Jengeni tabia ya kupima afya za mioyo yenu mara kwa mara - Prof. Janabi


Wananchi wakipata huduma  ya ushauri wa magonjwa ya moyo katika banda la Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)


Wananchi wameshauriwa  kujenga mazoea ya kupima afya zao mara kwa mara  ili  kufahamu kama wana magonjwa ya moyo  au la na kama wanamatatizo  wataweza  kupata matiba mapema kabla ya tatizo kuwa kubwa na kama hawana itawasaidia kujikinga ili  wasipate magonjwa hayo.

Rai hiyo imetolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi wakati akizungumza na waandishi wa habari  katika maonesho ya 45 ya Kimataifa ya Dar es Salaama (Sabasaba) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

Prof. Janabi alisema ni muhimu kwa wananchi kutumia maonesho hayo kupima afya zao na kupata uelewa wa jinsi ya kujikinga na magonjwa mbalimbali ikiwemo moyo, figo na saratani.

“Katika banda letu tunapima vipimo mbalimbali vya magonjwa ya  moyo vikiwemo vipimo vya kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography - ECHO) , umeme wa moyo unavyofanya kazi (Electrocardiography – ECG) , vipimo vya damu na vipimo vya urefu na uzito na kuangalia kiangalia kiwango cha  sukari kwenye damu”,.

“Pia tunatoa elimu ya lishe ambayo itamsaidia mtu kufahamu ni vyakula gani anatakiwa kula ili aweze kutunza mwili na moyo wake, nawakaribisha wananchi mtembelee katika banda letu ili mpate huduma hizi”, alisema Prof. Janabi.

Prof. Janabi ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alisema katiba banda hilo mwananchi akipimwa na kukutwa na tatizo la moyo au sukari anapewa dawa bila malipo yoyote pia anapewa rufaa ya moja kwa moja ya kwenda kutibiwa matibabu ya kibingwa katika Taasisi hiyo.

Kwa upande wa wananchi waliopata huduma ya kufanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo na wataalamu wa Taasisi hiyo walishukuru kwa huduma waliyoipata.

“Nimefika hapa sikuwa najua kama ninatatizo la ugonjwa wa kisukari, nimepima na kupata msaada mkubwa wa vipimo na elimu wataalamu wanakusikiliza kwa umakini , kama una swali unauliza wanakujibu”,.

“Nimepewa dawa za ugonjwa wa kisukari ambazo nitaenda kuzitumia sijalipia fedha yeyote ile. Ninaiomba Serikali izidishe elimu kwa wananchi ili wajue umuhimu wa kupima afya zao mara kwa mara kama mimi nisingepima leo hii nisingefahamu kama ninatatizo la kisukari”, alishukuru Salehe Abdala mkazi wa Ukonga jijini Dar es Salaam.


Fundi sanifu wa moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Paschael Kondi akimpima mwananchi aliyetembea banda la Taasisi hiyo kipimo cha kuangalia jinsi mfumo wa umeme wa moyo unavyofanya kazi (Electrocardiography – ECG) wakati wa  maonesho ya 45 ya Kimataifa ya Dar es Salaama (Sabasaba) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Aloyce  akimpima mwananchi aliyetembea banda la Taasisi hiyo kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography - ECHO) wakati wa  maonesho ya 45 ya Kimataifa ya Dar es Salaama (Sabasaba) yanayofanyika katika viwanja vya Mwalimu Julius Kambarage Nyerere vilivyopo barabara ya Kilwa.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)