Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wawawekea wagonjwa wanne ambao uwezo wa moyo wao kusukuma damu uko chini ya asilimia 50 kifaa cha kuusadia moyo kufanya kazi vizuri (Cardiac Resynchronization Therapy Device – CRT-D)
Wagonjwa wanne wenye matatizo ya
kutanuka kwa moyo, uwezo wa moyo kusukuma damu kuwa chini ya asilimia 50, mfumo
wa umeme wa moyo kuwa na shida iliyopelekea moyo kutokufanya kazi sawasawa
wamewekewa kifaa cha kuusadia moyo kufanya kazi vizuri kijulikanacho
kitaalamu kwa jina la Cardiac Resynchronization Therapy Device – CRT-D.
Wagonjwa hao waliwekewa kifaa
hicho katika kambi maalum ya matibabu iliyofanywa kwa muda wa siku
mbili na wataalamu wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
iliyopo jijini Dar es Salaam.
Akizungumza na mwandishi wa habari
hizi mtaalamu mbobezi wa moyo na mzibuaji wa
mishipa ya damu ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) ambaye
pia ni mratibu wa kambi hiyo Yona Gandye alisema wagonjwa waliowekewa vifaa
hivyo mfumo wao wa umeme wa moyo ulikuwa na hitilafu kubwa hali iliyopeleka
moyo kushindwa kusukuma damu ya kutosha mwilini.
“Wengi wao walikuwa wanalalamika
kuchoka kutwa nzima na hivyo kushindwa kufanya shughuli zao vizuri
na kukosa pumzi. Wagonjwa hawa tumewawekea kifaa cha High Power
Device (CRT- D) ambacho kitausaidia moyo kufanya kazi vizuri hivyo basi
wataweza kuendelea na maisha yao kama kawaida”, alisema Dkt. Gandye.
Alizitaja sababu za kutanuka kwa
moyo kuwa ni magonjwa hatarishi kama sukari, shinikizo la juu la damu,uzito
mkubwa,uvutaji wa sigara na unywaji wa pombe uliokithiri, urithi kutoka kwa
wazazi, maambukizi yanayotokana na virusi au bakteria au fungus.
Dkt. Gandye alisema katika kambi
hiyo pia walimtibu mgonjwa mmoja aliyekuwa na tatizo la mapigo ya moyo kwenda
haraka kuliko kawaida (zaidi ya mapigo 200 kwa dakika) kawaida huwa
ni 60 hadi 90 kwa dakika.
“Kabla ya kumtibu mgonjwa huyu
tuliuchunguza moyo ili kubaini chanzo na njia inayosababisha mapigo ya moyo
kwenda haraka kuliko kawaida na baada ya kubaini sehemu hiyo tuliithibiti kwa
kuziziba au kuziunguza njia hizo kwa jina la kitaalamu matibabu hayo
yanajulikana kama Electrophysiological (EP) studies & ablation”.
“Kimaumbile mtu mwenye tatizo hili
moyo wake hauna shida lakini una hitilafu kwenye mfumo wa
umeme wa moyo hali hii ilipelekea moyo kudunda kwa haraka zaidi.
Dalili za ugonjwa huu ni kusikia mapigo ya moyo yakidunda, kuzimia na pumzi
kubana”, alisema Dkt.Gandye.
Alizitaja sababu za moyo kuwa na
hitilafu ya mfumo wa umeme ni mtu kuzaliwa na hitilafu hii.
Wakizungumza wakiwa wodini
wakiendelea na matibabu wagonjwa waliowekewa vifaa hivyo walisema tangu
wamewekewa hali ya mwili kuchoka imepungua sana pia wanapata pumzi
vizuri tofauti na ilivyokuwa awali.
Bibi Safira Chirege kutoka
wilayani Ukerewe alisema kabla hajafika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete
mwezi wa kwanza mwaka huu kwa ajili ya matibabu alikuwa na tatizo la kifua
kubana na hakuwa anaweza kuongea sana na miguu ilikuwa inavimba.
“Kama unavyoniona baada ya kuwekea
kifaa hicho sasa hivi naweza kuongea vizuri, ninapata pumzi vizuri na ninaweza
kutembea. Hapa nilipo ninamaumivu ya kidonda tu mahali ambapo wameniweka kifaa
hiki na ninaamini kikipona nitakuwa mzima kama zamani”, alisema Bibi Sarafina.
Alisema kabla ya kufika JKCI miaka
mitatu iliyopita alikuwa anatibiwa katika Hospitali mbalimbali alilazwa Ukerewe
na kuwekewa mashine ya kumsaidia kupumua mara moja na pia alitibiwa Morogoro na
kuwekewa mashine ya kumsaidia kupumua mara mbili.
Tangu mwaka 2016 jumla ya wagonjwa
31 wameshawekewa vifaa hivyo katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa
upande wa matibabu ya tatizo la mapigo ya moyo kwenda haraka kuliko
kawaida (Electrophysiological (EP) studies & ablation) wagonjwa
watano wameshafanyiwa tiba hiyo ambayo iliyoanza mwaka 2019.
Wataalamu wabobeza wa moyo na wazibuaji wa
mishipa ya damu ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimwekea kifaa cha kuusadia moyo kufanya kazi
vizuri kijulikanacho kitaalamu kwa jina la Cardiac Resynchronization Therapy
Device – CRT-D mgonjwa ambaye uwezo wa moyo wake kusukuma damu uko
chini ya asilimia 50 wakati wa kambi maalum ya siku mbili iliyofanywa na
madaktari wa Taasisi hiyo hivi karibuni.
Comments
Post a Comment