Wafanyakazi wa Benki ya Exim Idara ya Fedha wachangia gharama za matibabu ya mtoto mwenye matatizo ya moyo

Msimamizi wa Wodi ya Watoto ambaye pia ni Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theresia Marombe akiwaeleza wafanyakazi wa Benki ya Exim Idara ya Fedha waliofika katika Taasisi hiyo kwa ajili ya kuchangia gharama za upasuaji wa moyo kwa mtoto alizaliwa na  tundu kwenye moyo huduma zinazotolewa kwa wagonjwa wanaolazwa katika wodi hiyo.

Mkuu wa Idara ya Fedha kutoka Benki ya  Exim Issa Hamisi akimkabidhi Mhasibu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mohamed Isimbula kiasi cha Tshs. 3,000,000/= fedha zilizochangwa na  baadhi ya wafanyakazi wa Benki hiyo  Idara ya Fedha kwa ajili ya kulipia gharama za upasuaji wa moyo kwa mtoto aliyezaliwa na tatizo la tundu kwenye moyo.

Mama ambaye mtoto wake amezaliwa na tundu kwenye moyo Elizabeth John akipokea kiasi cha Tshs. 400,000/= kutoka kwa Mkuu wa Idara ya Fedha wa Benki ya  Exim Issa Hamisi fedha ambazo atazitumia kwa ajili ya kununua chakula na mahitaji mengine  ya mtoto kabla na baada ya kufanyiwa upasuajia wa moyo utakaofanyika katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).   

Baadhi ya wafanyakazi wa Benki ya  Exim kutoka  Idara ya Fedha wakiwajulia hali watoto waliolazwa katika wodi ya watoto wenye magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati walipotembelea wodi hiyo leo kwa ajili ya kuchangia gharama za matibabu ya mtoto aliyezaliwa na tundu kwenye moyo.


Na: JKCI

Taasisi zinazotegemea watu ili ziweze kujiendesha zimeombwa kuisaidia jamii yenye uhitaji wa matibabu ya magonjwa mbalimbali ili iweze kuwa salama na yenye afya bora kwani jamii iliyo salama itaendelea kuwa sehemu ya Taasisi hizo na kuzifanya ziweze kufikia malengo ya kazi waliyojipangia.

Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mhasibu wa Benki  ya Exim Beatus Temba alipokuwa akizungumza na uongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wafanyakazi wa benki hiyo kutoka Idara ya Fedha walipotembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya kuchangia gharama za upasuaji wa moyo kwa mtoto aliyezaliwa na  matatizo ya moyo.

Temba alisema kupitia Redio Clouds kipindi cha Njia panda alipata taarifa za mtoto aliyezaliwa na tundu kwenye moyo ambaye familia yake ilikosa fedha za  kumlipia gharama za matibabu akawashirikisha  wafanyakazi wenzake ili waweze kuokoa maisha ya mtoto huyo.

“Baada ya kuwashirikisha wafanyakazi wenzangu ofisini walilipokea wazo langu ndipo tukaamua kuchangishana fedha za matibabu ya mtoto huyo ili aweze kupata matibabu na kuwa na maisha ya furaha kama watoto wengine”,.

“Bila Jamii Taasisi zetu haziwezi kujiendesha inatupasa kuhakikisha kuwa jamii yetu ipo salama na yenye afya bora, nawashukuru wafanyakazi wenzangu kutoka Idara ya Fedha ambao kwa pamoja tumeweza kukusanya kiasi cha Tshs. 3,400,000/= fedha ambazo zitatumika katika matibabu ya mtoto huyu”, alisema Temba.

Aidha Temba aliipongeza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa huduma za matibabu ya moyo inazozitoa kwa wagonjwa na kuishukuru kwa kupokea mchango wao walioutoa ambao utasaidia kuokoa maisha ya mtoto huyo.

“Kiasi cha fedha tuliyokusanya ni Tsh. 3,400,000/= fedha ambazo tumeikabidhi JKCI ni shilingi 3,000,000/= ikiwa ni gharama za upasuaji wa moyo pamoja na gharama nyingine za matibabu na kiasi cha shilingi 400,000/= tumemkabidhi mama wa mtoto kwa ajili ya matumizi ya chakula na mahitaji mengine atakayotumia kabla na baada ya upasuaji.

Kwa upande wake  Msimamizi wa Wodi ya Watoto Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theresia Marombe aliwashukuru wafanyakazi wa Benki ya Exim kwa moyo wao wa upendo wa  kumsaidia mtoto huyo gharama za matibabu na lishe kwani ni kitu cha kipekee watu kusaidia gharama za matibabu na kukumbuka upande wa lishe.

“Watoto wetu wengi tumekuwa tukiwapokea wakiwa na lishe duni, hivyo kuchukuwa muda mrefu wodini kuwahudumia ili kuhakikisha wanafikia uzito ambao utawawezesha kwenda kufanyiwa upasuaji lakini nyie mmekuja mkiwa mmefikiria kusaidia katika upande wa matibabu na lishe”, alisema Theresia.

Theresia aliwaahidi wafanyakazi hao wa Banki ya Exim kuwa JKCI itaendelea kuwapa taarifa zote za matibabu ya mtoto huyo hatua kwa hatua hadi pale matibabu yake yatakapokamilika na kuwaomba kwenda kumuona mtoto huyo mara atakapofanyiwa upasuaji.



Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari