Kwa mara ya kwanza JKCI yafanya upasuaji wa myo kwa mtoto wa siku mbili

 

Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao kutoka mradi wa Little Heart wa Shirika la Muntada Aid  kutoka nchini Uingereza wakimfanyia upasuaji wa kuziba tundu lililopo kwenye moyo wa mtoto  wakati wa kambi maalumu ya siku sita iliyokuwa ikifanyika katika Taasisi hiyo na kumalizika jana jijini Dar es Salaam.


Baadhi ya wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakisikiliza wakati wa kuhitimisha kambi maalumu ya siku sita ya upasuaji wa moyo kwa watoto iliyokuwa ikifanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao kutoka  mradi wa Little Heart  wa Shirika la Muntada Aid kutoka nchini Uingereza na kumalizika jana jijini Dar es Salaam


Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya akiwa katika picha ya pamoja na wataalamu wa afya wa JKCI na wenzao kutoka mradi wa Little Heart wa Shirika la Muntada Aid lenye makao yake nchini Uingereza mara baada ya kuhitimisha kambi maalumu ya upasuaji wa moyo kwa watoto iliyokuwa ikifanyika katika Taasisi hiyo na kumalizika jana jijini Dar es Salaam.

Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya akimpatia zawadi Daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto kutoka Shirika la Muntada Aid Ahmet Sasmazel wakati wa kuhitimisha kambi maalumu ya upasuaji wa moyo kwa watoto iliyokuwa ikifanywa na wataalamu hao na kumalizika jana jijini Dar es Salaam.


Kaimu Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya akimpatia zawadi Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Muntada Aid lililopo nchini Uingereza Nayaf Sheick wakati wa kuhitimisha kambi maalumu ya upasuaji wa moyo kwa watoto iliyokuwa ikifanyika katika Taasisi hiyo na kumalizika jana jijini Dar es Salaam.

Picha na JKCI

***********************************************************************                                                ***********************


Na Mwandishi Maalumu - Dar es Salaam.

Kwa mara ya kwanza Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) imefanikiwa kumfanyia upasuaji wa moyo mtoto wa siku mbili aliyezaliwa akiwa na tatizo la kubana kwa mshipa wa damu unaopeleka damu kwenye mapafu (Severe pulmonary valve stenosis).

Upasuaji huo wa bila kufungua kifua kwa kutumia mtambo wa Cathlab (Percutaneous balloon pulmonary valvuloplasty- PBV) umefanyika akatika kambi maalumu ya siku sita iliyokuwa ikifanywa na watalaamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao kutoka mradi wa Little Heart wa shirika la Muntada Aid lililopo nchini Uingereza.

Akizungumza na waandishi wa habari jana jijini Dar es Salaam Kaimu Mkurugenzi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya alisema ushirikiano huo wa kimatibabu umeleta matokeo makubwa ikiwemo kufanikiwa kumfanyia upasuaji mtoto wa siku mbili.

“Hii ni mara yetu ya kwanza kumfanyia mtoto wa umri huu, mafanikio haya ni matokeo ya msaada wa vifaa tiba uliofanywa na shirika hili pamoja na serikali yetu ya Tanzania kwa kuweka mazingira wezeshi na kufanikisha upasuaji huu,” alisema Dkt. Angela.

Aidha Dkt. Angela ambaye pia ni daktari bingwa wa usingizi alisema jumla ya Watoto 44 wamefanyiwa upasuaji mdogo na mkubwa ambapo watoto 28 wamefanyiwa upasuaji kwa njia ya tundu dogo kwa kutumia mtambo wa Cathlab huku watoto 16 wakifanyiwa upasuaji mkubwa wa moyo wa kufungua kifua.

“Kupitia kambi hiyo wataalamu kutoka shirika la Muntada Aid wamekuja na vifaa tiba vyenye thamani ya milioni 50 ili kwa pamoja tuweze kuwasaidia watoto wengi wenye magonjwa ya moyo ya kuzaliwa nayo”, alisema Dkt. Angela

Katika hatua nyingine Dkt. Angela alitoa rai kwa wanawake wajawazito kufanya uchunguzi wa mapema ili kubaini changamoto za moyo kwa mtoto ili waweze kuwasaidia watoto na kuokoa maisha yao.

“Wazazi wa watoto wenye magonjwa ya moyo wengi wao utufikia wakiwa wamechelewa na matokeo ya kimatibabu yanakuwa siyo mazuri sana hivyo tunawahamasisha wafike mapema ili kupunguza changamoto hizo kwani JKCI tunatoa huduma za uchunguzi wa magonjwa ya moyo mapema kuwalinda watoto”, alisema Dkt. Angela

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Muntada Aid Nayaf Sheikh alisema shirika hilo limesafiri katika mataifa mbalimbali kuwasaidia watoto wanaohitaji upasuaji wa kibingwa lakini limeona upekee wa JKCI kutokana na kuwa na miundombinu wezeshi.

“Hii ni mara yetu ya 9 kuja JKCI na mara zote ambazo tumekuwa tukija hapa tumekuwa tukipewa ushirikiano wa watalamu ambao unatuwezesha kufanya upasuaji wa kibingwa kwa kiwango kikubwa hivyo watanzania na Afrika Mashariki kwa ujumla hawana haja tena ya kusafiri kwenda nje ya nchi kufuata matibabu ya kibingwa”, alisema Sheikh.

-Mwisho-


Comments

Popular posts from this blog

Serikali yazindua kitabu safari ya upandikizaji wa moyo Tanzania, JKCI yaweka historia mpya ya huduma za kibobezi

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma