Watu 200 wanufaika na huduma ya uchunguzi na matibabu ya macho Arusha

Daktari bingwa wa macho wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI - ALMC) John Njelango akimpima kipimo cha kuchunguza macho mwananchi aliyefika katika kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza inayofanyika katika Hospitali hiyo iliyopo jijini Arusha.

Afisa Uuguzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI - ALMC) Fabian Bura akimsaidia mkazi wa Arusha aliyefika katika kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza kwaajili ya kufanya uchunguzi wa afya inayofanyika katika Hospitali iliyopo jijini Arusha.

Mhudumu wa afya wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI - ALMC) Ombeni Daniel akimpima joto la mwili mkazi wa Arusha aliyefika katika kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza inayofanyika katika Hospitali hiyo iliyopo jijini Arusha.

Baadhi ya wananchi wa mkoa wa Arusha wakisoma vipeperushi vinavyoelezea  elimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza inayofanyika katika Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI-ALMC) iliyopo jijini Arusha.

Afisa huduma kwa wateja wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI - ALMC) Josephine Butesigirwe akitoa elimu kuhusu magonjwa yasiyoambukiza kwa wakazi wa Arusha waliofika katika kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza inayofanyika katika Hospitali hiyo iliyopo jijini Arusha.

Na JKCI

**************************************************************************************************************

Watu 200 wamepatiwa huduma za uchunguzi na matibabu ya macho kupitia kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa macho inayoendeshwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI–ALMC) kwa kushirikiana na Kampuni ya GSM Foundation.

Akizungumza wakati wa kambi hiyo Daktari Bingwa wa Macho wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI–ALMC) John Njelango alisema watu hao wamepatiwa huduma za macho ikiwemo kufanyiwa kipimo cha presha ya macho, uchunguzi wa madhara ya kisukari kwenye macho pamoja na vipimo vya miwani.

Dkt. John alisema kupitia kambi wataalamu wamebaini kuwa wagonjwa wenye matatizo yanayohitaji matibabu zaidi ikiwemo mtoto wa jicho na presha ya macho ni wengi huku baadhi wakigundulika kuwa na matatizo ya macho ambayo huenda walidhani hayatibiki.

“Ikiwa leo ni siku ya tatu tangu kambi hii ianze tayari tumeshawaona watu 200 waliohitaji huduma za uchunguzi wa macho. Watu wote hawa tumewafanyia vipimo na wale waliogundulika kuwa na matatizo tumewapa huduma kutokana na matatizo waliyonayo”, alisema Dkt. John.

Dkt. John alisema huduma hizo zimewasaidia wataalamu kubaini mahitaji mbalimbali ya wagonjwa ambapo wengi wameonekana kuhitaji miwani ya kutembelea na kusomea huku wengine wakibainika kuwa na matatizo yanayohitaji ufuatiliaji na matibabu zaidi.

 “Kuna uhusiano kati ya magonjwa ya kisukari na presha ya macho, magonjwa haya yanaweza kuathiri macho, ni muhimu watu wakaendelea kufika katika Hospitali yetu kupata huduma katika kambi ili waweze kupima macho na magonjwa mengine yanayotolewa katika kambi yetu”, alisema Dkt. John.

Kwa upande wake mkazi wa Arusha Joyce Molel alisema amefurahishwa na huduma alizopata katika kambi hiyo akibainisha kuwa kupitia kambi hiyo ameweza kujitambua na kufahamu tatizo lililokuwa likimsumbua.

“Nimehudumiwa vizuri nimepata majibu yangu hapohapo na kujua tatizo linalonisumbua kwa miaka mingi, lakini pia nimeshauriwa miwani ambayo natakiwa kuvaa ili iweze kunisaidia katika shughuli zangu”, lisema Joyce.

Charles Manga mkazi wa Arusha alisema kambi kama hizo ziwe zinafanyika mara kwa mara kuwasaidia wananchi kupata huduma za afya bila gharama na hata kuweza kutatua changamoto za kiafya walizonazo.

“Kama kuna watu bado hawajafika katika kambi hii basi wasisite kufika kwani wataondoka hapa wakiwa na furaha kufuatia huduma watakazozipata”, alisema Charles.

Kambi hiyo inalenga kusogeza huduma za uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo na macho karibu na wananchi wa Kanda ya Kaskazini huku ikitoa fursa kwa wananchi kutambua mapema changamoto za afya na kuchukua hatua stahiki.



Comments

Popular posts from this blog

Serikali yazindua kitabu safari ya upandikizaji wa moyo Tanzania, JKCI yaweka historia mpya ya huduma za kibobezi

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma