JKCI yawataka wanamichezo, mashabiki kuchunguza afya ya moyo kuepuka vifo vya ghafla
Na Mwandishi
Maalumu-Dar es Salaam.
Wanamichezo na
mashabiki wametakiwa kuchunguza afya ya moyo kabla ya kufanya mazoezi na
kushiriki katika shughuli za michezo ili kuepuka vifo vya gafla vinavyoweza
kujitokeza uwanjani.
Hayo yamesemwa na
daktari bingwa wa moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)
Hospitali ya Dar Group Eva Wakuganda
wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi wa afya ya moyo kwa wanamichezo na
mashabiki wa timu ya mpira wa miguu ya Azam FC iliyofanyika jana katika viwanja
vya Hospitali ya JKCI Dar Group iliyopo jijini Dar es Salaam.
Kambi hiyo iliambatana
na utoaji wa mahitaji mbalimbali kwa wagonjwa pamoja na matembezi ya pamoja ya
wafanyakazi wa JKCI Hospital ya Dar Group ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya
kueleka mchezo wa mzizima Derby kati ya Azam FC na Simba Sports Club.
Dkt. Eva alisema jumla
ya mashabiki 95 walifanyiwa uchunguzi wa afya ya moyo lengo likiwa kuhamasisha jamii
hasa wanamichezo kufanya uchunguzi wa afya na kujua hali zao.
“Mashabiki wa Azam FC
wameonyesha umuhimu wa kujua hali ya afya zao kabla ya kushuhudia mechi kati ya
timu hiyo na Simba Sports Club kwani uchunguzi wa afya ya moyo ni muhimu katika
kuzuia vifo vya gafla vinavyotokea wakati wa michezo”, alisema Dkt. Eva.
Kwa upande wake Makamu
wa Rais Timu ya Mpira wa Miguu ya Azam FC Abdulkarimu Popat alisema ataendelea
kushirikiana na wataalamu wa JKCI Hospital ya Dar Group katika kuhakikisha kuwa
mashabiki na wachezaji wanapata huduma za afya.
“Sikujua kama natakiwa
kuchunguza afya yangu kabla ya kwenda uwanjani kushabikia, tumekuwa tukiona
mashabiki wenye mapenzi na timu zao wanapata mstuko wa moyo pale timu zao
zinapofungwa na hata wakati mwingine kupoteza maisha hivyo ni muhimu kufahamu
hali zetu ili tusipate madhara”, alisema Popat.
Naye Diwani wa Kata ya Vingunguti
na Meya Mstaafu wa jiji la Dar es Salaam Mhe. Omar Kumbilamoto aliishukuru
serikali kwa kuendelea kuboresha huduma za afya na kurahisisha upatikanaji wa
huduma hizo kwa jamii.
“Zamani tulijua ubora
wa huduma unapatikana katika hospital binafsi lakini baada ya kufika hapa na
kufanyiwa uchunguzi wa afya nimejionea maboresho makubwa ya vifaa tiba na
uwekezaji uliofanywa katika sekta ya afya”, alisema Kumbilamoto.
Mmoja wa mashabiki wa
timu ya mpira wa miguu ya Azam FC Octavian Achimpota alisema zoezi la kufanyiwa
uchunguzi wa afya kwa mashabiki limekuwa la kipekee na kuleta mchango mkubwa katika
kuimarisha afya za mashabiki na wanamichezo.
“Niwaombe wale ambao
hawajanufaika na zoezi hili wajitokeze tarehe 16 mwezi huu kwani zoezi la
uchunguza wa afya kwa mashabiki na wanamichezo litaendelea katika viwanja vya
chamazi jijini Dar es Salaam”, alisema Octavian






Comments
Post a Comment