Madaktari wazawa wabadilisha mshipa wa damu uliotanuka na Valvu yake
Kwa mara ya kwanza madaktari wazawa mabingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya
damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamefanya upasuaji wa kubadilisha
mshipa mkubwa wa damu (Aorta) uliokuwa umetanuka pamoja na valvu yake (Aortic
valve insufficiency) bila ya usimamizi wa madaktari kutoka nje baada ya miaka
kadhaa ya kujifunza upasuaji huo kutoka kwa wataalam wenzao wanaofika JKCI kwa
ajili ya kubadilishana uzoefu.
Upasuaji
huo unaojulikana kwa jina la kitaalamu la Bentall Surgery uliochukua masaa matano kukamilika ulifanyika hivi
karibuni ambapo mgonjwa anaendelea vizuri na anatarajia kuruhusiwa wakati
wowote kuanzia sasa.
Mgonjwa
huyo alikuwa anasumbuliwa na maumivu ya kifua na baada ya uchunguzi aligundulika
kuwa mshipa mkubwa wa damu (aorta) unaotoa damu kutoka kwenye moyo na kusambaza
damu mwili mzima umepanuka sana na valvu yake ya moyo inavuja damu.
Akizungumzia
upasuaji huo Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Upasuaji wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Godwin
Sharau alisema tatizo hilo mara nyingi huwapata
watu wengi wenye umri wa kuanzia miaka ya 50 kwenda juu lakini pia uwapata watu
wanaosumbuliwa na shinikizo la damu la muda mrefu hivyo mshipa huo kupoteza
umahiri wake wa kuweza kustahimili presha.
Dkt.
Sharau ambaye pia ni daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto alisema kwa
mgonjwa ambaye hatapata matibabu husika kwa wakati mshipa huo huendelea
kutanuka na hivyo kupelekea kufa ghafla.
“Kwa
miaka mingi upasuaji wa Bental operation kwa hapa JKCI umekuwa ukifanyika
lakini chini ya usimamizi wa madaktari wenzetu kutoka nje ya nchi, sasa
wataalam wetu wameonesha umahiri mkubwa wa kufanya upasuaji huu. Hii ni hatua
nzuri sana katika Taasisi yetu”, alisema Dkt. Sharau.
“Upasuaji
wa kubadilisha mshipa mkubwa wa damu (Aorta) uliotanuka pamoja na valvu yake huchukua
muda mrefu kutokana na ubadilishaji wa mishipa lakini pia baada ya upasuaji huu
mgongwa anaweza akavuja damu kwa wingi na wakati mwingine kupoteza maisha”,
alisema Dkt. Sharau.
Kwa
upande wake Mkuu wa Idara ya upasuaji watu wazima wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Evarist Nyawawa alisema mgonjwa huyo baada ya kufanyiwa
uchunguzi wa kina ilionesha yakuwa mshipa mkubwa wa damu (Aorta) ulikuwa
umetanuka kiasi cha kwamba muda wowote ungeweza kupasuka.
“Mgonjwa
tuliyemfanyia upasuaji wa mshipa wake mkubwa wa damu (Aorta) pamoja na valvu
yake (Aortic valve) iliyokuwa inarudisha damu kwenye chemba ya kushoto ya moyo
ilikua inamfanya mgonjwa akose nguvu na kushindwa kupumua vizuri”, alisema Dkt.
Nyawawa.
“Sasa tuna uzoefu mkubwa naamini tutaendelea
kuokoa maisha ya watanzania wengi ambao wanahitaji upasuaji kama huu, na hii
itapunguza wagonjwa kwenda nje ya nchi kwa ajili ya kutafuta huduma za kibingwa
za matibabu ya moyo”, alisema Dkt. Nyawawa.
Naye
Mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji wa kubadilisha mshipa mkubwa wa damu (aorta)
uliotanuka pamoja na valvu yake (Bental operation) Benny Mongi aliwashukuru wataalamu hao wa JKCI na kuwapongeza kwa
kutumia utaalam wa hali ya juu waliokuwa nao kwa kuokoa maisha yake.
“Nimeambiwa
huduma kama hii niliyofanyiwa na madaktari wa JKCI haikuwahi kufanyika kupitia
madaktari wazawa lakini kwangu wameweza, nikirejea nyumbani baada ya matibabu
haya naenda kutoa ushuhuda wa huduma hii niliyoipata hapa hapa Tanzania ili
watanzania wenzangu wafahamu na kutumia vizuri rasilimali zetu ambazo serikali
yetu imetuwekea”,.
“Nimekuwa
nikitafuta hewa kwa mikono kutokana na matatizo ya moyo niliyokuwa nayo, sikuwa
naweza kupumua kabisa mikono yangu muda wote ndio ilikua ikinisaidia
kujipulizia ili nipate hewa, sitaacha kumshukuru Mwenyezi Mungu na wataalam
hawa kwa kuokoa maisha yangu”, alisema Mongi.
Kwa
kipindi cha mwezi mmoja wa Oktoba hadi Novemba 2021 madaktari wazawa mabingwa waupasuaji
wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wamefanya
upasuaji wa kubadilisha mshipa mkubwa wa damu (aorta) uliokuwa umetanuka pamoja
na valvu yake (Aortic valve insufficiency) bila ya usimamizi wa madaktari
kutoka nje ya nchi kwa mgonjwa mmoja na upandikizaji wa mishipa ya damu ya moyo
bila ya kusimamisha moyo kwa wagonjwa watatu.
Comments
Post a Comment