi hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema JKCI kupitia HTAF imekuwa ikiratibu
upatikanaji wa fedha kwaajili ya kusaidia matibabu ya watoto wenye magonjwa ya
moyo pamoja na kuendeleza tafiti na elimu kuhusu magonjwa hayo.
Dkt. Kisenge alisema
HTAF imekuwa daraja muhimu la kuwahusisha wadau mbalimbali katika kusaidia
matibabu ya watoto wenye matatizo ya moyo na kuimarisha elimu pamoja na tafiti
za magonjwa hayo hivyo kubadilisha maisha ya watoto wengi waliokuwa katika hali
ngumu kiafya.
“Moja ya kazi inayofanywa na Shirika hili ya
HTAF ni kukusanya rasilimali fedha lakini vilevile kusimamia masuala ya tafiti
na elimu kuhusu magonjwa ya moyo ambayo yanachangia vifo vingi duniani, mwaka
jana tulikusanya bilioni 2.7 na tumeweza kuwasaidia watoto zaidi ya 305 wenye
matatizo ya moyo kufanyiwa upasuaji bila kulipia gharama za matibabu”, alisema
Dkt. Kisenge.
Kwa upande wake Mtendaji
Mkuu wa Shirila lisilo la Kiserikali la Heart Team Africa Foundation (HTAF) Dkt.
Naizihijwa Majani alisema licha ya Serikali kubeba sehemu kubwa ya gharama za
matibabu ya moyo bado familia nyingi zinashindwa kumudu gharama ndogo iliyobakia
katika huduma hizo bingwa za matibabu ya moyo hivyo ikaona ishiriki ili watoto
wapate matibabu kwa wakati.
“Matibabu ya moyo ni
miongoni mwa matibabu yenye gharama kubwa sana duniani hata baada ya Serikali kuchangia
sehemu kubwa ya gharama bado kuna gharama nyingi zinahitajika kukamilisha
matiababu kwa baadhi ya magonjwa ya moyo”,
“Tunawashukuru TAKUKURU
kwa kutushika mkono kwa sababu fedha hizi zimetoka mifukoni mwa wafanyakazi wa
TAKUKURU wakiwa na lengo la kuwasaidia watoto wanaohitaji matibabu ya moyo”, alisema
Dkt. Naizihijwa.
Naye Mkuu wa Taasisi ya
Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Ilala Faustine Maijo alisema
taasisi hiyo imeguswa na changamoto zinazowakabili watoto wenye matatizo ya moyo
pamoja na familia zao na kuamua kurudisha kwa jamii kwakuchangia matibabu yao.
“Tunatambua kuwa mtoto
mwenye tatizo la moyo anahitaji matibabu ya haraka na gharama zake mara nyingi
ni kubwa kwa wazazi wengi, mchango huu mdogo ukawe faraja na ufungue mlango wa
matibabu kwa baadhi ya watoto wanaoendelea kupata matibabu katika Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)”, alisema Maijo.
Akitoa neno la shukrani
Meneja Mkuu kutoka Global Medicare Daniel Lazaro aliishukuru TAKUKURU kwa
kuonesha mfano bora wa uwajibikaji kwa jamii kupitia msaada huo.
“Uongozi wa TAKUKURU
umeweza kuwashirikisha watumishi wake katika jambo muhimu la kusaidia wahitaji
kwenye jamii, huu ni mfano wa kuigwa kwa sababu si taasisi nyingi zenye
utamaduni wa kujitolea kusaidia watu wenye mahitaji maalum kama ambavyo
mmefanya”, alisema Lazaro.
Mchango huo wa shilingi
milioni 20.89 unatarajiwa kuwasaidia watoto wengi zaidi wenye matatizo ya moyo
kupata matibabu ya kibingwa yanayotolewa na JKCI katika kurejesha tabasamu
lililofichwa na maumivu ya magonjwa ya moyo yanayowakabili.
Picha na JKCI
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
Comments
Post a Comment