Klabu ya Mazoezi ya Xtreme Workout Bootcamp watembelea wodi ya watoto JKCI
WATOTO wawili wanaosubiri matibabu katika
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamekatiwa bima ya afya na mabalozi wa
klabu ya mazoezi ya Xtreme Workout Bootcamp.
Mabalozi hao mapema leo wamefanya usafi wa
mazingira ya jengo la watoto, wamewatembelea baadhi ya watoto waliolazwa wodini
kuwajulia hali na kuwagawia zawadi mbalimbali pamoja na kuwaombea dua kwa
Mwenyezi Mungu.
Akizungumza na waandishi wa habari Mratibu wa
shughuli hiyo, Felix Chengule amesema waliona vema kutumia kipindi hiki cha
sikukuu ya Eid Al-Adha kutoa walichojaliwa na Mwenyezi Mungu na kuwaonesha
upendo watoto wenye uhitaji.
“Kipindi hiki cha sikukuu kibinadamu watu
wengi huwa wanajifikiria wenyewe, familia zao na furaha zao wenyewe lakini kuna
watu ambao wanakosa vitu hata kidogo kama upendo.
“Ukiacha mahitaji mengine kama malazi, wapo
wanaokosa upendo, hivyo tukaona tuje tujitoe kwa wenzetu, badala ya sisi
kusubiri kupewa, tutoe tulichojaliwa,” amesema.
Ameongeza “Tumekuja, tumefanya usafi,
tumekata bima kwa watoto wawili na kugawa zawadi ikiwamo miswaki na dawa za
meno, sabuni za kufulia na kuogea, taulo za kina mama penseli na zawadi
nyinginezo.
“Zawadi tulizotoa ni chache, tulitamani kutoa
nyingi zaidi hasa bima ya afya, tukipata watu wa kutuunga mkono tutafurahi
zaidi, hivi tulivyotoa tumechangishana, tunakaribisha watu wengi zaidi
tushirikiane hasa vijana waje tufanye mazoezi pamoja,” alisema.
Akizungumza, Msanii Nguli wa Muziki wa Bongo
Flavor kutoka kundi la Wanaume Halisi TMK, Kassim Ally (Sir Juma Nature) ambao
ni mabalozi wa Klabu hiyo, amesema wamejifunza mambo mengi kwa kufanya ziara
hiyo ya kuwajulia hali wagonjwa.
“Hospitalini ni sawa na kwenda mahakamani
ukienda huko ujue tayari ni shida, wasanii wengi wanajisahau hii ni kama
‘primary school’ (shule ya msingi), hapa shida zote zipo mwisho wa siku lazima
uje.
“Ni sehemu ya kutakiana faraja, kuna watu
wanaumwa hawana msaada, sisi tumekuja hapa leo naamini tumetumwa na Mwenyezi Mungu
tuje kuwaona,” amesema Sir Nature.
Ameongeza “Leo ni mwanzo, TMK imerudi,
tumeona tuanze hospitalini, tuwaone, tuwajulie hali wenzetu waliolazwa,
wanaendeleaje.
Amesema TMK tayari imeanza kuandaa nyimbo
mbalimbali ikiwamo zinazotoa elimu kwa jamii kuhusu masuala ya afya. Ipo chini
ya ‘carpet’, unajua msanii ukitembea ndiyo unatunga, ukikaa nyumbani huwezi
kutunga, tumefika, tumejionea, tutapeleka ujumbe,” amesisitiza.
Kwa upande wake Msanii Amani Temba
amewahimiza wasanii wengine na vijana kujenga utamaduni wa kuwakumbuka wagonjwa
na wenye mahitaji mengine.
“Wodini, nimewaona watu wana hali ngumu,
imenigusa mpaka nimelia, tuwakumbuke wahitaji,” amesema Temba.
Msanii Dollo Francis amesema ni muhimu pia
watu kutenga muda wa kumshukuru Mwenyezi Mungu wanapoamka wazima kwani wapo
wanaougua, wamelazwa hospitalini.
“Maisha yetu ni mafupi, ukiamka mzima ujue
kuna mwingine amelazwa hospitalini, kutoa ni moyo na sisi tumeguswa, tukafika
Taasisi ya Moyo na kujitolea tulichojaliwa,” alisema Msanii Dollo
Naye Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Husna Mzunga amewashukuru wanachama wa klabu ya mazoezi ya
Xtreme workout bootcamp kwa kuwa mfano wa kuigwa katika jamii kwa kuwakumbuka
watoto waliolazwa, kuwajulia hali, pamoja na kuwapatia zawadi.
Comments
Post a Comment