DC Ubungo, msanii wa mziki G Nako wahamasisha wananchi kujua Namba Zao za Afya

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimpima shinikizo la damu msanii wa Bongo Fleva George Mdemu almaarufu kama G Nako alipofika katika Taasisi hiyo tawi la Oysterbay kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Albert Msando pamoja na msanii wa bongo fleva George Mdemu almaarufu kama G Nako alipofika katika Taasisi hiyo tawi la Oysterbay kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya. 

Mtaalamu wa Maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) tawi la Osterbay Jesca Mlay akimtoa damu msanii wa bongo fleva George Mdemu maarufu kama G Nako alipofika katika Taasisi hiyo tawi la Oysterbay kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya. 

Picha Na JKCI
***************************************************************************************************************************************************************

Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Albert Msando amewahimiza wananchi kuwa na utamaduni wa kupima afya zao mara kwa mara ili kujua namba zao mapema na kupata matibabu sahihi kwa wakati.

Rai hiyo imetolewa jana na Mhe. Msando alipotembelea Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) tawi la Osterbay akiwa ameongozana na msanii wa Bongo Fleva George Mdemu almaarufu kama G Nako kwa ajili ya kufanya vipimo vya afya na kujua namba zake.

Mhe. Msando alisema wananchi wanapaswa kuchukulia uzito suala la afya zao na kuhakikisha wanafahamu namba zao ili waweze kupata ushauri na matibabu kwa wakati.

“Kama tunavyofahamu sasa hivi taasisi yetu ya JKCI wanaendesha kampeni ya kuhamasisha kila mwananchi kufahamu namba zake na mimi nimeongozana na G Nako kwa ajili ya kufanya vipimo na kufahamu namba zake”, alisema Mhe. Msando

Aidha Mhe. Msando alimpongeza msanii huyo kwa kuitikia wito wa kushirikiana na JKCI katika kuhamasisha jamii kuhusu umuhimu wa kupima afya mara kwa mara.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema Taasisi hiyo imeendelea kuwafikia wananchi katika maeneo mbalimbali lengo likiwa ni kuiwezesha jamii kufahamu afya zao.

“Leo tumetembelewa na Mkuu wa Wilaya ya Ubungo Mhe. Albert Msando na mwanamuziki G Nako ambaye amekuja kwa ajili ya kupima afya yake na kujua namba zake, ni muhimu wasanii wakaiga mfano wake na kujitokeza kupima kuepuka madhara yanayoweza kujitokeza kama hawatapima afya zao mara kwa mara”, alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge alisema JKCI imekuwa ikipanua huduma zake kwa kuzisogeza karibu na wananchi, kutoa huduma kwa makundi mbalimbali ikiwemo wasanii, wanamichezo, waandishi wa Habari, na makundi mengine yaliyopo katika jamii.

Akizungumzia umuhimu wa kufanya uchunguzi wa afya msanii wa Bongo Fleva George Mdemu almaarufu kama G Nako alisema wananchi hususan wasanii wanapaswa kuwa na utamaduni wa kupima afya zao mara kwa mara pale wanapopata nafasi.

“Kuna wakati tunaona baadhi ya wasanii wanaanguka wakiwa katika steji, kuna wengine wamekuwa wakipata matatizo ya shinikizo la damu  lakini kuna ambao hawajui wingi wa sukari yo kwenye damu, uzito au wingi wa mafuta kwenye damu hivyo ni muhimu kufanya uchunguzi wa afya kabla ya kupata maradhi”, alisema G Nako.

Kampeni ya JKCI ya kuhamasisha wananchi kujua namba zao za afya inaendelea kuwa sehemu ya juhudi za taasisi hiyo katika kuelimisha jamii kuhusu umuhimu wa kuchunguza afya na utambuzi wa mapema wa changamoto mbalimbali za kiafya.



 

Comments

Popular posts from this blog

Serikali yazindua kitabu safari ya upandikizaji wa moyo Tanzania, JKCI yaweka historia mpya ya huduma za kibobezi

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma