Asilimia 30 ya watu wenye magonjwa yasiyoambukiza wanaotibiwa JKCI hutoka Kanda ya Kaskazini

Kaimu Mkurugenzi wa Tiba na Mkuu wa Kitengo cha Huduma za Dharura wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI – ALMC) Peter Mabula akimueleza Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya GSM Foundation Faith Gugu huduma zinazotolewa katika kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza inayofanyika katika Hospitali ya JKCI-ALMC jijini Arusha.
Kaimu
Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya Arusha Lutheran
Medical Centre (JKCI – ALMC) Dkt. Godwin Kivuyo, Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya GSM
Foundation Faith Gugu, wafanyakazi wa JKCI – ALMC na GSM foundation wakiwa katika
picha ya pamoja wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya magonjwa
yasiyoambukiza inayofanyika katika hospitali ya JKCI-ALMC jijini Arusha.
Inakadiriwa
kuwa takribani asilimia 30 ya watu wenye magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo
magonjwa ya moyo wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
hutoka kanda ya kaskazini.
Hayo
yamesemwa na Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete – Hospitali ya
Arusha Lutheran Medical Centre (JKCI – ALMC) Dkt. Godwin Kivuyo wakati akizungumza
na waandishi wa habari katika kambi maalumu ya uchunguzi na matibabu ya
magonjwa yasiyoambukiza inayofanyika katika Hospitali ya JKCI – ALMC iliyopo mkoani
Arusha.
Dkt.
Kivuyo alisema kambi hiyo inalenga kuwapa wananchi fursa ya kupata huduma za uchunguzi
na matibabu ya magonjwa yasiyoambukiza hususani magonjwa ya moyo na macho bila
gharama lakini pia kuwapa fursa ya kuwa na tabia ya kuchunguza afya zao mara
kwa mara.
Dkt.
Kivuyo alisema kambi hiyo imefadhiliwa na Kampuni ya GSM Foundation hatua
ambayo imewezesha huduma za uchunguzi na matibabu kusogezwa karibu na wananchi
wa Arusha na maeneo mengine ya Kanda ya Kaskazini.
“Kampuni
ya GSM Foundation imetoa mchango mkubwa kwa kuwezesha upatikanaji wa huduma za
afya kwa wananchi wa mkoa wa Arusha na mikoa ya jirani, tunafurahi kuona
mwitikio umekuwa mkubwa kama ambavyo tulitarajia”, alisema Dkt. Kivuyo.
Kwa
upande wake Mkurugenzi Mkuu wa Kampuni ya GSM Foundation Faith Gugu alisema
taasisi hiyo imeamua kufadhili kambi hiyo baada ya kubaini kuwa asilimia 20
hadi 30 ya wagonjwa wanaotibiwa katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
tawi lake kuu lililopo jijini Dar es Salaam wanatoka Kanda ya Kaskazini.
Faith
alisema Kampuni ya GSM Foundation imekuwa ikishirikiana na JKCI kwa muda mrefu,
ikiwemo kufadhili matibabu ya watoto wenye matatizo ya moyo lakini pia kutoa
vifaa vya matibabu katika Hospitali ya JKCI-ALMC na na sasa imepanga kutoa
mashine itakayowezesha kufanyika kwa upasuaji wa moyo wa kufungua kifua katika
hospitali hiyo.
“Kampuni ya GSM Foundation tumekuwa tukishirikiana
na JKCI kwa muda mrefu, hata sasa tunawafadhili watoto wanaotoka katika familia
duni na wanatakiwa kufanyiwa upasuaji katika Taasisi hii”, alisema Faith
Mkazi
wa Levolosi mkoani Arusha Aziza Abdallah alisema amefurahishwa na huduma
alizopata katika kambi hiyo huku akiwataka wahudumu wa afya kuendelea
kuwahudumia wananchi licha ya kuwepo kwa idadi kubwa ya wagonjwa.
“Wataalamu
wanaotoa huduma katika kambi hii wasikate tamaa, waendelee kuwahudumia wananchi
kwani kazi yao ni ya wito, tunawapongeza sana”, alisema Aziza.
-
Mwisho -




Comments
Post a Comment