Kampuni ya WATU yatoa vifaa tiba vyenye thamani ya shilingi milioni 11 kwa JKCI
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akipokea vifaa tiba aina ya Syringe Pump System vyenye thamani ya shilingi milioni 11 kutoka kwa Mkuu wa Kitengo cha Huduma kwa Wateja kutoka Kampuni ya Mikopo ya Simu na Vyombo vya Moto (WATU) Patricia Sempinge wakati kampuni hiyo ilipochangia mashine hizo ili kuongeza ufanisi wa huduma kwa wagonjwa wa moyo wanaotibiwa JKCI.
Mfanyakazi wa Kampuni ya Mikopo ya Simu na Vyombo vya Moto (WATU) akimpatia mzazi wa mtoto aliyelazwa katika wodi ya watoto wenye magonjwa ya moyo zawadi wakati wafanyakazi wa kampuni hiyo walipotembelea Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwaajili ya kutoa vifaa tiba na zawadi kwa watoto katika kuongeza ufanisi wa huduma kwa wagonjwa wa moyo wanaotibiwa JKCI.
Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na wafanyakazi kutoka
Kampuni ya Mikopo ya Simu na Vyombo vya Moto (WATU) walipotembelea Taasisi hiyo kwaajili ya kutoa vifaa
tiba aina ya Syringe Pump System vyenye thamani ya shilingi milioni 11 kama
sehemu ya kuongeza ufanisi wa huduma kwa wagonjwa wa moyo wanaotibiwa JKCI.
Picha na JKCI
*********************************************************************************************
Kampuni ya huduma za mikopo ya simu na vyombo vya moto “Watu” yatoa vifaa
tiba aina ya Syringe Pump System vyenye thamani ya shilingi milioni 11 kwaajili
ya kuongeza ufanisi wa huduma kwa wagonjwa wa moyo wanaotibiwa katika Taasisi
ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).
Vifaa hivyo hutumika kuingiza dawa kwa usahihi mkubwa kupitia mishipa ya damu
kwa wagonjwa waliolazwa katika wodi ya
wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU).
Akizungumza wakati wa kupokea vifaa hivyo leo katika ukumbi wa JKCI
iliyopo jijini Dar es Salaam Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge aliishukuru kampuni hiyo kwa moyo wa
kujitolea na kuona umuhimu wa kuwekeza katika sekta ya afya.
“Vifaa hivi ni msaada mkubwa kwa
wagonjwa wetu na kwa madaktari wanaovitumia katika kutoa huduma lakini pia
ushirikiano kama huu una mchango mkubwa katika kuendelea kuboresha huduma za
matibabu ya moyo nchini”, alisema Dkt. Kisenge
Aidha kupitia mchango huo Dkt. Kisenge
amewaomba wadau na makampuni mengine nchini kuiga mfano huo kwa kushirikiana na
taasisi za afya kupitia uwajibikaji kwa jamii huku akisisitiza kuwa mchango wa
sekta binafsi una nafasi muhimu katika kuimarisha huduma za afya na kuokoa
maisha ya wananchi.
“Kampuni ya WATU imekuwa ya mfano kwa kuwafikiria
wagonjwa wetu na kutoa vifaa hivi, kampuni nyingine ziendelee kugusa maisha ya
wagonjwa wetu na kuwa sehemu ya kuboresha sekta ya afya kwa kushirikiana na
Serikali”, alisema Dkt. Kisenge
Kwa upande wake Mkuu wa kitengo cha
huduma kwa wateja kutoka kampuni ya mikopo ya simu na vyombo vya moto (WATU)
Patricia Sempinge alisema kampuni hiyo imeamua kutoa msaada wa mashine hizo na mahitaji
mengine ya wagonjwa kwa lengo la kutambua mchango mkubwa unaotolewa na JKCI
katika kutoa huduma bingwa na bobezi za magonjwa ya moyo.
“Kampuni ya WATU inaadhimisha miaka
mitano ya kuboresha maisha ya Watanzania kupitia huduma za mikopo ya simu pamoja
na vyombo vya moto na leo tumefika JKCI kukabidhi mashine hizi ili kuunga mkono
juhudi zinazofanywa na Taasisi hii katika kuokoa maisha ya wagonjwa wa moyo”,
alisema Patricia.
Aidha Patricia aliipongeza JKCI kwa kuendesha
kampeni ya jua namba zako kwani wamepata fursa ya kupima viashiria muhimu vya
afya na kutambua hali zao mapema.
“Magonjwa yasiyoyakuambukiza yanaendelea
kuongezeka, hivyo kupata nafasi ya kufanyiwa uchunguzi na kujua namba tano
muhimu za afya bila malipo ni fursa muhimu kwetu”, alisema Patricia.





Comments
Post a Comment