Watu 204 wamefanyiwa upimaji wa magonjwa ya moyo bila malipo katika maadhimisho ya siku ya Shinikizo la Juu la Damu Duniani
Afisa Muuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Joseph Katoto akimpima urefu na uzito mkazi wa Mbezi Luis wakati wa upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wakazi wa Wilaya ya Ubungo na vitongoji vyake katika kuadhimisha siku ya Shinikizo la Juu la Damu Duniani jana katika Ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam. Jumla ya wananchi 204 wamefanyiwa upimaji wa magonjwa ya moyo bila malipo.
Mkuu wa Kitengo cha Uhusiano na Mawasiliano wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Anna Nkinda akigawa vitabu vya mfumo bora wa maisha kwa wananchi wa Ubungo waliojitokeza kupima magonjwa ya moyo wakati wa upimaji wa moyo kwa wakazi wa Wilaya hiyo katika kuadhimisha siku ya Shinikizo la Juu la Damu Duniani jana katika Ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam.
Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Husna Faraji akitoa elimu ya lishe kwa wakazi wa Wilaya ya Ubungo waliojitokeza kupima magonjwa ya moyo wakati wa upimaji wa moyo kwa wakazi wa Wilaya hiyo katika kuadhimisha siku ya Shinikizo la Juu la Damu Duniani jana katika Ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam.
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Aloyce Mohamed akimpima jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiograph) mkazi wa Ubungo wakati wa upimaji wa magonjwa ya moyo kwa wakazi wa Wilaya ya Ubungo na vitongoji vyake katika kuadhimisha siku ya Shinikizo la Juu la Damu jana katika Ofisi za Mkuu wa Wilaya ya Ubungo jijini Dar es Salaam. Jumla ya wananchi 204 wamefanyiwa upimaji wa magonjwa ya moyo bila malipo.
Na: JKCI
Watu 204 wamefanyiwa
upimaji wa magonjwa ya moyo bila malipo katika maadhimisho ya siku ya Shinikizo
la Juu la Damu Duniani yaliyofanyika jana katika viwanja vya ofisi ya
Mkurugenzi wa manispaa ya Ubungo iliyopo Mbezi Luis eneo la Luguluni jijini Dar
es Salaam.
Upimaji huo wa siku moja ulifanywa na wataalamu wa Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete(JKCI) kwa
kushirikiana na wenzao wa manispaa ya Ubungo.
Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam
daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Samwel Rweyemamu alisema
upimaji uliofanyika ni wa kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi
(Echocardiography-ECHO), umeme wa moyo (Electrocardiography-ECG), urefu, uzito,
Shinikizo la Damu (PB) na kiwango cha sukari mwilini.
“Kati ya watu tuliowapima 30 hadi 40 walikuwa na shida ya shinikizo
la juu la damu ambalo lilisababisha misuli yao ya moyo kutanuka na wote hawa
hawakuwa wanajijua kama wanamatatizo mbalimbali katika mioyo yao”,.
“Wengine tuliowapima tuliwakuta wanashida kwenye Valvu, moyo
kutanuka, umeme wa moyo, matundu kwenye moyo na mmoja alikuwa na shida ya mshipa
mkubwa unaosambaza damu sehemu zote za mwili (Aorta) ulikuwa umevimba. Huyu
tuliyemkuta na matundu kwenye moyo ni mtu mzima wa miaka 45”, alisema Dkt.
Rweyemamu.
Kwa upande wake Mganga Mkuu wa manispaa ya Ubungo Dkt. Peter
Nsanya aliishukuru Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kuona umuhimu wa
kuadhimisha siku hiyo na kwenda kufanya upimaji wa magonjwa ya moyo bila malipo
kwa wananchi wa manispaa ya Ubungo na vitongoji vyake.
Dkt. Nsanya alisema katika upimaji huo wananchi waliojitokeza
kupima ni kutoka wilaya za Ubungo, Ilala, Kinondoni, Temeke na Kigamboni na wengine walitoka mkoa wa
Pwani na kulikuwa na huduma ya msaada wa kijamii kwa watu waliokuwa wanahitaji
huduma hiyo.
“Kila mwananchi alipimwa wingi wa sukari mwilini, urefu na
uzito na wengine ambao walionekana kuwa na dalili za ugonjwa wa moyo walifanyiwa
vipimo zaidi. “Waliofanyiwa kipimo cha ECHO walikuwa 133, ECG 75, waliopewa
dawa walikuwa 132 na 34 walikutwa na matatizo yaliyohitaji matibabu ya kibingwa
hivyo basi walipewa rufaa ya kwenda kutibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI)”,.
“Kati ya watu 204 ambao tuliwafanyia upimaji ni 38 tu
hawakukutwa na matatizo yoyote yale ya moyo hivyo basi ninawaomba wananchi
wanaposikia mahali kunafanyika upimaji wa magonjwa yoyote yale wajitokeze kwa
wingi kupima ili kujuwa kama wanamatatizo au la na kama wanamatatizo wataanza matibabu mapema”, alisisitiza Dkt. Nsanya.
Naye Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Husna Faraji alisema katika upimaji huo
walitoa elimu ya lishe bora kwa wananchi na kuwaeleza umuhimu wa lishe katika
afya zao wao binafsi na familia zao.
“Nilipata muda wa kutoa ushauri nasaha kwa mtu mmoja mmoja wengi wa niliowaona walikuwa na tatizo la uzito uliokithiri na
hawakuwa wanatambua kuwa ni tatizo katika afya zao. Wengine walikuwa hawajijui
kama wanashida ya shinikizo la juu la damu
na walikuwa wanatembea na kufanya shughuli zao kama kawaida”.
“Tulitoa elimu ya matumizi sahihi ya chumvi katika chakula na
mlo kamili kwa mgonjwa wa shinikizo la damu, umuhimu wa lishe na uhusiano wa
magonjwa yasiyo ya kuambukiza na lishe bora”, alisema Husna.
Alimalizia kwa kusema kuwa wanawake wengi walikuwa na shida
ya uzito mkubwa ukilinganisha na wanaume hiyo ni kutokana na aina ya vyakula
wanavyokula kabla na baada ya
kujifungua.
Nao wananchi waofika katika upimaji huo waliishukuru Serikali
kwa huduma hiyo na kuwaomba wataalamu
hao wawe wanatoa huduma ya upimaji bila malipo mara kwa mara kwa kufanya hivyo
kutawasaidia wananchi wasio na uwezo kiuchumi kupata huduma za matibabu ya kibingwa
kirahisi zaidi.
“Mimi nilifika hapa kwa ajili ya kufanya upimaji wa magonjwa
ya moyo baada ya kupima nimekutwa na tatizo la moyo kutanuka. Nashukuru
nimepewa dawa za kutumia za mwezi mmoja pia nimepewa rufaa ya kwenda kutibiwa
katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete ninaenda kumjulisha mme wangu ili
tujipange na kwenda kutibiwa huko”, alisema Halima Hussein mkazi wa Kibaha.
“Ninashukuru nimefanyiwa vipimo bila malipo yoyoye yale
bahati mbaya nimekutwa na shida ya umeme wa moyo nimepewa dawa za kutumia pamoja
na rufaa ya kwenda kutibiwa JKCI pia wataalamu wameniambia nisikate tamaa nitatibiwa na kupona maradhi
haya”,alishukuru Joseph Mushi mkazi wa Kimara .
“Mimi nimefanyiwa vipimo sijakutwa na shida yoyote ile ya
moyo, nashukuru nimepata elimu ambayo imenifanya kuelewa ni jinsi gani nitaweza
kuutunza moyo wangu na kuepuka kupata magonjwa
haya hii ikiwa ni pamoja na kufanya mazoezi na kuepuka kula vyakula vyenye
mafuta mengi na chumvi nyingi”, alisema Baraka Suleiman mkazi wa Temeke.
Katika upimaji huo kampuni za uagizaji na usambazaji wa dawa
za binadamu za Phillips pharmaceuticals Ltd, Ajanta Pharma na Astra Pharma (T)LTD zilitoa dawa bila malipo kwa
wananchi waliokutwa na matatizo ya moyo, kisukari na kikohozi.
Kauli
mbiu ya siku ya shinikizo la juu la Damu Duniani kwa mwaka huu ni : “Pima Shinikizo la damu; Ishi maisha marefu”.
Comments
Post a Comment