Ngusa: Tumieni vizuri ujio wa madaktari bingwa wa moyo kuchunguza afya zenu
Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya
Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Nuru Letara akimwelezea Katibu Tawala Mkoa wa Lindi
Ngusa Samike huduma zinazotolewa kwa watoto wenye magonjwa ya moyo alipofika
katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi Sokoine (SRRH) kwa ajili ya kufungua
kambi maalum ya siku tatu ya matibabu ya moyo inayofanywa na wataalam wa afya
wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa SRRH. Wanne kutoka kushoto ni Mganga
Mfawidhi wa SRRH Dkt. Mohamed Muhaji
Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Khairoon
Mohamed akimfanyia uchunguzi mama ambaye amepata kiharusi wakati wa kambi
maalum ya siku tatu ya uchunguzi na matibabu ya moyo inayofanywa na wataalam wa
afya wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi
Sokoine (SRRH).
Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Josephat Katoto akimpima wingi wa sukari mwilini mwananchi wa mkoa wa Lindi
aliyefika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi Sokoine (SRRH) wakati wa
kambi maalum ya siku tatu ya uchunguzi na matibabu ya moyo inayofanywa na
wataalam wa afya wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa SRRH.
Na: JKCI
***********************************************************************************************************
Wananchi wa Mkoa wa Lindi wameombwa kutumia vizuri ujio wa
madaktari mabingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
kupata huduma za uchunguzi wa magonjwa ya hayo kwani mkoa wa Lindi upo mbali na
hospitali kubwa za kibingwa tofauti na ambavyo mikoa mingine ilivyo.
Rai hiyo imetolewa jana na Katibu Tawala Mkoa wa Lindi Ngusa
Samike alipofika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Lindi Sokoine (SRRH)
kufungua kambi maalum ya siku tatu ya uchunguzi na matibabu ya moyo inayoende
katika Hospitali hiyo.
Ngusa alisesma wananchi wa Lindi waliokuwa na hamu ya kufanya
uchunguzi wa magonjwa ya moyo sasa wamepata nafasi ambayo imewasaidia kupunguza
gharama za kufuata huduma hizo zinazopatikana nje ya Mkoa wa Lindi.
“Kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa wa Lindi Mhe. Zainab Telack
tunatoa shukrani zetu za dhati kwa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa ubunifu
wa hali ya juu kuendesha zoezi la kuwafikia wananchi kupata huduma za matibabu
ya moyo jambo ambalo linaleta thamani katika maisha ya binadamu”, alisema Ngusa
Ngusa alisema uelewa wa magonjwa mbalimbali kwa wananchi wa
Lindi upo chini hivyo mara nyingi wanapojisikia kusumbuliwa na matatizo tofauti
tofauti huona ni jambo la kawaida lakini kwa ujio wa wataalam kutoka JKCI kutawasaidia
wananchi hao kutambua magonjwa mbalimbali na kuona umuhimu wa kuchunguza afya
zao mara kwa mara.
Aidha Ngusa alisema Mkoa wa lindi ni mkoa wa tatu kwa ukubwa
ukiacha mkoa wa Tabora na Mkoa wa Morogoro hivyo kuwaomba wataalam kutoka JKCI wakati
mwingine wanavyoandaa matibabu kama hayo waufikirie Mkoa huo ulivyo na eneo
kubwa na kupeleka huduma eneo ambalo litawakutanisha wananchi wengi zaidi ili
wananchi hao waweze kufaidika.
“Kijografia jinsi Mkoa wetu ulivo ni ngumu sana kwa hapa
lindi mjini kuwapata wananchi wa Liwale, Ruangwa na Nachingwea ambapo idadi ya
watu ni kubwa zaidi katika Mkoa wetu hivyo tunawaomba kipindi kingine
mtakaporudi tena mjipange ili tuweze kutoa huduma kuendana na jografia ya eneo
letu na wananchi wengi zaidi wafaidike na huduma hizi”, alisema Ngusa
Kwa upande wake Mkurugenzi wa Kurugenzi ya Uuguzi wa Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Robert Mallya alisema JKCI imeweka mpango wa
kuzunguka mikoa mbalimbali ya Tanzania kusogeza huduma kwa wananchi ili waweze
kujitambua na kuchukua tahadhari mapema.
“Katika kambi za matibabu tunazozifanya tumekua na malengo
manne makubwa ambayo ni kuwafikishia huduma za matibabu ya moyo wananchi
walipo, kutoa elimu ya magonjwa hayo, kushirikishana uzoefu na wataalam wenzetu
wa afya pamoja na kufanya tafiti mbalimbali kuhusu magonjwa ya moyo kulingana
na maeneo na mikoa tunayotembelea”,
“Tunawaomba wananchi kubadilisha mfumo wao wa maisha ili
kuepukana na magonjwa haya yasiyoambukiza hasa magonjwa ya shinikizo la juu la
damu tatizo ambalo limeonekana kuwa kubwa kwani shinikizo la juu la damu
hupelekea moyo kutanuka, kupata kiharusi na kuleta shida nyingine nyingi katika
mwili wa binadamu”, alisema Mallya
Naye mwananchi aliyepatiwa huduma katika kambi hiyo maalum ya
matibabu ya moyo Amina Ngumbe amewaomba wataalam kutoka JKCI kufika katika Mkoa
huo mara kwa mara kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo kwani wananchi
wengi wanahitaji huduma hizo.
“Mimi mwenyewe nilikua nampango wa kwenda Taasisi ya Moyo
Jakaya Kikwete Dar es Salaam kwa ajili ya kufanyiwa vipimo vya moyo lakini
nilivyosikia wanakuja Lindi nikafarijika sana, Nawaomba waweke ratiba za
kutuhudumia mara kwa mara ili tusihangaike kuwafuata wakati tunaumwa”, alisema
Amina
Amina alisema kwa watalam hao kufika mkoani Lindi kunatoa motisha
kwa wananchi kuchunguza afya zao kwa wakati kwani mara nyingi wananchi wengi
huwa hawachunguzi afya zao hadi wanapozidiwa ndio hutafuta huduma za matibabu.
Mbali na wataalam wa JKCI waliofika katika Hospitali ya Rufaa
ya Mkoa wa Lindi Sokoine kutoa huduma za matibabu wataalam hao pia wanatoa
elimu ya namna ya kujikinga na magonjwa ya moyo pamoja na kubadilishana uzoefu
na wataalam wa afya wa Hospitali ya Sokoine kujenga uzoefu wa ndani wa kutoa
huduma hizo kwa wananchi.
Comments
Post a Comment