Jamii yatakiwa kuchunguza afya mara kwa mara ili kuzuia magonjwa yasiyoambukiza

Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Edward Martin akiwafundisha wafanyakazi wa TATA Africa Holdings Limited umuhimu wa kupata vipimo na matibabu ya magonjwa ya moyo mapema wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya moyo iliyofanyika katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo vingunguti Dar es Salaam.

Fundi sanifu wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikiwete (JKCI) Renata Kulwa akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography - ECHO) mfanyakazi wa TATA Africa Holdings Limited wakati wa kambi maalum ya uchunguzi na matibabu ya moyo iliyofanyika katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo vingunguti Dar es Salaam.

Afisa Lishe wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Husna Faraji akimfundisha namna ya kuzingatia lishe bora mfanyakazi wa TATA Africa Holdings Limited wakati wa kambi maalum ya uchunguzi na matibabu ya moyo iliyofanyika katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo vingunguti Dar es Salaam.


Baadhi ya wafanyakazi wa TATA Africa Holdings Limited wakifuatilia elimu ya umuhimu wa kufanya uchunguzi wa afya na matibabu ya magonjwa ya moyo mapema iliyokuwa yakitolewa na daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Edward Martin wakati wa kambi maalum ya uchunguzi na matibabu ya moyo iliyofanyika katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo vingunguti Dar es Salaam.


Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wafanyakazi wa TATA Africa Holdings Limited wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo iliyofanyika katika ofisi za kampuni hiyo zilizopo vingunguti Dar es Salaam.

Na JKCI

***************************************************************************************************************

Jamii imetakiwa kujenga utaratibu wa kufanya uchunguzi wa afya mara kwa mara ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza ambayo mara nyingi hukua kimya kimya bila dalili za awali na hatimaye kuhatarisha maisha ya watu wengi.

Wito huo umetolewa na Daktari kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Edward Martin wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya moyo iliyofanyika kwa wafanyakazi wa kampuni ya TATA Africa Holdings Limited eneo la Vingunguti jijini Dar es Salaam.

Dkt. Martin alisema bado kuna hitaji kubwa la kuongeza elimu kwa umma kuhusu umuhimu wa kupima afya mapema, kwani ongezeko la magonjwa yasiyoambukiza linachangiwa kwa kiasi kikubwa na mifumo duni ya maisha pamoja na kukosa uelewa sahihi wa afya.

“Watu wengi hugundulika na matatizo ya moyo wakiwa katika viwango vya juu vya hatari kwa sababu ya kutofanya uchunguzi wa afya mara kwa mara",alisema Dkt. Martin.

“Tumekuwa tukikutana na wagonjwa wenye shinikizo la damu 200 juu ya 120 bila kujua kama wako hatarini. Wanapopata kiharusi ndipo hugundua. Kama wangefanya uchunguzi mapema, wangeepuka hali hiyo",aliongeza.

Kwa upande wake Meneja wa Rasilimali Watu kutoka kampuni ya TATA Africa Holdings Limited Kissa Mwasomola alisema zoezi hilo la upimaji limeenda sambamba na maadhimisho ya wiki ya maadili ya kampuni hiyo ambayo mwaka huu imejikita katika uwadilifu kwa vitendo.

“Tunawashukuru wataalamu wa JKCI kwa kutupatia huduma hizi muhimu. Afya ni kipaumbele kwetu na ujio wao umetusaidia sana kupata vipimo na elimu ya moyo bila usumbufu", alisema Kissa.

Baadhi ya wafanyakazi wa kampuni hiyo walieleza kufurahishwa na huduma hiyo huku wakisema imekuwa msaada mkubwa kutokana na changamoto ya kukosa muda wa kwenda hospitalini.

“Mimi ni mvivu wa kwenda hospitali, lakini ujio wa JKCI hapa kazini umenisaidia kupata vipimo vya moyo kirahisi", alisema Davis Moshi.

“Kwa upande wangu nina uzito mkubwa na madaktari wamenipa ushauri wa kupanga mlo wangu vizuri kuanzia asubuhi hadi jioni. Nilikuwa nakula bila mpangilio na ndiyo uliosababisha niongeze uzito", alisema Amina Mweta.

Huduma za uchunguzi na elimu inayotolewa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika taasisi mbalimbali nchini zinalenga kuhakikisha jamii inapima afya mapema, kutambua dalili hatarishi na kuchukua hatua kabla ya magonjwa ya moyo kufikia hatua mbaya.

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na Burkina Faso zasaini makubaliano ya ushirikiano katika kutoa tiba ya magonjwa ya moyo

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi

Msumbiji kushirikiana na JKCI katika tiba ya moyo