JKCI kushiriki maonesho ya kimataifa nchini Comoro

 

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza kuhusu JKCI kushiriki maonesho ya kimataifa nchini Comoro

*********************************************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) inatarajia kushiriki maonesho ya bidhaa na huduma zinazozalishwa Tanzania yanatakayofanyika nchini Comoro kuanzia tarehe 10 hadi tarehe 20 Desemba mwaka huu.

Katika maonesho hayo Taasisi hiyo itaonesha huduma za kibingwa za matibabu ya moyo inazozitoa kwa wananchi wa Comoro.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt. Peter Kisenge alisema Taasisi hiyo imeona ni muhimu kushiriki katika maonesho hayo ili kutangaza huduma za kibingwa za matibabu ya moyo ambazo zimekuwa zikihitajika na watu kutoka nchini humo.

 Dkt. Kisenge alisema JKCI imeendelea kukuwa kwa kasi na kuwa bora Afrika Mashariki na kati hivyo kuifanya kuwa moja ya Taasisi kubwa inayotoa matibabu ya moyo na upasuaji wa moyo nchini Afrika.

“Sisi kama Taasisi tunaendelea kutoa huduma zetu kwa wananchi hapa Tanzania na sasa tunaenda kutoka nje ya mipaka ya Tanzania kuwafikia wagonjwa wa moyo katika nchi mbalimbali za Afrika ili nao wafaidike na huduma zetu na kupunguza gharama za kuwapeleka wagonjwa wao nchi zilizo nje ya bara la Afrika,”

 “Sambamba na kushiriki katika maonesho hayo tumejipanga kwenda nchini Comoro mwezi Februari 2023 kwa ajili ya kufanya kambi maalum ya matibabu ya moyo ili wananchi wa Comoro waweze kuona vizuri huduma zetu zilivyo na kutoa nafasi kwa wananchi hao kuchunguza afya zao,” alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge alisema kwa sasa JKCI inajulikana barani Afrika kwa kutoa huduma za kibingwa za matibabu ya moyo kwani hivi karibuni wanatarajia kumpokea Katibu Mkuu Wizara ya Afya wa nchini Zambia pamoja na Mkurugenzi wa Hospitali ya Moyo wan chi hiyo  kwa ajili ya kusaini mkataba wa kushirikiana katika kutoa mafunzo ya huduma zinazotolewa JKCI.

“Mkataba huo pia utahusisha makubaliano ya JKCI kupokea baadhi ya wagonjwa kutoka nchini Zambia ambao hapo awali walikuwa wanapelekwa nchini India ili waweze kupatiwa matibabu ya moyo hapa nchini,” alisema Dkt. Kisenge.

Dkt. Kisenge alisema mkakati wa kuvuka mipaka ya Tanzania unakusudia pia kuzifikia nchi za Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, Burundi na nchi nyingine barani Afrika ambazo kwa namna moja zitafaidika na huduma za kibingwa na bobezi za matibabu na upasuaji wa moyo zinazotolewa JKCI.

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Upasuaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema Taasisi hiyo imekuwa ikipokea wagonjwa kutoka nchi za jirani ikiwemo Visiwa vya Comoro hivyo sasa imeona ni muda muafaka wa wao kwenda na kuzitangaza huduma wanazozitoa katika nchi hizo.

Dkt. Angela ambaye pia ni daktari bingwa wa usingizi na wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum alisema kwa sasa JKCI inatoa huduma zote za dharura na huduma za matibabu ya moyo kwa masaa 24 ili kuweza kutoa huduma kwa wakati na kwa ufanisi mkubwa.


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari