JKCI mbioni kushirikiana na Jamhuri ya watu wa Czech kutoa huduma za matibabu ya moyo
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akijadiliana na madaktari kutoka Hospitali ya Ostrava iliyopo Jamhuri ya Watu wa Czech namna ambayo watashirikiana katika kutoa huduma za matibabu ya moyo jana baada ya madaktri hao kutembelea JKCI Jijini Dar es Salaam
Madaktari kutoka Hospitali ya Ostrava iliyopo
nchini Czech na wenzao kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
wakifuatilia majadiliano wakati madaktari hao walipotembelea JKCI kwa ajili ya kuona
namna ya kushirikiana katika kutoa huduma za matibabu ya moyo jana katika ukumbi
wa Taasisi hiyo Jijini Dar es Salaam
Afisa Muuguzi wa Chumba cha wagonjwa
wanaohitaji uangalizi maalum (ICU) wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Prisca Kiyuka akiwaelezea namna ambavyo wagonjwa wanapatiwa huduma katika
chumba hicho madaktari kutoka Hospitali ya Ostrava iliyopo Jamhuri ya Watu wa
Czech walipotembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya kuona namna ambavyo wanaweza
kushirikiana katika kutoa huduma za matibabu ya moyo jana Jijini Dar es Salaam
Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ipo mbioni kuanzisha
ushirikiano katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa kushirikiana na
madaktari kutoka Hospitali ya Ostrava iliyopo Jamhuri ya Watu wa Czech.
Akizungumza baada ya kufanya ziara JKCI jana Jijini Dar es Salaam Mkuu
wa msafara wa madaktari sita kutoka nchini Czech Miroslav Homza amesema kuwa
lengo kuu wa madaktari hao kufika JKCI ni pamoja na kuangalia jinsi ambavyo wataweza
kushirikiana katika kutoa huduma za matibabu ya moyo ikiwa ni njia ya
kubadilishana uzoefu kati ya Tanzania na Czech.
“Tumefika hapa JKCI na kukutana na uongozi kujadilina juu ya
uwezekano wa madaktari kutoka JKCI na wale wa Hospitali ya Ostrava iliyopo
Jamhuri wa watu wa Czech kuweza kubadilishana uzoefu katika kutoa huduma za
matibabu ya moyo haswa upande wa upasuaji wa moyo”,
“Sambamba na kutoa huduma za matibabu ya moyo pia tutaangalia
namna gani tunaweza kushirikiana upande wa utafiti katika masuala ya magonjwa
ya moyo kati yetu na Tanzania”, alisema Homza.
Aidha Homza amesema kuwa katika ushirikiano huo Czech itaangalia kama
kuna uwezekano wa wagonjwa ambao wapo Tanzania na wanahitaji huduma za matibabu
ya kina kuchukuliwa na kupelekwa Jamhuri ya watu wa Czech kwa ajili ya matibabu
hayo kwani Czech inatoa huduma za matibabu ya hali ya juu na kwa gharama nafuu
tofauti na nchi nyingine duniani.
Akizungumzia ushirikianao wa kutoa huduma za matibabu ya moyo
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed
Janabi alisema kuwa JKCI imekua ikishirikiana na madaktari kutoka nchi
mbalibmali ikiwa ni sehemu ya kuongeza uzoefu na kutoa hudama bora na za
kibingwa za matibabu ya moyo.
“Leo tumepokea madaktari kutoka Jamhuri ya watu wa Czech ambao
wamefika kujadiliana nasi namna ambavyo tutashirikiana katika kubadilishana
uzoefu wa kutoa huduma za matibabu ya moyo, Tumekubaliana kuandaa makataba wa
makubaliano ambao utatuongoza katika kushirikiana na kufaidia katika
kubadilishana uzoefu huo”, alisema Prof. Janabi
Comments
Post a Comment