Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete yapongezwa kwa kuanzisha duka la kuuza dawa za magonjwa mbalimbali ya binadamu




Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Doroth Gwajima akisafisha mikono kwa kutumia kitakasa mikono kilichotengenezwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Compounding unit alipotembelea duka la dawa za magonjwa mbalimbali lililoanzishwa na Taasisi hiyo leo Jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi wa JKCI Dkt. Delilah Kimambo


Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Doroth Gwajima ameipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuanzisha duka la dawa linalouza  dawa za kutibu magonjwa  mbalimbali na kuzitaka Hospitali zingine kuiga mfano huo.

Waziri Dkt. Gwajima amezitoa pongezi hizo  leo jijini Dar es Salaam wakati akizindua maktaba ya watoto wanaosumbuliwa na maradhi ya Moyo na saratani wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH).

Dkt. Gwajima alisema kuwepo kwa duka hilo la dawa kutawasaidia wagonjwa wanaotibiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)  na Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) badala ya kwenda kununua dawa nje ya Muhimbili watakwenda kuzinunua katika duka hilo.

“Kuna dawa ambazo hazipatikani ndani ya Hospitali , mgonjwa akiandikiwa dawa hizi na daktari analazimika kwenda kuzinunua nje ya Muhimbili . Kuwepo kwa duka hili kutawasaidia wagonjwa kupata dawa hizi ndani ya Muhimbili na kuweza kuokoa muda  wa kutembea kwenda kutafuta dawa”, alisisitiza Dkt. Gwajima.

Dkt. Gwajima pia aliipongeza compounding Unit ambao wanatengeneza dawa za watoto za moyo kutoka kidonge cha mtu mzima hadi kuwa kwenye matumizi ya watoto na kutengeneza vitakasa mikono “sanitizer” ambazo zinatumika katika Taasisi hiyo na zingine zinauzwa katika duka hilo la dawa.

“Hospitali zingine ziige mfano wa JKCI kwani kuwepo kwa duka la dawa ambalo mtu ananunua kwa kulipia na compounding unit ambao wanazalisha dawa na pamoja na vitakasa mikono kutasaidia Hospitali kuongeza kipato pamoja na kurahisisha upatikanaji wa dawa kwa wagonjwa”, alisisitiza Dkt. Gwajima.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa JKCI Prof. Mohamed Janabi alisema kabla ya kuanzishwa kwa duka hilo waliangalia ni aina gani za dawa ambazo hazipatikani MNH, JKCI na MOI na kuziweka katika duka hilo ili kuwarahisishia wagonjwa pamoja na watu wengie  kupata dawa hizo kirahisi.

“Dawa hizi pamoja na bidhaa zingine ambazo zinatakiwa kuuzwa katika duka la dawa zinauzwa kwa kulipia, mtu yeyote anafika katika duka hili na kununua dawa anazozitaka. Kuna dawa ambazo unanunua moja kwa moja bila ya kuandikiwa na daktari na kuna dawa ambazo unaandikiwa na daktari”, alisema Dkt. Janabi.

Akizungumzia kuhusu Compounding Unit Mkurugenzi wa Tiba Shirikishi  katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Delila Kimambo alisema imewasaidia katika upatikanaji wa dawa za moyo za watoto kwani dawa hizo hazipatikani kwenye soko la dawa nchini kutokana na dawa hizo kutozalishwa viwandani.

Dkt. Delila ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alisema duka hilo la dawa limeanza kufanya kazi mwanzoni mwa mwezi Juni  na linahudumia zaidi ya watu 100 kwa siku.

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Doroth Gwajima akisoma fomu ya mgonjwa aliyetembelea duka la dawa lililoanzishwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam leo kwa ajili ya kuuza dawa za magonjwa yote kwa wagonjwa wanaopatiwa huduma za matibabu katika Hospitali Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI) pamoja na watu wengine watakaohitaji huduma hiyo. 


Waziri wa Afya Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Mhe. Dkt. Doroth Gwajima akizungumza na mfamasia alipotembelea leo duka la dawa lililoanzishwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) iliyopo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kuuza  dawa za magonjwa yote kwa wagonjwa wanaopatiwa huduma za matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI), JKCI pamoja na watu wengine watakaohitaji kununua dawa hizo.


Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)