Wizara ya Afya, JKCI na Children’s HeartLink waweka mikakati ya kuimarisha huduma za moyo kwa watoto nchini
Mkurugenzi Mtendaji wa
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akielezea namna
Taasisi hiyo inavyotoa huduma kwa watoto wenye magonjwa ya moyo wakati wa
mkutano na wadau wa afya kuweka mikakati ya kitaifa kuimarisha huduma za matibabu
ya moyo kwa watoto uliofanyika jana katika ukumbi wa Taasisi hiyo iliyopo
jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi wa huduma za
tiba Wizara ya Afya Dkt. Hamad Nyembea akizungumza wakati wa mkutano na wadau
wa afya kuweka mikakati ya kitaifa kuimarisha huduma za matibabu ya moyo kwa
watoto uliofanyika jana katika ukumbi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Msaidizi
Magonjwa Yasiyoambukiza kutoka Wizara ya Afya Dkt. Omary Ubuguyu akizungumza wakati
wa mkutano na wadau wa afya kuweka mikakati ya kitaifa kuimarisha huduma za
matibabu ya moyo kwa watoto uliofanyika jana katika ukumbi wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam.
Makamu wa Rais Mkakati
wa Kimataifa na Utetezi Shirika la Children’s HeartLink Bistra Zheleva akielezea
namna Shirika hilo litakavyoweka mikakati ya kusaidia watoto wenye magonjwa ya
moyo waliopo nchini Tanzania wakati wa mkutano na wadau wa afya kuweka mikakati
ya kitaifa kuimarisha huduma za matibabu ya moyo kwa watoto uliofanyika jana
katika ukumbi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es
Salaam.
Wadau wa sekta ya afya
wakiwa katika makundi kujadili mikakati ya kusaidia watoto wenye magonjwa ya
moyo wakati wa mkutano na wadau wa afya kuweka mikakati ya kitaifa kuimarisha
huduma za matibabu ya moyo kwa watoto uliofanyika jana katika ukumbi wa Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam.
Na JKCI
**************************************************************************************************
Serikali kupitia Wizara
ya Afya, kwa kushirikiana na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Shirika la
Children’s HeartLink na Shirika la Afya Duniani (WHO) waweka mikakati ya
kitaifa kuimarisha huduma za matibabu ya moyo kwa watoto kuhakikisha kila mtoto
mwenye ugonjwa huo anagundulika mapema, anapata matibabu kwa wakati na kuongeza
nafasi ya kuishi.
Akizungumza wakati wa
mkutano uliofanywa na wadau hao jana jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji
wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema ushirikiano
huo umewakutanisha wataalamu na wadau hao ili kujadili njia bora za kuboresha
huduma za moyo kwa watoto nchini na katika ukanda wa Afrika.
Dkt. Kisenge alisema
mkutano huo umelenga kutengeneza mikakati ya kushirikiana na Serikali ili
kuondoa vikwazo vinavyowafanya watoto kushindwa kupata matibabu kutokana na
gharama, ikiwemo kuimarisha upatikanaji wa rasilimali fedha na kuendeleza
ajenda ya bima ya afya kwa wote.
“Wadau hawa pia wamekusudia
kubadilishana uzoefu na ujuzi kwa kutumia mafanikio yaliyopatikana JKCI kama
mfano wa kuigwa katika nchi nyingine huku wakijenga uwezo wa wataalamu kupitia
mafunzo ya kugundua mapema magonjwa ya moyo kwa watoto na kuimarisha tafiti
zitakazosaidia kubaini sababu za magonjwa hayo pamoja na njia za kuyazuia”,
alisema Dkt. Kisenge
Kwa upande wake
Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt.
Naizihijwa Majani alisema mkutano huo umekuwa jukwaa muhimu lililowakutanisha
wadau wa sekta ya afya nchini pamoja na washirika wa maendeleo kutoka Marekani
kwa lengo la kuandaa mpango madhubuti wa kitaifa wa kuhudumia watoto wenye
magonjwa ya moyo.
Dkt. Naizihijwa alisema
kupitia uzoefu wa washirika hao Tanzania itaweza kuimarisha mfumo wa utoaji wa
huduma ili kuhakikisha watoto wanaohitaji matibabu wanayapata kwa haraka, kwa
ubora na kwa uhakika bila kujali mahali walipo.
Naye Mkurugenzi
Msaidizi Magonjwa Yasiyoambukiza kutoka Wizara ya Afya Dkt. Omary Ubuguyu alisema
mkutano huo umejikita katika kujadili magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo pamoja
na yale yanayotokea baada ya kuzaliwa ambayo mara nyingi hayapewi kipaumbele
vya kutosha.
Dkt. Ubuguyu alisema baada
ya mkutano huo wadau hao wametoka na maazimio matatu muhimu ikiwemo kuweka
mikakati ya pamoja ya kupata rasilimali fedha, wataalamu na vifaa vya tiba
kuanzia ngazi ya jamii hadi hospitali za rufaa, kuboresha mifumo ya kugundua
wagonjwa ya moyo katika hatua za awali ili watoto waweze kupata huduma mapema,
na kuunda timu ya uratibu itakayosimamia utekelezaji wa maazimio yote
yaliyofikiwa.
Akihitimisha Makamu wa
Rais Mkakati wa Kimataifa na Utetezi Shirika la Children’s HeartLink Bistra
Zheleva alisema shirika hilo limekuja Tanzania kushirikiana na Wizara ya Afya
na JKCI katika kupanua huduma za magonjwa ya moyo kwa watoto na magonjwa ya
moyo ya kuzaliwa nayo.
Bistra alisema lengo
kuu la ushirikiano huo ni kuhakikisha huduma za moyo zinawafikia watoto wote
nchini kwa wakati ili kila mtoto mwenye ugonjwa wa moyo apate matibabu stahiki,
aishi maisha yenye afya na aweze kufikia uwezo wake kamili.
“Kupitia ushirikiano
huu tuliouanzisha na Tanzania tumepata nafasi kubwa ya kujenga mfumo imara na
endelevu wa huduma za moyo kwa watoto ambao unaweza kuwa mfano kwa nchi
nyingine Barani Afrika”, alisema Bistra





Comments
Post a Comment