JKCI yazindua Bodi ya kusimamia tafiti (Institutional Review Board – IRB) kuimarisha utafiti wa magonjwa ya moyo nchini


Mwenyekiti wa bodi ya kusimamia tafiti (Institutional Review Board – IRB) ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Ahmed Abdallah akifuatilia mada zilizokuwa zikiendelea wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa JKCI iliyopo jijini Dar es Salaam.

Wajumbe wa bodi ya kusimamia tafiti (Institutional Review Board – IRB) ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakisikiliza wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa JKCI iliyopo jijini Dar es Salaam.


Mwenyekiti wa bodi ya kusimamia tafiti (Institutional Review Board – IRB) ya Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Ahmed Abdallah na wajumbe wa bodi hiyo wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya kumalizika kwa uzinduzi wa bodi hiyo uliofanyika leo katika ukumbi wa mikutano wa JKCI iliyopo jijini Dar es Salaam.

Na JKCI

************************************************************************************************************************

Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imezindua Bodi ya kusimamia tafiti (Institutional Review Board – IRB) itakayohakikisha tafiti za JKCI zinazingatia maadili, sheria na viwango vinavyotakiwa katika tafiti zinazohusisha binadamu.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa bodi hiyo Mwenyekiti wa Bodi ya IRB Dkt. Ahmed Abdallah alisema kuanzishwa kwa IRB ni hatua muhimu katika kuimarisha mfumo wa usimamizi wa tafiti zinazofanywa na JKCI hivyo bodi hiyo ina jukumu la kupitia na kutoa kibali kwa tafiti zitakazofanyika.

“Tunatarajia kwamba tafiti zitakazofanyika hapa zitaangaliwa na bodi na kupewa kibali, hatua hii itasaidia kuongeza ufanisi wa JKCI katika kutekeleza majukumu yake ya utafiti na kuhakikisha tafiti zinazofanyika zinakuwa na msingi mzuri wa kitaalamu na kimaadili”, alisema Dkt. Abdallah.

Kwa upande wake daktari bingwa wa upasuaji wa moyo na mishipa ya damu  wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Evarist Nyawawa alisema kuanzishwa kwa bodi ya IRB ni hatua muhimu kwa JKCI kutokana na nafasi ya taasisi hiyo inavyotambulika kimataifa katika kutoa huduma bingwa za uchunguzi na matibabu ya magonjwa ya moyo.

“Taasisi yetu ina taarifa (data) nyingi sana na tunahitaji kufanya tafiti kubwa kuhusiana na magonjwa ya moyo ili mwisho wa siku jamii na taifa zima wafaidike na uchunguzi unaofanyika kutokana na magonjwa yanayotibiwa kwenye Taasisi yetu”, Alisema Dkt. Nyawawa

Dkt. Nyawawa alisema JKCI inaendelea kukua na kupanuka, hivyo uwezo wa kufanya tafiti ni wa muhimu ili iweze kuongeza mchango wake kitaifa na kimataifa na kuweza kuilinda jamii na magonjwa ya moyo.

Naye Afisa Utafiti wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Hilda Tutuba alisema bodi ya IRB itasaidia kuhakikisha tafiti zinazohusisha binadamu zinafanyika kwa kuzingatia usalama, haki na maadili ya wanaofanyiwa utafiti.

“Tunapoongelea tafiti yoyote ambayo inamhusisha mwanadamu ni lazima ipite katika mapitio ili kuangaliwa kama imefuata masharti na vigezo vinavyotakiwa kuhakikisha kwamba haileti madhara kwa yule mtu ambaye utafiti utafanywa kwake”, alisema Hilda.

Kuanzishwa kwa Bodi ya Kusimamia Tafiti (IRB) kunatarajiwa kuimarisha uwezo wa JKCI katika kufanya tafiti zinazolenga kuongeza maarifa kuhusu magonjwa ya moyo na kuboresha huduma za afya huku tafiti hizo zikifanyika kwa kuzingatia misingi ya maadili na usalama wa washiriki.

Comments

Popular posts from this blog

Serikali yazindua kitabu safari ya upandikizaji wa moyo Tanzania, JKCI yaweka historia mpya ya huduma za kibobezi

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma