Watu 303 wapimwa moyo mkoani Manyara
Daktari bingwa wa
magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Geofrey Mohammed akizungumza
na mwananchi aliyefika katika kambi maalumu ya siku 5 ya uchunguzi na matibabu
ya moyo ijulikanayo kama Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba iliyokuwa
ikifanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa
ya Mkoa wa Manyara (MRRH) na kumalizika hivi karibuni.
Jumla ya wananchi 303 wa
Mkoa wa Manyara wamefaidika na huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya
magonjwa ya moyo zilizokuwa zikitolewa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya
Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa
Manyara (MRRH).
Huduma hizo zimetolewa
katika kambi maalumu ya siku tano ijulikanayo kama Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan tiba mkoba iliyokuwa ikifanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa
Manyara (MRRH) na kumalizika hivi karibuni Mkoani Manyara.
Akizungumza wakati wa
kuhitimisha kambi hiyo daktari kutoka Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Pedro Pallangyo alisema wananchi hao wamefanyiwa vipimo vya kibingwa vya moyo
ikiwemo Echocardiography (Echo) na Electrocardiogram (ECG) ambapo asilimia 46
walibainika kuwa na magonjwa mbalimbali ya moyo.
“Kati ya wananchi tuliowachunguza
asilimia 46 tumewakuta na magonjwa mbalimbali ya moyo. Baadhi yao tumewapatia
huduma za matibabu na ushauri huku wengine tukiwapa rufaa kufika JKCI kwa ajili
ya uchunguzi na matibabu ya kibingwa zaidi”, alisema Dkt. Pedro.
Dkt. Pedro alisema matatizo
mengi waliyoyabaini kwa watu wazima ni pamoja na tatizo la shinikizo la juu la
damu ambalo ni miongoni mwa visababishi vikuu vya magonjwa ya moyo na mishipa
ya damu.
Kwa upande wake Kaimu
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara (MRRH) Dkt. Yesige
Mutajwaa alisema kambi hiyo imekuwa na mafanikio makubwa kwa kuwa imewawezesha
wananchi wengi kupata huduma za kibingwa ambazo awali zilikuwa hazipatikani kwa
urahisi.
“kupitia kambi hii
wataalamu wa JKCI wameweza kuwabainisha watu 23 ambao wameonekana kuwa na changamoto
zinazohitaji upasuaji wa moyo na matibabu ya kina zaidi”, alisema Dkt. Mutajwaa.
Dkt. Mutajwaa
aliwashukuru wataalamu wa JKCI kwa ushirikiano waliouonesha katika kutoa huduma
bingwa za moyo na kueleza kuwa hospitali hiyo imeanza kuwajengea uwezo
wataalamu wake kupitia kushirikiano walionao na JKCI ambapo zaidi ya watumishi
watano wamepata mafunzo ya uchunguzi wa magonjwa ya moyo katika Taasisi hiyo.
Aidha aliiomba JKCI
kuendelea kushirikiana na Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Manyara (MRRH) katika
kutoa huduma za kibingwa, kubadilishana uzoefu na kujenga uwezo wa wataalamu
ili kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa mkoa huo.
Wakizungumza kwa nyakati
tofauti wananchi waliopata huduma wakati wa kambi hiyo wamewapongeza wataalamu
wa JKCI kwa kutoa huduma kwa upendo bila kuchoka na kuhakikisha kuwa watu wote
waliohitaji huduma hizo wamezipata.
Catherine John mkazi wa
Manyara alisema huduma aliyoipata imemsaidia kujitambua, kuchukua hatua za
mapema na kufuata ushauri wa wataalamu wa afya ili tatizo la moyo alilonalo lisimdhuru
zaidi.
"Kambi hii
imetusaidia wananchi wengi ambao hatukuwa na uwezo wa kusafiri umbali mrefu kufuata
huduma za kibingwa za uchunguzi na matibabu kuzipata hapa kwetu kwa urahisi",
alisema Catherine
John Mbilinyi mkazi wa Manyara
alisema ni muhimu wananchi kutumia fursa kama hizi kupima afya zao kwa sababu
wanaweza kuwa na matatizo ya moyo bila ya wao kujua kama wanamatatizo hayo.
Kambi hiyo ya siku tano
ni sehemu ya juhudi za Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) za kusogeza huduma
za kibingwa za uchunguzi na matibabu ya moyo karibu na wananchi na kutekeleza
maagizo ya Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassan kufikisha huduma hizo kwa wananchi wote.
-
Mwisho -
Comments
Post a Comment