Serikali yaombwa kuyaingiza magonjwa yasiyoambukiza katika bima ya afya kwa watu wote
Katibu wa Shirikisho la Vyama vya magonjwa yasiyoambukiza
Tanzania (TANCDA) Prof. Kaushik Ramaiya akizungumza na wadau wa afya
walioshiriki katika uzinduzi wa mkakati wa bima ya afya kwa wote inayojumuisha
magonjwa yasiyoambukiza uliofanyika hivi karibuni katika Hoteli ya Protea
jijini Dar es Salaam. Walioshiriki katika uzinduzi huo ni wadau mbalimbali wakiwemo wizara ya Afya, wajumbe wa kamati ya
kudumu ya bunge ya masuala ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Dawa za kulevya na Magonjwa
yasiyoambukiza, Kamati ya kudumu ya bunge ya huduma na maendeleo ya jamii, watu
wanaoishi na magonjwa yasiyoambukiza na wahariri wa habari.
Picha na Henrick Chiwangu
**************************************************************************************************************************
Serikali imeombwa kuingiza matibabu ya magonjwa
yasiyoambukiza katika bima ya afya kwa wote ili kupunguza changamoto zinazowapata
watu wanaoishi na magonjwa yasiyoambukiza kwani tathmini iliyofanywa na Shirika
la Afya Duniani (WHO) inaonesha zaidi ya asilimia 45 ya vifo vinavyotokea
duniani hutokana na magonjwa hayo.
Ombi hili limetolewa hivi karibuni na Katibu wa Shirikisho la
Vyama vya magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA) Prof. Kaushik Ramaiya
wakati wa uzinduzi wa mkakati wa utetezi juu ya bima ya afya kwa watu wote inayojumuisha
magonjwa yasiyoambukiza uliofanyika katika Hoteli ya Protea jijini Dar es
Salaam.
Prof. Ramaiya alisema mfuko wa Taifa wa bima ya afya una bima
za aina mbalimbali ambazo zimekuwa zikitoa huduma za matibabu ya magonjwa
yasiyoambukiza pamoja na magonjwa mengine, lakini baadhi ya huduma za matibabu
hazipatikani katika bima hizo na hivyo kuwanyima fursa wagonjwa kupata huduma
iliyokamilia wanapofika hospitali kupata matibabu.
“Magonjwa yasiyoambukiza yanagharama kubwa katika kuyatibu, kupitia
mfuko wa Taifa wa bima ya afya wananchi wamekuwa wakikata bima za afya za aina
mbalimbali lakini kadi hizo zimekuwa zikitoa baadhi ya huduma, na huduma
nyingine kama dawa, upasuaji na vifaa kutokuwepo katika bima hivyo kuwanyima
fursa wagonjwa ya kupata matibabu kamili”,.
“Ninaiomba Serikali iliangalie hili kwani tathmini
iliyofanywa na WHO inaonesha baada ya miaka mitano hadi kumi ijayo vifo
vinavyotokana na magonjwa yasiyoambukiza vinaweza kuongezeka na kuwa zaidi ya
asilimia 55”,
“Magonjwa yasiyoambukiza yasipotibiwa vizuri hupelekea mtu
kupata madhara mengine kama vile kudhuru figo, mishipa ya damu, macho, kupata
kiharusi na madhara mengine mengi ambayo humsababishia mtu kupoteza uhai wake”,
alisema Prof. Ramaiya.
Aidha Prof. Ramaiya aliiomba Serikali kuratibu upatikanaji wa
matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza katika maeneo yote yenye zahanati na vituo
vya afya ili jamii iweze kupata huduma maeneo ya karibu na kwa wakati hivyo
kupunguza madhara yanayoweza kutokea kama magonjwa hayo hayatatibiwa mapema.
“Kama wagonjwa wenye magonjwa yasiyoambukiza watapata huduma
za matibabu kwa wakati katika vituo vya karibu vya afya wataweza kuendelea na
shughuli zao za kiuchumi hivyo kukuza vipato vyao na pato la taifa”,.
“Jamii inapaswa kujikinga na magonjwa haya yasiyoambukiza
kwani utafiti uliofanywa na WHO unaonesha kila dola moja unayoiweka katika
kinga dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza unapata nafuu ya dola 7 hadi 12 kwa kila
dola uliyotumia kuwekeza katika kinga”, alisema Prof. Ramaiya
Kwa upande wake Mbunge wa Jimbo la Mbozi Mkoa wa Songwe Mhe.
George Mwenisongole alisema suala la bima ya afya kwa wote likawe ajenda ya
kitaifa ili kutoa fursa kwa kila mtanzania kuwa na matumaini ya kupata matibabu
pale wanapougua magonjwa mbalimbali.
“Bima ya afya kwa wote inapaswa kuwa bima isiyobagua lakini
bima inayotoa huduma zote za matibabu ili watanzania wafaidike na huduma za
matibabu hasa wale wenye magonjwa yasiyoambukiza ambayo yamekuwa yakitibiwa kwa
gharama kubwa”,
“Nimepata nafasi ya kushiriki semina iliyoandaliwa na TANCDA
na kujifunza mengi kuhusiana na magonjwa yasiyoambukiza, wito wangu kwa Serikali
ni kuhakikisha tunapata sera ya kitaifa ya kupambana na magonjwa yasiyoambukiza
ambayo itaweza kuzuia uvutaji wa sigara hadharani ili kuokoa maisha ya watu
wanaoathirika na moshi wa sigara”, alisema Mhe. Mwenisongole
Naye Mhariri wa Makala kutoka gazeti la Habarileo Gloria
Tesha aliiomba Serikali iwekeze katika elimu ya magonjwa yasiyoambukiza kuanzia
ngazi ya shule za msingi ili watoto wanapokuwa wawe na ufahamu wa kutosha juu
ya magonjwa hayo, hii itawasaidia kujikinga na magonjwa hayo.
“Waandishi wa habari tupo tayari kutumia kalamu zetu kupaza
sauti ili jamii ifahamu athari za magonjwa yasiyoambukiza na namna ambavyo
itaweza kujikinga na magonjwa hayo. Ninaiomba Serikali pamoja na taasisi
zinazojihusisha na mapambano dhidi ya magonjwa yasiyoambukiza kututumia ili
tuweze kuzifikia jamii na kuziokoa”,
“Wadau na Serikali kwa pamoja tukubaliane kupiga vita
magonjwa yasiyoambukiza kwa kuyafanya magonjwa haya kuwa ajenda ya kitaifa
katika kila kikao kinachofanyika kuanzia ngazi za mitaa, kata, wilaya na mikoa
ajenda hiyo ikipewe kipaumbele ninaamini tutaweza kupunguza ama kuyaondoa
kabisa magonjwa haya”, alisema Gloria.
Uzinduzi wa mkakati wa utetezi juu ya bima ya afya kwa watu
wote inayojumuisha magonjwa yasiyoambukiza uliandaliwa na Shirikisho la Vyama
vya magonjwa yasiyoambukiza Tanzania (TANCDA) na kushirikisha wadau
mbalimbali wakiwemo wizara ya Afya, wajumbe
wa kamati ya kudumu ya bunge ya masuala ya UKIMWI, Kifua Kikuu, Dawa za kulevya
na Magonjwa yasiyoambukiza, Kamati ya kudumu ya bunge ya huduma na maendeleo ya
jamii, watu wanaoishi na magonjwa yasiyoambukiza na wahariri wa habari.
Comments
Post a Comment