Wagonjwa nane wenye mishipa ya damu iliyoziba kufanyiwa upasuaji wa moyo
Wataalamu wa Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakishirikiana na mwenzao kutoka Hospitali ya Jaslok
iliyopo Mumbai nchini India Upendra Bhalerao kumfanyia upasuaji wa kupandikiza
mshipa wa damu wa moyo bila kusimamisha moyo mgonjwa mwenye matatizo ya mishipa
ya damu kuziba wakati wa kambi maalumu ya siku nane inayofanyika katika Taasisi
hiyo jijini Dar es Salaam.
Daktari bingwa wa
upasuaji wa moyo, mishipa ya damu na kifua kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo
Mumbai nchini India Upendra Bhalerao akitoa mafunzo kwa wataalamu wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) namna ya kutoa huduma kwa wagonjwa ambao
mshipa yao ya damu imeziba wakati wa kambi maalumu ya siku nane inayofanyika
katika Taasisi hiyo jijini Dar es Salaam.
Na JKCI
***************************************************************************************************
Wagonjwa nane wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba (coronary artery disease) kufanyiwa upasuaji wa kupandikiza mishipa ya damu ya moyo bila kusimamisha moyo (off Pump CABG).
Upasuaji huo unafanyika katika kambi maalumu ya siku nane inayofanywa na watalaamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo Mumbai nchini India.
Akizungumza na mwandishi wa habari hii leo jijini Dar es Salaam, Mkurugenzi wa Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba watumie kambi hiyo kupata matibabu na kupunguza gharama ambazo wangetumia kusafiri nje ya nchi kwaajili ya matibabu.
“Upasuaji huu unafaida kubwa kwa wagonjwa ambao wamekuwa wakitumia dawa kwa muda mrefu kwa kupata matibabu kwani unafanyika bila kusimamisha moyo na unamsaidia mgonjwa kupona kwa muda mfupi na kuendelea na shughuli zake za kawaida”, alisema Dkt. Angela.
Dkt. Angela alibainisha kuwa kupitia kambi hiyo wataalumu wa JKCI watapata fursa ya kujengewa uwezo na kubadilishana uzoefu na wenzao kutoka India jambo mbalo litasaidia kuimarisha zaidi huduma za upasuaji na mishipa ya moyo nchini.
“Tayari tumemfanyia upasuaji mgonjwa mmoja ambaye mishipa mitatu ya moyo ilikuwa imeziba kwa mafanikio makubwa na tunatarajia kuwafanyia upasuaji wagonjwa nane katika kambi hii”, alisema Dkt. Angela.
Kwa upande wake Daktari Bingwa wa Upasuaji wa Moyo na Mishipa ya Damu kutoka Hospitali ya Jaslok iliyopo Mumbai nchini India Upendra Bhalerao alisema upasuaji huo unafanyika kwa ufanisi mkubwa kutokana na uwekezaji mkubwa wa vifaa tiba uliofanywa na Serikali ya Tanzania kupitia JKCI.
“Tumekuwa tukija Tanzania mara kwa mara kutokana na ushirikiano mzuri wa kitabibu uliopo kati ya India na Tanzania na kuwasaidia wagonjwa ambao wanatumia gharama kubwa kufuata matibabu India hivyo uwepo wetu hapa umekuwa ukiwapunguzia adha wagonjwa wenye matatizo ya mishipa yad amu ya moyo iliyoziba”, alisema Bhalerao.
Kambi hiyo maamulu ya upasuaji wa mishipa ya damu ya moyo
iliyoziba inatarajiwa kumalizika mapema tarehe 15 mwezi Juni mwaka huu.



Comments
Post a Comment