Serikali yaombwa kutoa elimu kinga ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza ikiwemo umuhimu wa kudumisha afya ya akili kwa wanafunzi wa shule za msingi na sekondari
Watu wanaoishi na
magonjwa yasiyoambukiza wakiuliza maswali wakati wa mafunzo ya kutoa
uelewa wa magonjwa hayo yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano
wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) uliopo jijini Dar
es Salaam. Mafunzo hayo ya siku moja yaliandaliwa na Shirikisho la Vyama vya
Magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA) ambapo washiriki walikuwa 30 kutoka
mikoa mbalimbali.
Watu wanaoishi na
magonjwa yasiyoambukiza wakiuliza maswali wakati wa mafunzo ya kutoa
uelewa wa magonjwa hayo yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano
wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) uliopo jijini Dar
es Salaam. Mafunzo hayo ya siku moja yaliandaliwa na Shirikisho la Vyama vya
Magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA) ambapo washiriki walikuwa 30 kutoka
mikoa mbalimbali.
Msaikolojia tiba kutoka Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH)
Idara ya Afya na magonjwa ya akili Isaac Lema akitoa mada ya afya ya akili
kwenye mafunzo ya kutoa uelewa wa magonjwa yasiyoambukiza kwa watu wanaoishi na
magonjwa hayo yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi ya
Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu
(NIMR) uliopo jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya Magonjwa yasiyoambukiza
Tanzania (TANCDA) Prof Andrew Swai akitoa mada ya mtindo bora wa maisha kwenye
mafunzo ya kutoa uelewa wa magonjwa yasiyoambukiza kwa watu wanaoishi na
magonjwa hayo yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa mikutano wa Taasisi
ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu
(NIMR) uliopo jijini Dar es Salaam.
XXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXXX
Serikali imeombwa kutoa elimu kinga ya magonjwa yasiyo ya
kuambukiza ikiwemo umuhimu wa kudumisha afya ya akili kwa wanafunzi wa shule za
msingi na sekondari kwa kufanya hivyo kutawasaidia kutambua umuhimu wa afya na
kufanya uchunguzi wa magonjwa hayo na
kuziendea huduma mapema zaidi.
Ombi hilo limetolewa hivi karibuni na Msaikolojia tiba kutoka
Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH) Idara ya Afya na magonjwa ya akili Isaac
Lema wakati akitoa mada kwenye mafunzo ya kutoa uelewa wa magonjwa yasiyoambukiza
kwa watu wanaoishi na magonjwa hayo yaliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi
wa mikutano wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) uliopo jijini Dar es Salaam.
Lema alisema matatizo ya afya ya akili yanatokana na mtu kuwa
na kiwango kikubwa cha msongo wa mawazo, na watu wengi wanaokabiliwa na matatizo
haya wanakaa kimya na kutowashirikisha watu wa karibu yao au wataalamu
hivyo kuwafanya kupelekea mabadiliko ya
kitabia, kihisia, kifikra na mwitikio wa mwili.
“Wapo wanaokata tamaa ,kuwa na majonzi, kushindwa kudhibiti
hisia kama vile hasira. Kwa upande wa tabia ni matumizi ya vilevi
yaliyopindukia, kukosa usingizi, kushindwa kujiamini na kutawaliwa na mawazo
hasi”,.
“Njia ya kuondokana na matatizo ya afya ya akili ni pamoja na
kudhibiti msongo kwa kufanya mazoezi kila siku, kujitofautisha yeye na tatizo
lake alilonalo, kumtofatisha mtu na
tatizo lililopo, kutafuta suluhu ya
migogoro uliyonayo au kutokuwa na migogoro. Kumbuka kila mtu hukabiliwa
na msongo hivyo tunapoutawala tunazuia msongo kujitokeza mara kwa mara au
kuwa endelevu”, alisema Lema.
Msaikolojia tiba huyo alisema
iwapo mbinu hizo hazitatoa unaafuu uliotarajiwa na iwapo msongo bado utakuwepo kwa kiwango
cha juu muhusika asisite kuwaona
wataalamu wa afya ya akili.
Lema alisema “Unapobakia kwenye matatizo hayo unaongeza hali
ya uhatarishi wa kupata dalili za ugonjwa wa akili kumbuka uwezo wa kufurahia
maisha hutokana na afya bora ya akili furaha ya maisha hutokana na afya bora ya
akili”,.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Shirikisho la Vyama vya
Magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA) Prof Andrew Swai alisema mwaka 2010
aligundulika kuwa na ugonjwa wa kisukari aina ya pili alitumia dawa aina mbili
ambazo ni za vidonge na sindano mara mbili kwa siku na akaamua kupunguza uzito
hadi kufikia kilo 60 kwani alikuwa na
uzito mkubwa zaidi ya kilo 70.
Prof. Swai alisema tangu mwaka 2011 alipopungua uzito
hajatumia tena dawa za kisukari kwani ugonjwa wa kisukari aina ya pili wengi
wanaupata wakiwa watu wazima. Ukiwa na ugonjwa aina hiyo unaweza kupona
kwasababu magonjwa yasiyo ya kuambukiza yanatokana na mtindo mbaya wa maisha wa
kutokufanya mazoezi na kula vyakula bila kufuata mpangilio lakini unaweza kuyaepuka kwa kufanya mazoezi na kula vyakula sahihi kwa
wakati sahihi.
“Tumeamua kuwafundisha watu wanaoishi na magonjwa yasiyoambukiza
ambayo ni moyo, sukari, pumu, saratani, magonjwa ya akili na selimundu ili wawe
na uelewa wa kutosha kuhusu magonjwa haya, kutokana na uchache wa wataalamu waliopo
njia mojawapo ya kutatua tatizo hili ni kuwatumia wagonjwa wenyewe kutoa elimu
kwa wenzao”,.
“Kuna wagonjwa ambao wameugua muda mrefu na wanauelewa wa
kutosha kuhusu magonjwa haya hivyo basi wagonjwa hawa wanaweza kuwafundisha
wagonjwa wengine kupitia kitabu cha mtindo wa maisha na magonjwa yasiyoambuliza
ambacho kimeandaliwa na wataalamu wa magonjwa hayo”, alisema Prof.Swai.
Alisema mpango mwingine waliokuwa nao ni kuwafundisha
madaktari na wauguzi kutoka vituo vya
afya 500, kila kituo watawafundisha wauguzi wawili na madaktari wawili ambao watasaidia kuwafundisha wagonjwa wakati wanasubiri kupata huduma”, alisema
Prof. Swai.
Alizitaja changamoto wanayokabiliana nazo kuwa ni pamoja na upatikanaji
wa fedha ili waweze kutoa elimu kwa jamii kupitia vyombo vya habari kwa kuandaa
vipindi vya redio na televisheni ambavyo siyo bure vinahitaji kulipiwa, aliwaomba
wadau wa maendeleo waweze kushirikiana
na TANCDA ili waweze kuwafikia wananchi wengi zaidi.
Nao wagonjwa wanaosumbuliwa na magonjwa yasiyoambukiza
walisema katika upatikanaji wa matibabu watakutana na changamoto mbalimbalimbali ikiwa ni pamoja na kutokupewa
elimu ya kutosha kuhusu magonjwa hayo na
upatikanaji wa dawa hasa kwa wagonjwa wa kisukari.
Jenipher Kyala mkazi wa Mbezi Beach jijini Dar es Salaam alisema mwaka 2019 alipata tatizo la afya ya
akili ambalo lilitokana na msongo wa mawazo ya kazi aliokuwa nao hakumwambia
mtu yeyote kutokana na tatizo alilokuwa nalo kwani alijuwa ataweza kulitatua
yeye mwenyewe.
“Ninakumbuka kuna siku niliamka nikasikia ndani yangu kuna
msukumo wa kufanya kitu fulani, nilifanya vurugu nikiwa saluni ndugu zangu walinikamata
na kunipeleka Hospitali ya Taifa Muhimbiili (MNH) nikatibiwa na hivi sasa
nimepona kama unavyoniona kwani ugonjwa huu unatibika kama magonjwa mengine na watu wanapona na wanaendelea na maisha kama
kawaida”,
“Katika jamii yetu watu wanamsongo wa mawazo lakini hawaongei
ninawasihi muongee matatizo mliyonayo msijifungie na kufikiria kuwa mtaweza
kuyatatua nyinyi wenyewe. Changamoto kubwa niliyokutana nayo wakati ninaumwa ni
kutokubalika katika jamii kwani nilifukuzwa kazi kwa ajili ya ugonjwa. pia vigumu
kupata kibali cha kufanya jambo fulani”, alisema Jenipher.
Juma Bahati mkazi wa jijini Dar es Salaam alisema akiwa na umri wa miaka 14 alianza
kutokwa na jasho jingi, kunywa maji mengi na kupata haja ndogo mara kwa mara
hasa wakati wa usiku baada ya kufanyiwa vipimo mwaka 2009 aligundulika kuwa na ugonjwa wa kisukari aina ya kwanza hivi sasa anamiaka 12 anaishi na ugonjwa huo.
Bahati alisema watu
wengi katika jamii hawaamini kuwa mtoto mdogo anaweza kupata ugonjwa wa
kisukari na akipata ugonjwa huo wanaamini
wanaamini kuwa karogwa lakini ukweli ni kuwa hata watoto wadogo wanapata
ugonjwa huo kama alivyopata yeye.
“Wazazi wakiwa wanaenda kupima afya zao wawapime na watoto
ambao wameambatana nao kwani hata wao wanaweza kuwa na ugonjwa huo pia wakijua
wanasukari itawasaidia kupata tiba mapema:, alisema Bahati.
Naye Erick Mtei mkazi wa Kilimanjaro ambaye anasumbuliwa na
ugonjwa wa saratani ya pua alisema akiwa na umri wa miaka 19 alipata tatizo la
nyama za pua baada ya kwenda katika Hospitali ya Kanda ya KCMC alifanyiwa upasuaji lakini tatizo
likaendelea.
“Ninawashauri wananchi
wenzangu wakiona kuna kitu ambacho hakiko sawa katika miili yao waende
Hospitali kwa wakati kupima, mimi nilizembea kwenda kutibiwa mapema baada ya
kuona shida imezidi mwaka 2015 ndiyo nikaenda kutibiwa”,.
“Sasa hivi ninapata matibabu yangu katika Taasisi ya Saratani
ya Oceanroad ninaishukuru Serikali kwani dawa ziko za kutosha na hakuna
unyanyapaa wowote ninaoupata kutoka kwa watoa huduma za afya pamoja na jamii inayonizunguka”, alisema Mtei.
Mafunzo hayo ya siku moja yaliandaliwa na Shirikisho la Vyama
vya Magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA) ambapo washiriki ambao ni watu wanaoishi na magonjwa hayo
walikuwa walikuwa 30 kutoka mikoa ya Arusha, Kigoma, Tabora, Simiyu, Shinyanga,
Mwanza, Tanga, Kilimanjaro, Morogoro na Dar es Salaam.
Comments
Post a Comment