Rais wa Zanzibar Dkt. Hussein Ali Mwinyi aipongeza JKCI kwa ubunifu wa kutoa kinga na tiba ya maradhi ya moyo nchini


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiagana na Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Dkt.Peter Kisenge, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mhe. Hemed Suleiman Abdulla na Naibu Waziri wa Afya Zanzibar Mhe.Hassan Khamis Hafidh, baada ya kumalizika kwa Matembezi ya Kuhamasisha Upimaji wa Moyo, Kufanya mazoezi “Tembea na JKCI Linda Afya ya Moyo Wako” na Ufungaji wa Kambi ya Upimaji wa Moyo iliyofanyika tarehe 23-27 Januari 2023 , katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja Unguja Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akiwa katika picha ya pamoja na viongozi mbalimbali pamoja na wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) mara baada ya kumalizika kwa Matembezi ya Kuhamasisha Upimaji wa Moyo, Kufanya mazoezi “Tembea na JKCI Linda Afya ya Moyo Wako” na Ufungaji wa Kambi ya Upimaji wa Moyo iliyofanyika tarehe 23-27 Januari 2023 , katika Hospitali Kuu ya Mnazi Mmoja Unguja Jijini Zanzibar.

*******************************************************************************************************************************************************************************************************************

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema magonjwa ya moyo yameongezeka kwa wingi na yanathiri afya za wananchi, utendaji kazi na uchumi wa nchi kwa ujumla.

 Dk. Mwinyi alieleza hayo wakati akifunga kambi ya upimaji wa moyo pamoja na matembezi ya kampeni maalum ya zuia magonjwa yasioambukiza yaliyoanza katika viwanja vya Maisara hadi viwanja vya Amani Stadium.

 Alisema kutokana na hali hiyo taifa limekuwa likitumia fedha nyingi za kigeni kugharamia matibabu ya moyo na magonjwa mengine nje ya nchi.

 Aidha alisema takwimu mbalimbali zilizokuwepo zinaonesha kuna ongezeko kubwa la magonjwa yasiambukuza hutokana na mfumo wa maisha na aina ya vyakula vinavyoliwa.

 Hivyo, aliipongeza Taasisi ya JKCI kwa mipango mizuri na ubunifu wa kinga na tiba ya maradhi hayo hapa nchini na kuendelea kuwajengea uwezo watumishi wa Zanzibar katika kutoa huduma.

 Aliwasihi kufika na kisiwa cha Pemba kwa ajili ya uchuguzi na kuhamasisha ufanyaji wa mazoezi kama njia bora ya kuimarisha afya za wananchi kwani wanahitaji huduma hizo kama walivyofanya Unguja.     

   Hivyo aliishauri taasisi hiyo kufikisha huduma hizo za upimaji kwa jamii pana zaidi kwani hatua hiyo itasaidia kupambana na matatizo mbalimbali ya kiafya ambayo jamii imekuwa ikikumbana nayo.

 Alisema hatua hiyo ya kufanya kambi za mara kwa mara katika mikoa ya pembezoni itapunguza wagonjwa wanaohitaji rufaa kwenda Dar es salam kwa matibabu na badala yake watatibiwa walipo.

 Akizungumzia utaratibu wa kuleta timu ya madaktari bingwa alisema ni utaratibu mzuri wa kuanza kujenga uwezo wa Zanzibar hasa katika hospitali ya Mkoa ya Lumumba kuona inaanza kutoa huduma za matibabu ya moyo.

 Hivyo aliiomba taasisi hiyo kutoa msaada kwa madaktari bingwa watakaonza katika hospitali hiyo ili waweze kujenga uwezo kuona jambo hilo linafanikiwa   

  Rais Mwinyi alisema ni matumaini yake kwamba kambi hiyo haitakuwa ya mwisho na wataendelea kutekeleza majukumu yao kikamilifu ili lengo la kuanzishwa kwa tasisi hiyo liweze kufikiwa.

 Hata hivyo, aliishauri taasisi hiyo kuendelea kuimarisha utendaji wao ili wananchi wengi waweze kunufaika na huduma bora wanazozitoa zenye kiwango cha kimataifa.

 Aliwasihi wananchi kuendelea kushiriki katika kambi mbalimbali za upimaji wa magonjwa na matembezi kama hayo kwani kufanya mazoezi ni kinga muhimu ya kujikinga na magonjwa mbalimbali hasa yasioambukiza.

 “Sote kwa pamoja tuhimizane kuwa na utamaduni wa kufanya mazoezi ili kuimarisha afya zetu na kuwa na utamaduni wa kupima afya mara kwa mara ili kubaini mapema kama tuna matatizo na kuchukua hatua za matibabu mapema,” alisisitiza. 

  Alimpongeza Mkurugenzi Mtendaji wa taasisi hiyo na wizara ya afya kuanzisha program hiyo ambayo inakuwa ni mfano mzuri kwa jamii kufanya mazoezi ili kujikinga na maradhi yasiambukiza. 

 Akimkaribisha Rais Mwinyi, Waziri wa Afya Zanzibar, Nassor Ahmed Mazrui alisema ipo haja ya kuwa na taasisi ya moyo hapa Zanzibar kwani kwa mwaka 2021/2022 jumla ya wagonjwa 584 wanaohitaji huduma tofauti na matibatu ya kibingwa walisafirishwa nje ya Zanzibar kati ya hao ugonjwa wa moyo unaongoza kwa rufaa ya asilimia 28.

 Alisema hadi kufikia Disemba 2022 jumla ya watoto 2030 walionekana kuwa na maradhi hayo huku waliofanyiwa upasuaji walikua 1,125 kati ya hao 800 walifanyiwa Izrael, 275 walifanyiwa India na 50 katika taasisi ya JKCI.

 Aidha alisema wastani wa watoto watatu hadi watano hufariki dunia kila mwezi katika hospitali ya Mnazimmoja na wastani wa kesi 110 mpaka 150 za watoto wapya hugundulika na magonjwa ya moyo kila mwaka katika hospitali hiyo huku gharama zinazotumika kutibu wagonjwa wa moyo Tanzania bara kwa mwaka ni milioni 650 hadi milioni 850.      

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete Dk. Peter Richard Kisenge, alisema taasisi hiyo imekuwa ikipata wagonjwa wanaotoka nchi mbalimbali ikiwemo Comoro, Zimbabwe, Malawi, Zaire na sehemu za Ulaya.

 Alibainisha kuwa mwaka 2021/2022 walipokea wagonjwa 1,087 kutoka Zanzibar huku wagonjwa 570 walilipiwa na serikali kupata huduma huku wagonjwa 519 walikuwa na bima za afya na wengine walijitolea wenyewe. 

 Aliipongeza serikali inavyojitoa katika kuwahudumia wananchi wa Zanzibar kwani matatizo ya magonjwa ya moyo hapa Zanzibar yanaongezeka kwa kasi kubwa.

 Hivyo alimuhakikishia Rais Mwinyi kuwa taasisi hiyo kwa kushirikiana na hospitali ya rufaa Mnazimmoja katika kutoa huduma hiyo kwani wanataka hospitali hiyo nayo iweze kutoa matibabu ya ubingwa wa moyo na hata kufanya upasuaji wa moyo.

 “Tunaweza kusimika mtambo wa Cathlab kufungua upasuaji wa moyo kwani Jakaya Kikwete ilianza kwa chumba katika hospitali ya mifupa Moy hivyo tutumie utaratibu huo huo kuanza katika hospitali ya Rufaa Mnazimoja,” alishauri.

 Mbali na hayo alisema taasisi hiyo imekuwa ikishirikiana na serikali kupitia wizara ya Afya kuhakikisha wananchi wanapata huduma za matibabu ya kibingwa ya magonjwa ya moyo kwa kufuata walipo na sasa wameshahudumia zaidi ya wagonjwa 3000. 

 Alisema katika kambi hiyo walihudumia wagonjwa 718 kati ya hao wagonjwa watu wazima walikuwa 627 na watoto 91 huku watu wazima 549 waligundulika na matatizo ya moyo huku rufaa 75 wakiwemo watu wazima 49 na watoto 26.

 Akizungumzia lengo la kuanzisha program ya tembea na Jakaya Kikwete Linda moyo wako alisema inalenga kuwahamisha wananchi kufanya mazoezi, ili kujikinga na magonjwa hayo yasioambukiza kwani karibu watu 17,000,000 wanapoteza maisha kutokana na matatizo hayo.      

 Aliahidi kwamba taasisi hiyo itaendelea kuhakikisha wananchi wanapata huduma bora za matibabu ya moyo na kutoa elimu kwa wananchi juu ya kujikinga na magonjwa hayo.

 


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari