Watu 429 wafanyiwa uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo Mkoani Mtwara

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Ally Athuman akimpima wingi wa sukari mwilini mwananchi wa Mkoa wa Mtwara aliyefika katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini (SZRH) kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na matibabu ya moyo wakati wa kambi maalum ya siku tatu iliyokua ikifanywa na madaktari wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa SZRH na kumalizika jana kwa kuwafanyia uchunguzi na matibabu ya moyo wananchi 429.

Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Janeth Mmari akiwaelezea namna ya kujikinga na magonjwa ya moyo wananchi wa Mkoa wa Mtwara waliofika katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini (SZRH) kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na matibabu ya moyo wakati wa kambi maalum ya siku tatu iliyomalizika jana kwa kuwafanyia uchunguzi na matibabu ya moyo wananchi 429.

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Nuru Letara akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography – ECHO) mtoto aliyefika katika Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini (SZRH) kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na matibabu ya moyo wakati wa kambi maalum ya siku tatu iliyomalizika jana katika Hospitali hiyo. 


Baadhi ya wananchi wa Mkoa wa Mtwara wakiwa katika foleni ya kupatiwa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo wakati wa kambi maalum ya siku tatu iliyofanywa na wataalam wa afya kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini (SZRH) na kumalizika jana kwa kuwahudumia wananchi 429.

Na: JKCI
*****************************************************************************************************

Jumla ya watu 429 wamefanyiwa uchunguzi na matibabu ya moyo katika kambi maalum ya matibabu iliyofanywa na wataalam wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini (SZRH)

Kambi hiyo ya matibabu ya moyo iliyofanyika kwa siku tatu ilianza tarehe 28 hadi 30 Novemba 2022 kwa kutoa huduma za uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa watu wazima 408 pamoja na watoto 21

Akizungumzia kambi hiyo Mkuu wa Kitengo cha Utafiti na Mafunzo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Pedro Pallangyo alisema upande wa watu wazima ugonjwa wa shinikizo la juu la damu umeonekana kuwa tatizo kubwa kwani asilimia 51 ya watu wazima waliofanyiwa vipimo wamekutwa na tatizo hilo.

“Katika asilimia 51 ya watu wazima tuliowakuta na matatizo ya shinikizo la juu la damu asilimia 23 wamegundulika kwa mara ya kwanza wakati wa upimaji huu huku asilimia 28 ya waliokutwa na shinikizo la juu la damu walikuwa wanajitambua lakini tatizo hilo halikua likitibiwa vizuri hivyo wataalam wetu kuwabadilishia dawa ili presha zao ziwe vizuri”, alisema Dkt. Pedro

Dkt. Pedro alisema ugonjwa wa kutanuka kwa moyo na ugonjwa wa kuziba kwa mishipa ya damu ni miongoni mwa magonjwa ambayo yalifuatia kuwa na watu wengi kwa upande wa watu wazima.

“Kwa upande wa watoto jumla ya watoto 21 wamefanyiwa vipimo vya moyo kati yao watoto 17 wamekutwa na matatizo mbalimbali ya moyo yakiwemo matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo yaliyogundulika kwa watoto 15”,

“Tumetoa rufaa kwa wagonjwa 73 kufika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa lengo la kufanyiwa matibabu ya juu zaidi ya uchunguzi na matibabu ya mishipa ya damu na kwa upande wa watoto kufanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo na upasuaji wa kutumia tundu dogo ili kuweza kuziba matundu kwenye mioyo yao na kurekebisha kasoro ambazo wamezaliwa nazo”, alisema Dkt. Pedro

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Hospitali ya Rufaa Kanda ya Kusini (SZRH) Dkt. Herber Masigati ameushukuru uongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete kwa kuwezesha wataalam mabingwa wa magonjwa ya moyo kufika SZRH kwa ajili ya kuwahudumia wananchi wa Mkoa wa Mtwara ambao walikua na kiu kubwa ya kupatiwa uchunguzi na matibabu ya moyo.

Dkt. Masigati alisema hali ya magonjwa ya moyo mkoani Mtwara inaonekana kuwa kubwa kutokana na kliniki mbalimbali zinazofanywa na Hospitali hiyo kliniki inayohudumia wagonjwa wengi kuwa ni ile yenye wagonjwa wa Kisukari, Shinikizo la damu pamoja na magonjwa ya moyo hivyo kupitia kambi hiyo kutaongeza zaidi idadi ya wagonjwa wa moyo katika kliniki zao.

“Mwitikio wa wananchi kufika katika kambi hii umekuwa mkubwa, wagonjwa ni wengi wanaohitaji huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo na huu ni mwanzo wakufikisha huduma za kibingwa kwani hatutaishia hapa bali kila tutakapopata nafasi tutaendelea kushirikiana”, alisema Dkt. Masigati

Naye mkazi wa Mtwara Pudensiana Sungura alisema amepata taarifa kupitia vyombo vya habari kuhusu ujio wa madaktari bingwa wa magonjwa ya moyo hivyo kutokana na hali yake ya kusumbuliwa mara kwa mara na shinikizo la juu la damu akaona ni vyema kutumia nafasi hiyo ili aweze kufanyiwa uchunguzi zaidi.

“Nina tatizo la shinikizo la juu la damu, tatizo la sukari na kuna wakati nasikia moyo wangu ukiuma, nashukuru nimefika hapa nimepata huduma nzuri za kufanyiwa vipimo kuangaliwa kama moyo wangu hauko vizuri lakini namshukuru Mungu majibu yametoka vizuri”,

“Wananchi wenzangu nawaomba tukisogezewa huduma karibu tusizipuuze kama hawa wenzutu wameamua kuacha shughuli zao na kutufuata kwanini sisi tushindwe kuacha shughuli zetu na kupatiwa matibabu ambayo labda bila wao kuja huku leo nisingekuwa najua afya ya moyo wangu”, alisema Pudensiana

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari