JKCI yaokoa milioni 951 matibabu ya wagonjwa 25 nje ya nchi

Madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo na Mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakishirikiana na mwenzao kutoka Hospitali ya Max iliyopo nchini India Dkt. Sinha Kumar kuvuna mshipa wa damu katika mguu wa mgonjwa utakaopandikizwa katika moyo wakati wa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya moyo kwa wagonjwa ambayo mioyo yao inafanya kazi kwa asilimia 17 hadi 45. Jumla ya wagonjwa 25 wamepatiwa matibabu katika kambi hiyo


 Madaktari bingwa wa upasuaji wa moyo na Mishipa ya damu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakishirikiana na mwenzao kutoka Hospitali ya Max iliyopo nchini India Dkt. Sinha Kumar wakipandikiza mshipa wa damu katika moyo wakati wa kambi maalum ya siku tano ya matibabu ya moyo kwa wagonjwa ambayo mioyo yao inafanya kazi kwa asilimia 17 hadi 45. Jumla ya wagonjwa 25 wamepatiwa matibabu katika kambi hiyo

Picha na: Khamis Mussa

****************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imeokoa zaidi ya shilingi milioni 951 ambazo Serikali ingetumia kama wagonjwa 25 wenye matatizo ya mishipa ya damu kuziba, matatizo ya hitilafu ya mfumo wa umeme wa moyo, matatizo ya moyo kwenda kasi na matatizo ya moyo kuchoka na kushindwa kufanya kazi wangepelekwa nje ya nchi kwa ajili ya matibabu

Wagonjwa hao ambao viwango vya ufanyaji kazi wa mioyo yao ni kuanzia asilimia 17 hadi 45 wamefanyiwa upasuaji katika kambi maalum ya siku tano iliyofanywa na madaktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya Max iliyopo nchini India.

Akizungumzia kambi hiyo Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema upasuaji wa moyo kwa wagonjwa hao umefanyika kwa ufanisi mkubwa lakini pia kutoa nafasi kwa wataalamu wa JKCI kujifunza namna ya kuwapatia huduma wagonjwa ambao mioyo yao ufanyaji kazi wake upo chini.

“Katika kambi hii tulijikita kuwafanyia upasuaji wagonjwa ambao viwango vya ufanyaji kazi wa mioyo yao imeshuka ambapo mgonjwa mmoja tuliyemfanyia upasuaji kiwango chake cha ufanyaji kazi wa moyo kilikuwa kimeshuka hadi asilimia 17”,

“Kadiri kiwango cha ufanyaji kazi wa moyo kinavyoenda chini upasuji wake unakuwa mgumu na matokeo yake huwa ya hatari, hivyo hawa wenzetu kutoka India wamekuwa wakifanya upasuaji kwa wagonjwa wa aina hii bila shida kutokana na uzoefu na vifaa walivyonavyo”, alisema Dkt. Angela

Dkt. Angela alisema gharama za upasuaji mkubwa wa moyo kwa mgonjwa mmoja akifanyiwa hapa nchini umgharimu shilingi milioni 16, lakini kama angeenda nje ya nchi ingemgharimu sio chini ya shilingi milioni 40.

Dkt. Angela aliongezea kuwa kwa upande wa upasuaji mdogo kwa kutumia mtambo wa Cathlab mgonjwa mmoja umgharimu kiasi cha shilingi milioni 29 lakini kama angeenda nje ya nchi ingemgharimu hadi shilingi milioni 80 kufanyiwa upasuaji wa moyo.

“Hapo awali wagonjwa ambao ufanyaji kazi wa mioyo yao ulikua umeshuka tulikuwa tunawapeleka nje ya nchi kwa ajili ya matibabu lakini tunavyoendelea kupata ujuzi wagonjwa hawa watakuwa wakipatiwa matibabu katika Taasisi yetu kwa ubora zaidi”, alisema Dkt. Angela

Kwa upande wake Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kutoka Hospitali ya Max iliyopo nchini India Sinha Subhash alisema wataalam wa JKCI wamekuwa na shauku ya kujifunza mambo mapya katika upasuaji wa moyo hivyo kuifanya Taasisi hiyo kukuwa kwa kasi.

“Nimekuwa nikiwafundisha njia tofauti za kufanya upasuaji wa kuzibua mishipa ya damu kwa wagonjwa ambao ufanyaji kazi wa mioyo yao ni wa asilimia ya chini na kwa madaktari wa hapa naona mabadiliko kwani sasa wanaweza kufanya hata bila ya kusimamiwa”, alisema Dkt. Sinha

Aidha Dkt. Sinha aliongezea kuwa kutokana na uhusiano mzuri alionao na watalaam wa JKCI ataendelea kushirikiana nao mara kwa mara kwani Tanzania imekua sehemu anayoiona kama nyumbani kwake.

Naye Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Dkt. Evarist Nyawawa alisema katika kambi hiyo wamewafanya upasuaji wagonjwa ambao mishipa yao ya damu ilikuwa imeziba  kwa kiwango kikubwa.

“Kutokana na uzoefu wa wataalam kutoka nchini India wamekuwa wakichagua wagonjwa ambao mishipa yao imeziba kwa kiwango kikubwa hivyo kufanya upasuaji wake kuwa mgumu tofauti na tunapokuwa peke yetu wakati mwingine huwaacha wagonjwa wa aina hiyo ili waende nje ya nchi kwa ajili ya matibabu”,

“Tumepata uzoefu wa kiwango kikubwa kuwahudumia wagonjwa ambao mishipa yao imeziba kwa kiwango kikubwa na utendaji wa kazi wa mioyo yao ni wa asilimia ndogo, tunawashukuru sana wataalam hawa kutushika mkono na kuweza kuhimili kuwatibu watanzania wenzetu”, alisema Dkt. Nyawawa


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari