Wagonjwa 19 ambao mishipa yao ya damu ya moyo ilikuwa imeziba kwa asilimia 100 na kushindwa kupitisha damu na ambao valvu zao za moyo zilikuwa zimeziba wafanyiwa upasuaji mdogo

 

Madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Shirika la Madaktari Afrika lililopo nchini Marekani wakimzibua mgonjwa mshipa wa damu wa moyo uliokuwa umeziba kwa asilimia 100 na kutokupitisha damu kabisa (Complex Percutaneous Coronary Intervention – PCI) wakati wa kambi maalum ya ya matibabu ya moyo ya siku tano inayoendelea katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.
Madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Shirika la Madaktari Afrika lililopo nchini Marekani wakimzibua mgonjwa  Valvu ya moyo iliyokuwa imeziba na kushindwa kupitisha damu  (Balloon Mitral Valve -BMV) wakati wa kambi maalum ya matibabu ya moyo ya siku tano inayoendelea katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam. Mara nyingi matibabu ya aina hiyo yanafanyika JKCI kwa njia ya upasuaji mkubwa wa moyo wa  kufungua kifua.

******************************************************************************************************************************************************************************************************

Wagonjwa 19 ambao  mishipa yao ya damu ya moyo ilikuwa imeziba  kwa asilimia 100 na kushindwa kupitisha damu  na ambao valvu zao za moyo zilikuwa zimeziba wamefanyiwa upasuaji wa bila kufungua kifua kupitia tundu dogo linalotobolewa kwenye paja.

Upasuaji huo unafanyika kwa kutumia mtambo wa Cathlab (Catheterization Laboratory) ambayo ni maabara inayotumia mionzi maalum kwa ajili ya uchunguzi wa matatizo na tiba za magonjwa ya moyo.

Kati ya hao wagonjwa 15  ni wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba sehemu kubwa kwa asilimia 100 na haikuwa inapitisha damu kabisa wamefanyiwa upasuaji mgumu (Complex Percutaneous Coronary Intervention – PCI) na wanne ambao valvu zao zilikuwa zimezibwa na ilibidi wafanyiwe upasuaji mkubwa wa kufungua kifua na kuzibadilisha valvu hizo  wamezibuliwa valvu kwa njia ya upasuaji mdogo (Balloon Mitral Valve -BMV).

Akizungumzia kuhusu kambi hiyo ya siku tano ambayo ilianza tarehe 14 hadi 18 mwezi huu  daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka JKCI Peter Kisenge alisema wanafanya matibabu hayo kwa kushirikiana na wenzao kutoka Shirika la Madaktari Afrika lililopo nchini Marekani.

“Kwa kushirikiana na madaktari wenzetu ambao wanautaalamu mkubwa kuliko sisi wa kuzibua mishipa ya damu ya moyo ambayo imeziba kwa asilimia 100 na kushindwa kupitisha damu na valvu ambazo zimeziba hazipitishi damu vizuri  tumefanya matibabu kwa wagonjwa 19 ambao hali zao zinaendelea vizuri, kuna ambao wapo wodini  na wengine wamesharuhusiwa kurudi nyumbani”,.

“Moja ya sababu ya valvu za moyo kuziba kwa kiasi kikubwa na kushindwa kupitisha damu vizuri ni pamoja na kupata ugonjwa wa  mafindofindo na homa kali ambayo hupelekea kuharibu valvu na kuzisababishia kushikamana na kushindwa kupitisha damu, wagonjwa wa aina hii huwa tunawafanyia upasuaji mkubwa wa kufungua kifua lakini katika kambi wamefanyiwa upasuaji mdogo na kuzibuliwa valvu zilizoziba”, alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge aliongeza kuwa wagonjwa ambao valvu zao zilikuwa zimeziba kama wangepelekwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu mgonjwa mmoja ingemgharimu kulipia gharama ya matibabu zaidi ya shilingi milioni 20 lakini kwa kupata matibabu hayo hapa nchini mgonjwa amelipia shilingi milioni sita fedha ambazo kwa  wengi wao zimellipwa na bima za afya wanazozitumia  na pia mgonjwa anapata nafasi ya kuwa karibu na familia yake kipindi chote anachopatiwa matibabu.

Kwa upande wake Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Shirika la Madaktari Afrika Mazen Albaghdadi alisema mara nyingi wamekuwa wakifanya kambi za matibabu ya moyo ambapo kambi hizo zimekuwa zikienda sambamba na utoaji wa mafunzo kwa wataalamu waliopo JKCI pia  wamekuwa wakibadilishana ujuzi wa kazi jambo ambalo limeifanya JKCI kuweza kutoa huduma za kisasa na za kibingwa kwa wagonjwa.

“Tunapenda kuja JKCI mara kwa mara kubadilishana ujuzi na madaktari hawa kwani wamekuwa wakihamasika kujifunza vitu vipya kila wakati na kuvifanyia kazi,  na kuyafanya matibabu ya moyo kuwa ya kibingwa hapa Tanzania”, alisema Dkt. Mazen.

Naye Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Khuzeima Khanbai alisema Madaktari kutoka Shirika la Madaktari Afrika wapo kwa ajili ya kuwaongezea  ujuzi wa kazi wataalamu wa JKCI  ili waweze kupata mbinu mpya za kutoa huduma kwa kutumia njia za kisasa kwa wagonjwa wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba kwa kiwango kikubwa  na wale wenye matatizo ya valvu za moyo zilizoziba.

“Ujuzi tulioupata katika kambi hii umetuwezesha kutumia njia maalum ambazo zimeweza kutufikisha katika moyo kupitia tundu dogo linalotobolewa kwenye paja na kuweza kuzibua mishipa ya damu pamoja na Valvu zilizoziba. Mafunzo tunayoyapata katika kambi hii tutaendelea kuyafanyia kazi”, alisema Dkt. Khuzeima .

Nao wagonjwa waliopata huduma ya matibabu katika kambi hiyo walishukuru kwa huduma waliyoipata na kuipongeza Serikali kwa kujenga Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete, kuhakikisha inavifaa tiba vya kisasa na kuwasomesha wataalamu wa magonjwa ya moyo.

Christopher Taji mkazi wa Kinondoni jijini Dar es Salaam alisema alikuwa akisumbuliwa na tatizo la moyo lililomfanya kushindwa kulala usingizi mzuri kwa muda mrefu kutokana na maumivu makali aliyokuwa anayapata  katika eneo la kifua.

“Nilipofika JKCI madaktari walinifanyia vipimo na kugundua mishipa ya damu kwenye moyo wangu imeziba hivyo kunishauri nifanyiwe upasuaji wa kuzibua mishipa hiyo na sasa nimeshafanyiwa upasuaji ambao madaktari wamekiri kuwa umefanyika kwa mafanikio makubwa”,.

“Sasa nalaa vizuri bila kusikia maumivu yoyote, madaktari wangu wamefanya kazi kubwa sana, nawashukuru kwa kujitoa kwao kwa ajili yangu. Wito wangu kwa jamii pale wanapopata changamoto yoyote ya kiafya wafike katika hospitali zetu kwani huduma za kibingwa zinapatikana”, alisema Christopher

Ally Mahamud mkazi wa Mombasa jijini  Dar es Salaam alisema alikuwa na tatizo la  kuziba kwa  mishipa ya damu ya moyo kwa muda mrefu baada ya kuzibuliwa  kumeondoa kabisa maumivu makali  aliyokuwa akiyapata  kabla ya kufanyiwa  upasuaji huo.

Sitaacha kuwashukuru madaktari waliookoa maisha yangu tena kwa dharura kwani nililetwa hapa kwa dharura nikiwa na hali mbali na maumivu makali lakini leo nipo hapa naongea kwa furaha nikiwa sina maumivu yoyote, Mungu awabariki kwa kazi hizi ngumu wanazofanya madaktari na wauguzi za kuokoa maisha yetu”, alisema  Mahamud.

Katika kambi hiyo maalum ya matibabu wataalamu hao mabingwa wa magonjwa ya moyo na wazibuajji wa mishipa ya damu ya moyo wanatarajia kufanya upasuaji kwa wagonjwa 19 wenye matatizo ya mishipa ya damu ya moyo iliyoziba kwa asilimia 100 na wagonjwa 6 wenye matatizo ya valvu za moyo ambazo zimeziba na hazipitishi damu vizuri.


 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari