Kamati ya Bunge Maendeleo ya Jamii yatembelea JKCI, yaipongeza kambi ya upasuaji wa moyo kwa watoto


Daktari wa upasuaji mdogo wa moyo kwa watoto kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu kilichopo nchini Saudi Arabia Dkt. Jameel Al-Ata akiwaeleza wajumbe wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya huduma na maendeleo ya jamii kuhusu upasuaji wa moyo kwa watoto wanaofanyika  katika Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI).  Wajumbe hao walitembelea Taasisi hiyo kwa ajili ya kuona kambi ya upasuaji wa moyo kwa watoto inayofanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao kutoka nchini Saudi Arabia.

Mbunge wa Jimbo la Mchinga ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya huduma na maendeleo ya jamii Mhe. Salma Kikwete akisoma bango la Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu kilichopo nchini Saudi Arabia ambacho kimetuma wataalamu wake kwenda katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kushirikiana na wataalamu wa taasisi hiyo kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto. Kushoto ni Mwenyekiti wa kamati hiyo Mhe. Stanslaus Nyongo akifuatiwa na Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel.


Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel, Mwenyekiti wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya huduma na maendeleo ya jamii Mhe. Stanslaus Nyongo, wajumbe wa kamati hiyo wakiwa  katika picha ya pamoja na wataalamu wa magonjwa ya moyo kwa watoto kutoka Kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu kilichopo nchini Saudi Arabia ambao wako katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ajili ya kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto kwa kushirikiana na wataalamu wa JKCI.
                
 *******************************************************************************************************************************************************************************************************************************************************

Na Andrew Chale - Dar es Salaam

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii imetembelea Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na kukutana na Wataalamu wa magonjwa ya moyo ya watoto kutoka Saudi Arabia wanaoendesha kambi maalum ya upasuaji bure kwa watoto.

 Kamati hiyo ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Stanslaus Nyongo (MB) iliambatana   na Naibu Waziri wa Afya, Dkt. Godwin Mollel ambapo Wajumbe wa Kamati hiyo (Wabunge) waliweza kupatiwa maelezo juu ya kambi hiyo ya matibabu  na Mkurugenzi wa Taasisi hiyo, Prof. Mohamed Janabi.

 Kambi hiyo ya matibabu ya moyo kwa watoto iliaanza Septemba 3, mwaka huu na kutarajia kumalizika Septembe 9, 2022 inafanywa na wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao kutoka kituo cha Mfalme Salman cha Misaada ya Kibinadamu kilichopo nchini Saudi Arabia.

 Aidha, JKCI kupitia kwa Dkt. Winnie Masakuya ilisema wanafanya kambi maalum ya upasuaji wa moyo  kwa watoto bure, ambapo aliomba wazazi waweze kuwapeleka watoto wao kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na kupewa matibabu.

 "Tunawaomba wazazi na Madaktari wenye watoto wanaosumbuliwa na matatizo ya moyo kama;matundu, mishipa ya damu ya moyo kutokuwa katika mpangilio wake (ASD for device closure, PDA for device closure, BAD, & Pulmonary valvular stenosis) wawalete kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi na upasuaji kwa wale itakaolazimika." alisema Dkt.Winnie Masakuya.

 Naye Mbunge wa Jimbo la Mchinga ambaye pia ni mjumbe wa Kamati ya kudumu ya Bunge ya huduma na maendeleo ya jamii Mhe. Salma Kikwete aliwaomba wazazi kutoka mikoa yote kuweza kujitokeza kwa wingi kupeleka watoto wao wenye matatizo ya moyo katika Taasisi hiyo ili kupatiwa uchunguzi wa moyo, kwani ni fursa ya kipekee ya uwepo wa wataalam hao hapa nchini.



Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yapata tuzo ya taasisi ambayo imetoa mchango wa kipekee kiuchumi na kijamii katika kuleta matokeo makubwa kwa kipindi cha mwaka 2023/2024

Wafanyakazi waliohama JKCI waagwa