Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) yaanzisha kliniki maalum kwa wagonjwa wa sikoseli wanaokabiliwa na magonjwa ya moyo
Mwakilishi wa Mganga mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Ayoub Kibao, Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi na Mkuu wa Idara ya Tiba wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) ambaye pia ni Mkuu wa Utafiti katika programu ya sikoseli na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Figo, Paschal Ruggajo wakikata utepe kuashiria ufunguzi wa kliniki maalum ya wagonjwa wenye sikoseli ambao pia wanakabiliwa na magonjwa ya moyo iliyoko katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam.
Na
Mwandishi Maalum – Dar es Salaam
16/09/2020 Kliniki maalum kwa ajili ya
kuhudumia wagonjwa wa sikoseli ambapo wanaokabiliwa pia na magonjwa ya moyo
imeanzishwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Akizungumza wakati wa uzinduzi wa kliniki
hiyo, Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI, Pro. Mohamed Janabi amesema wameshirikiana
na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) kupitia Programu
yake ya Sikoseli.
Prof. Janabi, amesema juhudi za kuianzisha
kliniki hiyo zilianza takribani miaka miwili iliyopita na kwamba inalenga
kuboresha huduma za matibabu ya wagonjwa hao.
Amesema JKCI kila wiki huwa tunawaona kwenye
kliniki zetu na kwamba kabla ya kuanzisha kliniki hiyo ilimlazimu mgonjwa
anayehudhuria kliniki ya sikoseli anayegundulika kuwa na shida ya moyo,
kuelekezwa JKCI ili kwenda kupangiwa tarehe ya kuanza kliniki ya moyo.
“Tukaona ni adha kubwa kwao, maana yake
analazimika kuhudhuria kliniki mbili. Sikoseli ni ugonjwa wa damu, mtu mwenye
sikoseli yupo kwenye uwezekano wa kupata magonjwa ya moyo, japo si wote ambao
huishia kupata magonjwa ya moyo, lakini mtu akiwa na ugonjwa wa moyo hawezi
kupata sikoseli,” amebainisha.
Ameongeza “Kwa sababu sikoseli wenyewe ni
ugonjwa ambao mtu anaupata kwa kurithi vinasaba kutoka kwa wazazi, uhusiano
wake na magonjwa ya moyo ni kwamba sikoseli ni tatizo la kwenye damu, wagonjwa
wa sikoseli hukabiliwa na upungufu wa damu, hali hii inaweza kuleta athari
kwenye moyo na hata viungo vingine vya mwili.
“Kunapokuwa na upungufu wa damu, maana yake
mwili unakuwa na damu chache lakini moyo bado hulazimika kupiga zaidi ili
kuisukuma.
“Sasa neno ‘circle’ limetokana na vile visu
vya kunolea mpunga (mundu), yaani zile chembe chembe za damu huwa hazipo kwenye
muundo wa kawaida wa duara, zinapokuwa kwenye umbo la mundu ‘zina-tendency’
(tabia) ya kugandisha damu.
“Damu inapoganda inaweza kuziba kuziba
mishipa ya damu na hali hiyo huwa haichagui itokee wapi, ikiganda kwenye
mishipa iliyopo kwenye moyo ndipo uhusiano na magonjwa ya moyo unapotokea,
wengne hupata pia ugonjwa wa kiharusi,” amebainisha.
Ameongeza “Zile changamoto zinazotokea kwenye
damu ndiyo zinaleta athari kwenye moyo, kwa hiyo sikoseli ndiyo inasababisha
ugonjwa wa moyo, lakini mnoyo wenyewe hauwezi kusababisha sikoseli.
“Hivyo, wataalamu tulishauriana na
kukubaliana kuanzisha kliniki hii maalum kwa wagonjwa hawa kwa sababu ni
magonjwa yanayoingiliana, mgonjwa atakapokuja ataweza kuonwa na madaktari wa
magonjwa yote mawili kwa wakati mmoja,” amesisitiza.
Amebainisha kutokuwa na kliniki ya wagonjwa
wa sikoseli kwa upande wa watoto pia watu wazima na kwamba watafanyiwa vipimo
vyote vya moyo na damu na kupatiwa dawa kadri itakavyoshauriwa.
“Tumeanza na sikoseli, siku zijazo dhumuni
letu ni kufikia hatua ya kuanzisha kliniki moja kwa magonjwa yanayoingiliana
kwa mfano moyo na figo, au moyo na kisukari, kumrahisishia mgonjwa kuhudumiwa
na kumuepushia adha ya kukimbizana huku na kule, kufuata huduma,” amesema.
Mkuu wa Idara ya Tiba wa Muhas ambaye pia ni
Mkuu wa Utafiti wa Muhas katika programu ya sikoseli na Daktari Bingwa wa
Magonjwa ya Figo, Paschal Ruggajo amesema kliniki hiyo itawasaidia pia
wataalamu kujadiliana na kufanya tafiti zaidi ili kuimarisha na kuboresha tiba
za wagonjwa wa sikoseli.
Mwenyekiti wa Chama cha Wagonjwa wa Sikoseli
Nchini, Arafa Said amepongeza hatua hiyo na kubainisha kwamba gharama za matibabu
bado ni changamoto kubwa inayowakabili.
“Wengi wetu hawana bima ya afya na wapo
wanaokata tamaa na kuacha kuhudhuria kliniki, tunaendelea kujitahidi kutafuta
wafadhili, ili kuwasaidia,” amesema.
Akizungumza, Mwakilishi wa Mganga Mkuu wa
Mkoa wa Dar es Salaam, Dk. Ayoub Kibao amewahamasisha watanzania kukata bima ya
afya kwani inasaidia kupunguza mzigo wa gharama za matibabu.
“Takwimu zinaonesha nchini kila mwaka watoto 8000 hadi 11,000 huzaliwa na ugonjwa huu, nawashauri hasa vijana wanaotaka kuingia kwenye ndoa, wapime ili kujua iwapo wamebeba vinasaba vya ugonjwa huu ama la,” ameshauri.
Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) wakimsikiliza mgeni rasmi Dkt. Ayoub Kibao aliyemwakilisha mganga mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa kliniki maalum ya wagonjwa wenye sikoseli ambao pia wanakabiliwa na magonjwa ya moyo iliyoko katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam.Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) wakimsikiliza mgeni rasmi Dkt. Ayoub Kibao aliyemwakilisha mganga mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam wakati wa uzinduzi wa kliniki maalum ya wagonjwa wenye sikoseli ambao pia wanakabiliwa na magonjwa ya moyo iliyoko katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam.
Mwakilishi wa Mganga mkuu wa mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Ayoub Kibao akizungumza jambo wakati akikagua chumba cha kufanyia kipimo cha kuangalia umeme wa moyo (Electrocardiogram) katika kliniki maalum ya wagonjwa wenye sikoseli ambao pia wanakabiliwa na magonjwa ya moyo iliyoko katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam.
Mwakilishi wa Mganga mkuu
wa mkoa wa Dar es Salaam Dkt. Ayoub Kibao akimsikiliza daktari bingwa wa
magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Naiz
Majani akielezea kuhusu mashine ya kuchunguza
jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiogram) iliyopo katika kliniki maalum ya wagonjwa wenye sikoseli ambao pia wanakabiliwa na magonjwa ya moyo
iliyoko katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akizungumza jambo na Dkt. Emmanuel Balandya ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Masomo ya Elimu ya juu wa Chuo Kikuu cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) na Mkuu wa Idara ya Tiba wa MUHAS ambaye pia ni Mkuu wa Utafiti katika programu ya sikoseli na Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Figo, Paschal Ruggajo mara baada ya kumalizika kwa ufunguzi wa kliniki maalum ya wagonjwa wenye sikoseli ambao pia wanakabiliwa na magonjwa ya moyo iliyoko katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam.
Wafanyakazi wa Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Chuo Kikuu
cha Afya na Sayansi Shirikishi Muhimbili (MUHAS) wakiwa katika picha ya pamoja
mara baada ya kufunguliwa kwa kliniki
maalum ya wagonjwa wenye sikoseli
ambao pia wanakabiliwa na magonjwa ya moyo iliyoko katika Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete jijini Dar es Salaam.
Picha na JKCI
Comments
Post a Comment