Jengo la Utawala na Vipimo lenye thamani ya Tshs Bilioni 9.7 lazinduliwa kuimarisha huduma za moyo nchini

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa na Mwenyekiti wa bodi ya Wadhamini ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Hassan Mshinda wakizindua jengo la Utawala na Vipimo wakati wa hafla fupi ya kuzindua jengo hilo iliyofanyika jana katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa akiangalia moja ya mashine inayotumia akili unde kufanya uchunguzi wa afya wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa jengo la Utawala na Vipimo iliyofanyika jana katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa akiangalia moja ya mashine inayotumia akili unde kufanya uchunguzi wa afya wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa jengo la Utawala na Vipimo iliyofanyika jana katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam.

Daktari bingwa wa magonjwa ya figo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Frida Moyo akimuelezea Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa huduma zinazotolewa katika kitengo cha Dialysis wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa jengo la Utawala na Vipimo iliyofanyika jana katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam.

Afisa Uhusiano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Agnes Sikaonga akifanya mahojiano na Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengera alipotembelea Studio ya Health Promotion wakati wa hafla fupi ya uzinduzi wa jengo la Utawala na Vipimo iliyofanyika jana katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam.

Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa akipokelewa na mtoto aliyelazwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) alipowasili katika Taasisi hiyo kwaajili ya hafla fupi ya kuzindua jengo la Utawala na Vipimo iliyofanyika jana jijini Dar es Salaam.

Picha na JKCI

****************************************************************************************************

Serikali kupitia Wizara ya Afya imezindua rasmi Jengo la Utawala na Vipimo lililopo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) hatua inayolenga kuimarisha huduma za kibingwa na ubingwa bobezi nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo iliyofanyika jijini Dar es Salaam Waziri wa Afya Mhe. Mohamed Mchengerwa, alisema uwekezaji huo unaonesha dhamira ya Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuboresha huduma za afya na kufanikisha malengo ya maendeleo ya taifa kuelekea mwaka 2050.

“Jengo hili limegharimu takribani shilingi bilioni 9.7, litasaidia kuongeza uwezo wa JKCI kwenye uchunguzi, matibabu na usimamizi wa huduma za moyo, kwani thamani yake halisi ipo katika maisha yatakayookolewa, tabasamu litakalorejeshwa kwa jamii na ubora wa huduma utakaoongezeka”, alisema Mhe. Mchengerwa.

Mhe. Mchengerwa alisema kwa kipindi cha zaidi ya miaka kumi iliyopita JKCI imeweza kutoka kuwa ndoto ya kuwa kituo cha kisasa cha moyo hadi taasisi inayotambulika kimataifa kwa huduma za uchunguzi, upasuaji wa moyo, mafunzo ya wataalamu na tafiti za kisayansi.

Mhe. Mchengerwa alisema jengo alilolizindua lina maabara ya kisasa iliyogharimu kiasi cha shilingi bilioni 5.4, yenye uwezo wa kufanya vipimo vya magonjwa ya moyo, damu, figo, homoni na kemia ya mwili kwa viwango vya kimataifa, hivyo kuboresha usahihi wa uchunguzi na matibabu.

“Maabara hii pia imefungwa teknolojia ya Akili Unde (AI) na mifumo ya kisasa ya Automation inayorahisisha uchakataji wa sampuli, kuongeza usahihi wa majibu na kupunguza muda wa kusubiri matokeo ya vipimo”, alisema Mhe. Mchengerwa

Aidha Mhe. Mchengerwa alisema jengo hilo pia linatoa huduma za vipimo vya Echocardiography (ECHO), X-Ray za kisasa, kliniki ya wagonjwa wakimataifa, kitengo cha Dialysis huku likiwa na studio ya uhamasishaji na uelimishaji wa afya (Health Promotion Studio) kwa ajili ya kutoa elimu kwa umma juu ya kinga ya magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya shinikizo la damu, kisukari na magonjwa ya moyo.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema uwepo wa jengo hilo ni sehemu ya kuokoa maisha ya wagonjwa wanaotibiwa katika taasisi hiyo kwani watafanyiwa uchunguzi vizuri kupitia maabara hiyo na kupatiwa matibabu stahiki.

Dkt. Kisenge alisema JKCI imekuwa kutokana na huduma inazozitoa kwani sasa Taasisi hiyo ni miongoni mwa Taasisi kubwa Afrika Mashariki na Kati kufanya upasuaji wa moyo mkubwa ikiwemo upasuaji wa kisasa wa kubadilisha valvu ya moyo bila kufungua kifua (Transcatheter Aortic Valve Implantation - TAVI).

“Tumefungua matawi ya JKCI maeneo mbalimbali hapa Dar es Salaam na mkoani Arusha, tunataka miaka 10 ijayo kila mkoa uwe na tawi la JKCI, lakini pia tunafikiria kufungua tawi la JKCI nje ya nchi yote haya ni kuionesha dunia kuwa JKCI tumeendelea katika kutoa huduma bingwa bobezi za moyo”, alisema Dkt. Kisenge

Aidha Dkt. Kisenge alisema maono ya JKCI katika miaka ijayo ni kuhakikisha kuwa inafanya upasuaji wa moyo kwa kutumia roboti lakini pia inaweza kupandikiza moyo kwa wagonjwa wanaohitaji huduma hiyo.


 

Comments

Popular posts from this blog

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi