JKCI kuanzisha Kitengo cha matibabu ya moyo Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe (NRRH).
Mkurugenzi
Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge
akizungumza na kamati ya kuanzisha huduma za matibabu ya moyo katika hospitali
ya Rufaa ya Mkoa Njombe (NRRH) wakati wa kikao cha kujadili ushirikiano kati ya
JKCI na NRRH kilichofanyika jana katika ukumbi wa mikutano wa JKCI iliyopo
jijini Dar es Salaam.
Baadhi
ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), wataalamu wa afya wa
mkoa wa njombe na wafanyakazi wa hospitali ya rufaa ya mkoa Njombe (NRRH) wakisikiliza
wakati wa kikao cha kujadili ushirikiano wa kuanzisha huduma za matibabu ya
moyo kati ya JKCI na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Njombe jana jijini Dar es
Salaam.
Mganga
Mkuu wa Mkoa wa Njombe Dkt. Juma Mfanga akizungumza na kamati ya kuanzisha
huduma za matibabu ya moyo katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa Njombe (NRRH)
wakati wa kikao cha kujadili ushirikiano kati ya JKCI na NRRH kilichofanyika jana
katika ukumbi wa mikutano wa JKCI iliyopo jijini Dar es Salaam.
Mkurugenzi
wa Hospitali ya JKCI Dar Group Dkt. Tulizo Shemu akizungumza na kamati ya
kuanzisha huduma ya magonjwa ya moyo katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa Njombe
(NRRH) wakati wa kikao cha kujadili ushirikiano kati ya JKCI na NRRH
kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa JKCI jijini Dar es Salaam.
Hayo
yamesemwa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt.
Peter Kisenge wakati wa kikao cha kwanza cha majadiliano kuhusu ushirikiano wa kuanzishwa
kwa kitengo cha moyo katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Njombe (NRRH).
Akizungumza
wakati wa kikao hicho Dkt. Kisenge alisema ushirikiano huo utasaidia kuwajengea
uwezo wataalamu wa afya wa NRRH kupitia mafunzo na kubadilishana uzoefu na
wataalamu wa JKCI.
“JKCI
inataka kuwafikishia wananchi huduma za magonjwa ya moyo pale walipo ndiyo maana
tunawajengea uwezo wataalamu wa afya wa NRRH ili wananchi wasisafiri umbali
mrefu kuweza kupata huduma hizi”, alisema Dkt. Kisenge.
Dkt.
Kisenge alisema Njombe ni eneo la kimkakati kutokana na kuwa karibu na nchi za
Malawi na Zambia hivyo kituo hicho hakitawahudumia wananchi wa Njombe pekee
bali kinaweza pia kuchangia katika kukuza utalii tiba nchini.
“Ni
matarajio yetu kwamba hospitali hii itakuwa moja ya kituo bora kabisa jumuishi
cha magonjwa ya moyo na mishipa ya damu mkoani Njombe ili kiweze kuwahudumia
wananchi wa Njombe, mikoa jirani na nchi zilizopo jirani”, alisema Dkt. Kisenge
Kwa
upande wake Mganga Mkuu wa Mkoa wa Njombe Dkt. Juma Mfanga alisema ushirikiano
huo ni muhimu kutokana na uhitaji mkubwa wa huduma za matibabu ya moyo katika ukanda
wa Nyanda za Juu Kusini.
Akizungumzia
ukubwa wa tatizo la magonjwa ya moyo mkoani Njombe Dkt. Mfanga alisema takwimu
za mwaka 2025 zinaonyesha kuwa kati ya asilimia 40 hadi 48 ya wagonjwa
waliotibiwa walikuwa na matatizo yanayohusiana na moyo au mishipa ya damu, hali
hiyo inaonesha umuhimu wa kuanzisha huduma hizo mapema ili wagonjwa wapate
matibabu kabla ya kupata madhara makubwa.
Naye
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe Dkt. Gilbert Kwesi alisema
hospitali hiyo imekuwa ikitoa wastani wa rufaa zisizopungua mbili kwa siku kwa
wagonjwa wanaohitaji huduma za matibabu ya moyo.
Dkt.
Kwesi alisema takwimu za hospitali zinaonesha ongezeko la wagonjwa wenye
magonjwa yasiyoambukiza hususan magonjwa ya moyo wanafika wakiwa tayari
wamepata madhara makubwa ikiwemo kiharusi.
Ushirikiano huo kati ya JKCI na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Njombe (NRRH) unatarajiwa kuongeza upatikanaji wa huduma za magonjwa ya moyo Nyanda za Juu Kusini na kupunguza mzigo wa wagonjwa kusafiri umbali mrefu kutafuta huduma hizo.
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
.jpeg)
Comments
Post a Comment