Watu 546 wapimwa Namba Zao katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma Dodoma

Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwa katika picha ya pamoja wakati wa maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyokuwa yakifanyika katika Viwanja vya Chinangali Park na kumalizika leo jijini Dodoma. Jumla ya watu 546 wamepimwa Namba Zao. 

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Bakar Mohamed akimpima shinikizo la damu mwananchi aliyefika katika banda la Taasisi hiyo kwaajili ya kujua Namba Zake wakati wa maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyokuwa yakifanyika katika Viwanja vya Chinangali Park na kumalizika leo jijini Dodoma. Jumla ya watu 546 wamepimwa Namba Zao. 

Wananchi wakiendelea kupata elimu kuhusu Namba Zao katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma yaliyokuwa yakifanyika katika Viwanja vya Chinangali Park na kumalizika leo jijini Dodoma. Jumla ya watu 546 wamepimwa Namba Zao.

Na JKCI

*************************************************************************************************

Jumla ya watu 546 wamefanyiwa uchunguzi wa afya kwa kupimwa Namba Zao wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi wa afya iliyokuwa ikifanyika katika Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma.

Kupitia kambi hiyo iliyomalizika leo katika Viwanja vya Chinangali Park vilivyopo jijini Dodoma watu waliotembelea katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) walifanyiwa vipimo vya kuchunguza ugonjwa wa shinikizo la damu, kiwango cha sukari kwenye damu, uwiano wa urefu kwa uzito pamoja na mzunguko wa kiuno.

Aidha watu 192 walifanyiwa kipimo cha kuchunguza utendaji kazi wa moyo (Echocardiography – ECHO), huku watu 11 wakifanyiwa kipimo cha kuangalia mfumo wa umeme wa moyo (Electrocardiography – ECG).

Akizungumza wakati wa kuhitimisha kambi hiyo Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Daud Gwilenza alisema watu 94 wamepewa rufaa kwenda katika Taasisi hiyo kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

“Watu 82 tumewabaini kuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu, huku watu 20 tumewabaini kuwa na tatizo la sukari. Baadhi ya watu hawa walikuwa tayari wanajua hali zao lakini wengine hawakuwa wanajua kama wana matatizo ya shinikizo la damu na sukari”, alisema Dkt. Daud.

Dkt. Daud aliongeza kuwa magonjwa mengine yaliyobainika kupitia kambi hiyo ni pamoja na kuziba kwa mishipa ya damu ya moyo na kutanuka kwa moyo hali ambayo kwa kiasi kikubwa husababishwa na shinikizo la damu la muda mrefu.

“Jamii inapaswa kujenga utamaduni wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara, hii itatusaidia kulinda afya zetu na kuchukua hatua mapema tunapogundulika kuwa na magonjwa yasiyoambukiza ambayo kwa sasa yanaongezeka kwa kasi katika jamii yetu”, alisema Dkt. Daud.

Kwa upande wao wananchi waliopata huduma katika banda la JKCI waliishukuru Serikali kwa kuwezesha kufanyika kwa Maonesho ya Wiki ya Utumishi wa Umma mkoani Dodoma jambo lililowapa fursa ya kufanyiwa uchunguzi wa afya bila gharama.

James Balilonga mkazi wa Dodoma alisema maonesho hayo yamemsaidia kutambua umuhimu wa kufanya uchunguzi wa afya hata pale mtu anapokuwa hana dalili za ugonjwa.

“Unapokutana na wataalamu wa afya na kupata elimu kuhusu umuhimu wa kuchunguza  afya unahamasika kuchukua hatua. Hili limekuwa fundisho kwangu kwamba siyo lazima nisubiri kuumwa ndipo nifanye uchunguzi wa afya”, alisema James.

Naye Doris Mwirezeyo alizitaka taasisi za afya kuanzia ngazi ya Wilaya kuendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu umuhimu wa kuchunguza afya mara kwa mara ili kuwasaidia wananchi kujikinga na magonjwa na kupata matibabu kwa wakati.

“Leo nimejifunza jambo muhimu, kama tungekuwa na utamaduni wa kupima afya mara kwa mara na kuzingatia mtindo bora wa maisha pengine tusingekuwa na wagonjwa wengi wenye matatizo ya moyo, elimu hii inapaswa kuwafikia wananchi hadi ngazi za chini ili waweze kujilinda”, alisema Doris.



 

Comments

Popular posts from this blog

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi