Prof. Janabi: Wanaume ombeni nafasi za kushiriki mafunzo mbalimbali

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akizundua mpango mkakati wa mwaka 2022/23 -2025/2026 wa taasisi hiyo wakati wa hafla fupi ya kuzindua mpango huo iliyofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa JKCI jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) CPA Agnes Kuhenga akielezea mpango mkakati wa mwaka 2022/23 -2025/2026 wa JKCI jinsi utakavyofanya kazi kwa viongozi wa Taasisi hiyo wakati wa hafla fupi ya kuzindua mpango huo iliyofanyika leo jijini Dar es Salaam

Viongozi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakimsikiliza Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) CPA Agnes Kuhenga wakati akiwaelezea kuhusu mkakati wa taasisi hiyo mwaka 2022/23 -2025/2026.

Mwenyekiti wa kamati iliyoandaa mpango mkakati wa mwaka 2022/23 -2025/2026 wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akielezea namna ambavyo mpango mkakati huo umelenga kuboresha huduma zinazotolewa na Taasisi hiyo kwa wananchi wakati wa hafla fupi ya kuzindua mpango mkakati huo iliyofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa JKCI jijini Dar es Salaam.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Prof. Mohamed Janabi akiwa katika picha ya pamoja na viongozi wa JKCI pamoja na  wajumbe wa kamati iliyoandaa mpango mkakati wa Taasisi hiyo wa mwaka 2022/23 -2025/2026 mara baada ya kuuzindua leo jijini Dar es Salaam.

Picha na Khamis Mussa

******************************************************************************************************************************
Na: Salome Majaliwa

Wafanyakazi wa kiume wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kuomba nafasi za mafunzo mbalimbali ili kuongeza ujuzi wa kazi tofauti na ilivyo sasa ambapo wanawake ndio wanaoomba zaidi nafasi za kushiriki mafunzo hayo.

Rai hiyo imetolewa leo jijini Dar es Salaam na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi hiyo Prof. Mohamed Janabi wakati akizundua mpango mkakati wa JKCI wa mwaka 2022/23 -2025/2026.

Prof. Janabi alisema katika kutekeleza mpango mkakati wa kwanza wa mwaka 2017-2022 JKCI imewekeza katika vifaa tiba vya kisasa hivyo basi kama wafanyakazi hawataongeza taaluma zao kwa kusoma kozi za muda mrefu na mfupi vifaa hivyo vitazidi taaluma walizonazo sasa na hivyo kushindwa kuvitumia.

“Taasisi yetu imekuwa ikiwawezesha wafanyakazi wa kada zote wanaotaka kusoma kuongeza elimu ili waweze kuendana na maendeleo ya sayansi na teknolojia changamoto iliyopo wanaume wanaojitokeza ni wachache ukilinganisha na wanawake ninawaomba nanyi wanaume mjitokeze kwa wingi kuomba nafasi za kusoma”,.

 “Takwimu nilizonazo zinaonesha wafanyakazi wengi wa jinsia ya kike wa JKCI wapo mstari wa mbele kushiriki mafunzo ya kuongeza ujuzi, nawahimiza sasa wafanyakazi wa jinsia ya kiume nanyi mjitokeze fursa hii ni yetu sote”, alisema Prof. Janabi.

Akisoma taarifa ya utekelezaji wa mpango mkakati wa mwaka 2017-2022 Mkurugenzi wa Fedha na Mipango wa JKCI CPA Agnes Kuhenga alisema mpango mkakati wa  kwanza umeleta mafanikio makubwa ikiwemo uboreshaji wa miundombinu na uwekezaji wa vifaa tiba vya kisasa.

“Mpango Mkakati wa mwaka 2017-2022 umeiwezesha JKCI kufunga mtambo mpya wa Cath lab, ujenzi wa duka la dawa za magonjwa mbalimbali, uanzishwaji wa maabara ya kutengeneza dawa za maji kwa ajili ya watoto wenye magonjwa ya moyo, ujenzi wa wodi ya watoto na ukarabati wa wodi za watu maarufu”,.

“Pia mpango mkakati huo uliwezesha ununuliwaji wa vifaa vya kisasa vya matibabu zaidi ya 500, uboreshwaji wa sehemu wanazokaa wauguzi, pamoja na kusimamia ukusanyaji wa mapato na matumizi ya fedha kwa asilimia 100”, alisema CPA Agnes.

CPA Agnes alisema mpango mkakati wa pili ulioanza kufanya kazi mwaka huu wa fedha wa 2022/23 umeandaliwa na wataalamu kutoka JKCI tofauti na ule wa kwanza ambao ulihusisha wadau kutoka nje ya taasisi kuuandaa.

“Nawapongeza wajumbe wa kamati ya kuandaa mpango mkakati wa mwaka 2022/23 -2025/2026 kwa kufanya kazi nzuri na kubwa kwani hii ni mara yetu ya kwanza kuwahusisha wataalam wetu kuandaa mpango huu tofauti na ule wa kwanza ambao uliwahusisha wadau kutoka nje ya Taasisi”, alisema CPA Agnes.

Akielezea mpango mkakati wa mwaka 2022/23 -2025/2026 Mwenyekiti wa uandaaji wa mpango mkakati huo Dkt. Peter Kisenge alisema kazi ya uandaaji wa mpango huo imekamilika sasa ni wakati kwa wafanyakazi wote kuusoma, kuuelewa na kutimiza majukumu yao kama mpango huo unavyowataka kufanya.

Dkt. Kisenge ambaye pia ni daktari bingwa wa magonjwa ya moyo alisema kwa kuwahusisha wataalam wa JKCI kuandaa mpango mkakati huo kumeongeza wigo mpana kwa wanakamati ambao kupitia wao wafanyakazi wote wapewe uelewa wa namna wanapaswa kutimiza majukumu yao kwa kufuata mpango mkakati wa mwaka 2022/23 -2025/2026.

“Nawashukuru wajumbe wa kamati ya kuandaa mpango mkakati wa mwaka 2022/23 -2025/2026, ushirikiano na utayari mliouonesha wakati tunaandaa muendelee kuuonyesha kwa wafanyakazi wengine pindi watakapohitaji kupata ufafanuzi ili malengo tuliyoyaweka yaweze kufikiwa ifikapo mwaka 2026”, alisema Dkt. Kisenge.

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Maabara ya JKCI yapata ithibati ya kimataifa (ISO 15189:2012)