Wagonjwa 20 wafanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo katika kambi maalum ya matibabu iliyofanywa na madaktari wa JKCI na mwenzao kutoka Hospitali ya Max iliyopo nchini India


Madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na mwenzao kutoka Hospitali ya Max ya nchini India Dkt. Subhash Sinha wakimbadilisha mshipa mkubwa wa moyo  (Aorta) mgonjwa ambaye mshipa wake uliokua umetanuka zaidi ya sentimita 5  wakati wa kambi maalum ya matibabu ya moyo ya siku saba iliyofanyika katika Taasisi hiyo Jijini Dar es Salaam. Jumla ya wagonjwa 20 wamefanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo

Wataalam wa Afya kutoka Idara ya Upasuaji mkubwa wa Moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakiwa katika picha ya pamoja na Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kutoka hospitali ya Max iliyopo nchini India Subhash Sinha baada ya kumalizika kwa kambi maalum ya matibabu ya moyo ya siku saba iliyofanyika katika Taasisi hiyo Jijini Dar es Salaam.


Na: JKCI

*********************************************************************************************

Wagonjwa 20 wamefanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo wa kufungua kifua katika kambi maalum iliyofanywa na madaktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kutoka hospitali ya Max iliyopo nchini India na kumalizika jana Jijini Dar es Salaam.

Kambi hii maalum ya matibabu ya moyo iliyoanza tarehe 18 hadi 25 Aprili 2022 imefanyika kwa wagonjwa ambao mioyo yao ilikua imechoka na kiwango cha ufanyaji kazi wa moyo umeshuka chini ya asilimia 35%.

Akizungumzia kambi hiyo Mkurugenzi Idara ya Upasuaji JKCI Dkt. Angela Muhozya amesema kuwa wagonjwa 7 (saba) wamefanyiwa upasuaji  wa kubadilisha mshipa mkubwa wa moyo  (Aorta) uliokuwa umetanuka zaidi ya sentimita 5 (5cm)na hivyo kuwa katika hatari ya kupasuka wakati wowote na mgonjwa kupoteza Maisha.

““Upasuaji huu hufanyika kwa kuondoa sehemu iliyotanuka na kupandikiza kipande cha mshipa wa bandia (graft) inayoendana na ukubwa wa mshipa wa moyo wa mgonjwa (ascending aorta replacement) ambapo wagonjwa wote wanaendelea na matibabu na afya zao zinazidi kuimarika”, alisema Dkt. Angela

Aidha Dkt. Angela amesema kuwa pamoja na wagonjwa hao saba waliobadlilishiwa mishipa mkubwa wa moyo, wagonjwa wengine 13 wamepandikizwa mishipa iliyokuwa imeziba katika moyo (bypass) isiyopungua miwili.

“Wagonjwa tuliowapandiza mishipa niwale ambao walikuwa na mishipa zaidi ya miwili iliyoziba  lakini pia kiwango cha ufanyaji kazi wa mioyo yao  kilikuwa kimeshuka sana”,

“Tofauti ya mishipa hii tunayopandikiza na ile amboyo tumekuwa tukipandikiza siku zote ni kuwa wagonjwa wengi waliofanyiwa katika kambi hii wana kiwango kidogo cha ufanyaji kazi wa moyo yaani chini ya 35 (ejection fraction)” alisema Dkt. Angela

“Kama Taasisi tumeshaanza kidogo kidogo kufanya upasuaji wa kupandikiza mishipa kwa wagonjwa lakini tunapokutana na wagonjwa ambao mioyo yao imechoka sana tunahitaji utaalam zaidi wa kufanya upasuaji bila kuusimamisha moyo na ndio maana tumekuwa na kambi hii kwa ajili ya kupata mafunzo zaidi na kutoa huduma kwa wagonjwa wanaohitaji upasuaji wa kupandikiza mishipa.

“Naamini baada ya kambi hii madaktari wazawa wataweza kufanya upasuaji huu kwa wagonjwa ambao mioyo yao ina kiwango kidogo cha kufanya kazi chini ya 35 kwani hapo awali tulilazimika kuwafanyia kwa kusimamisha moyo au kuwatuma wagonjwa hao nje ya nchi” alisema Dkt. Angela

Kwa upande wake Daktari kutoka Hospitali ya Max iliyopo nchini India Subhash Sinha amesema kuwa hii ni mara yake ya tatu kufika na kushirikiana na madaktari wa JKCI kwa sababu maalum za kusaidia kuwafanyia upasuaji wagonjwa ambao mioyo yao inafanya kazi kwa kiwango kidogo yaani chini ya 35.

“Kila ninapokuja tumekua tukifanya upasuaji kwa wagonjwa kati ya 20 hadi 25 na wakati huu tumeweza kuwafanyia upasuaji wagonjwa 20 ambao walikua katika hali mbali kutokana na mioyo yao kufanya kazi kwa kiwango cha chini”,

“Idara ya upasuaji ya JKCI inakua kwa kasi katika kutoa huduma za upasuaji, Madaktari wanajituma sana katika kutekeleza majukumu yao ya kila siku na wamekua wepesi kupokea mbinu mpya tunazotumia katika upasuaji kila ninapokuja”, alisema Dkt. Sinha  

Naye Mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji mkubwa wa kufungua kifua katika kambi hiyo Abdalla Bakari Mkazi wa Dar es Salaam ameishukuru serikali ya awamu ya nne ya Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete kwa kuwa na wazo la kanzisha Taasisi ya Moyo hapa nchini ili kuweza kuwahudumia watanzania ambao wengi wao hawana uwezo wa kufuata matibabu ya moyo nje ya nchi.

“Nashindwa kuongea na haya machozi ninayoyatoa ni ya furaha baada ya kuona tatizo langu la mishipa ya damu iliyokua imeziba na kunipa changamoto za kuchoka mara kwa mara na kukosa pumzi wakati nikiwa naongea sasa limetatuliwa, Nawashukuru sana wataalam hawa waliojitoa kuokoa maisha yetu”,

“Uwepo wa Taasisi hii umeweza kuwasaidia watu wa maisha ya chini kupata huduma za matibabu ya moyo kupitia bima ya afya mimi nikiwa mmoja wao, naipongeza serikali ya awamu ya nne ya Mhe. Kikwete kwa kuanzisha Taasisi hii na serikali za awamu ya tano na sita kuendelea kuipa kipaumbele Taasisi hii ili sisi watu wakawaidi tuweze kupata huduma za kibingwa hapa nchini”, alisema Bakari. 

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari