Watu wengi waliojitokeza kupima magonjwa ya moyo wilayani Kigamboni wamebainika kuwa na shinikizo la juu la damu. Kati ya watu 173 waliopimwa 58 wamethibitika kuwa na tatizo hilo

 

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Zitha Meela akimpima kiwango cha oxygen mwilini mtoto aliyefika katika viwanja vya Hospitali ya wilaya ya Kigamboni kwa ajili ya upimaji wa magonjwa ya Moyo uliofanywa na  wataalamu wa Taasisi hiyo kwa kushirikiana na wenzao wa Kigamboni ikiwa ni maadhimisho ya siku ya moyo Duniani

Jumla ya watu 173 wamefanyiwa upimaji wa magonjwa ya moyo wakati wa maadhimisho ya siku ya moyo Duniani yaliyofanyika katika viwanja vya Hospitali ya wilaya ya Kigamboni iliyopo Gezaulole.

Upimaji huo uliofanywa na wataalamu wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana  na wenzao wa Hospitali ya wilaya ya Kigamboni.

Watu wote 173 walifanyiwa vipimo vya kuangalia uwiano wa urefu na uzito, wingi wa sukari kwenye damu na shinikizo la damu, waliokutwa na viashiria vya magonjwa ya moyo walifanyiwa vipimo zaidi ambapo  124 walifanyiwa vipimo vya kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiogram - ECHO) na mfumo wa umeme wa moyo (Electrocardiogram – ECG).

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka JKCI Baraka Ndelwa alisema baada ya kufanyika kwa vipimo vya  ECG na  ECHO watu 58 walikutwa na  matatizo mbalimbali ya moyo ikiwemo  shinikizo la juu la damu ambalo halijadhibitiwa na 12 kati yao  walipewa Rufaa ya kwenda kutibiwa JKCI na  Hospitali ya Taifa Muhimbili.

“Watu 115 hawakukutwa na matatizo yoyote yale ya moyo hivyo basi tuliwapa ushauri wa jinsi ya kutunza mioyo yao ili wasipate magonjwa ya moyo ambayo ni magonjwa yasiyo ya kuambukiza na mtu akifuata ushauri wa wataalamu na mtindo bora wa maisha ataweza kuyaepuka”,.

“Wagonjwa tuliowapa  rufaa ni wale waliokutwa  na matatizo ya kutanuka kwa moyo,  dalili ya kansa ya koo,  tatizo la mfumo wa chakula, matatizo ya mishipa ya damu ya moyo  na  magonjwa ya valvu za moyo”, alisema Dkt. Ndelwa.

Dkt. Ndelwa alisema kuna baadhi ya wagonjwa ambao waliwaona walikuwa na tatizo la shinikizo la juu la damu zaidi ya 198 ambalo halijadhibitiwa  inawezekana ni kutokana na mtu kutokufahamu kama anatatizo hilo au alitumia dawa za moyo na kuacha kuzitumia.

Akizungumza na wananchi waliofika katika upimaji huyo Mkuu wa wilaya ya Kigamboni Mhe. Fatma Nyangasa aliishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kutoa wataalamu wake na kwenda kufanya upimaji kwa wakazi wa wilaya hiyo.

Mhe. Fatma aliwahimiza wananchi hao kufuata maelekezo ya wataalamu na kuyafanyia kazi kwani hakuna elimu nyingine ya magonjwa ya moyo watakayoipata tofauti na watakayopewa na wataalamu wa afya.

“Fursa hii ya matibabu mliyopata ni adimu kupatikana kwani wataalamu wamewafuata huku mnakoishi,  ninawasihi wakati mwingine zitakapotokea fursa kama hizi mjitokeze kwa wingi ili mpate huduma za matibabu”, alisema Mhe. Fatma.

Aidha Mhe. Fatma alimuagiza Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya wilaya ya Kigamboni  kuhakikisha dawa za magonjwa yasiyo ya kuambukiza ikiwemo za ugonjwa wa moyo zinapatikana katika Hospitali hiyo ili wagonjwa wanaotibiwa hapo wapate dawa hizo kabla hawajaenda kutibiwa katika Hospitali za Taifa.

Kuhusu ugonjwa wa  UVIKO -19 alisema ni tatizo la Dunia nzima na kuwahimiza wananchi kuchanja ingawa suala la kuchanja ni la hiari kwani wataalamu wamethibitisha chanjo hiyo ni salama na watumie fursa ya kusogezewa chanjo katika maeneo yao kuchanja kwa kufanya hivyo  watakuwa salalama.

Kwa upande wao wananchi waliopata huduma ya kufanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo bila malipo waliishukuru Serikali kwa kuwasogezea huduma hiyo ya kibingwa na kuomba huduma kama hizo ziwe zinatolewa mara kwa mara.

“Wanangu walisikia wataalamu wanakuja kupima wakanileta, baada ya kufanyiwa vipimo nimekutwa na tatizo la kutanuka kwa moyo sikuwa nafahamu kama ninatatizo hilo nimepewa dawa za kutumia kwa muda wa siku 10 pamoja na rufaa ya kwenda kutibiwa katika Taasisi ya Moyo”, alisema mzee  Crosteri Tarubera.

Katika upimaji huo kampuni za uagizaji na usambazaji wa dawa za binadamu na vifaa tiba za Samiro Pharmaceutical Ltd na Ajanta Pharma Ltd zilitoa dawa bila malipo kwa watu waliokutwa na matatizo ya moyo.

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Wafanyakazi waliohama JKCI waagwa