Kongamano la siku ya wanawake Duniani lafanyika JKCI


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wanawake wa JKCI wakati wa sherehe ya kuadhimisha kilele cha siku ya wanawake duniani iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi hiyo leo jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya NMB Ruth Zaipuna akiwapongeza wanawake wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakati wa sherehe ya kuadhimisha kilele cha siku ya wanawake duniani iliyofanywa na wanawake wa JKCI katika ukumbi wa Taasisi hiyo leo jijini Dar es Salaam

Mgeni rasmi wa sherehe ya kuadhimisha siku ya wanawake duniani iliyofanywa na wanawake wa JKCI Mkurugenzi Mkuu Benki ya NMB Ruth Zaipuna akikata keki wakati wa sherehe hiyo iliyofanyika leo jijini Dar es Salaam


Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Engerasiya Kifai akiwafundisha wanawake wa JKCI namna ya kujali afya zao wakati wa sherehe iliyoandaliwa na wanawake hao kuadhimisha kilele cha siku ya wanawake dunia leo katika ukumbi wa taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam

Mkurugenzi Mkuu Benki ya NMB Ruth Zaipuna akimkabidhi zawadi mmoja ya washindi wa michezo mbalimbali iliyofanywa na wanawake wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete Afisa Muuguzi Magreth Mbaruk wakati wa sherehe ya kuadhimishia kilele cha siku ya wanawake duniani leo katika Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam



Baadhi ya wanawake wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakifuatilia hotoba mbalimbali zilizokuwa zikitolewa wakati wa sherehe ya kuadhimisha siku ya wanawake duniani iliyofanywa na wanawake hao katika ukumbi wa JKCI leo jijini Dar es Salam


Mgeni rasmi katika sherehe ya kuadhimisha kilele cha siku ya wanawake duniani iliyofanywa na wanawake wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Mkurungezi Mkuu Benki ya NMB Ruth Zaipuna akiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wanawake wa JKCI baada ya sherehe hiyo iliyofanyika leo jijini Dar es Salaam. Kushoto ni Mkurugenzi Mtendaji JKCI Dkt. Peter Kisenge

Na: JKCI
*********************************************************************************************************

Wanawake wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wametakiwa kuwa na ubunifu katika kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa wananchi wanaowahudumia huku wakiendeleza upendo walionao kama wanawake.

Rai hiyo imetolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati wa sherehe ya kuadhimisha kilele cha siku ya wanawake duniani iliyofanywa na wanawake wa JKCI katika Ukumbi wa Taasisi hiyo leo jijini Dar es Salaam.

Dkt. Kisenge alisema kuwa kutokana na maumbili ya uumbaji wanawake wamezawadiwa hali ya kuwa na upendo hivyo kuwahudumia wagonjwa kwa upendo wa hali ya juu tofauti na wanaume wanavyowahudumia wagonjwa.

Dkt. Kisenge aliongeza kuwa ni jukumu la wanaume kuwalinda wanawake kwani wanawake ndio kila kitu katika familia, ikitokea wanawake wakiumwa watoto wanakosa upendo wa mama kutokana na uzoefu uliopo kuwa wanaume huwa ‘bize’ hivyo kuacha kazi ya malezi kuwa ya mwanamke.

“Tunaamini kazi kubwa ambayo wanawake wameifanya katika Taasisi hii hadi kuwa bora Afrika Mashariki na kati, muendelee kuwa wabunifu na kufanya tafiti mbalimbali ambazo zitasaidia kufikisha ujumbe wa afya bora kwa wanawake wengi zaidi na kuifanya Taasisi hii kuwa bora duniani”, alisema Dkt. Kisenge

Akizungumza wakati wa kongamano hilo Mkurugenzi Mkuu wa Benki ya NMB Ruth Zaipuna alisema usawa wa kijinsia bado ni changamoto ingawa hatua kubwa imepigwa katika harakati za kufanikisha usawa ambapo takwimu zinawabeba wanawake wengi katika masuala ya ufanisi mahala pa kazi.

Ruth alisema wanawake katika maeneo ya kazi wanatakiwa kufahamu ya kwamba kazi ni wito na si kufanya kazi kwa mazoea na kuangalia mshahara kwani kwa kufanya hivyo wanaweza kukuwa kutokana na maendeleo ya teknolojia yaliyopo.

“Teknolojia ndio kila kitu kwani imebadili masuala mengi, kwetu sisi watu wa Taasisi za fedha teknolojia imesaidia kufanikisha utoaji wa huduma nje ya matawi yetu ambapo sasa mteja anaweza kujihudumia mwenyewe kwa simu ya mkononi kuanzia kufungua akaunti hadi kupata mikopo midogo midogo”,

“Kwenye sekta ya afya, teknolojia imewezesha kurahisisha huduma mbalimbali za kitabibu ikiwemo ‘robot operation’ huku ikipunguza maumivu na athari za upasuaji sambamba na kuondoa tatizo la upotevu wa damu nyingi wakati wa upasuaji”, alisema Ruth

Aidha Ruth ameahidi kuwa NMB katika kuboresha huduma zinazotolewa katika vyumba vya wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalum (ICU) katika Taasisi hiyo itatoa vitanda vya ICU, magodoro pamoja na mashuka ili wagonjwa waendelee kupatiwa huduma bora.

Kwa upande wake Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa JKCI Engerasiya Kifai alisema wanawake wanatakiwa kuzingatia kula mlo kamili na kufanya mazoezi kila siku ili kujikinga na magonjwa yasiyo ya kuambukiza pamoja na uzito uliokithiri.

“Wanawake tujenge utaratibu wa tuangalie afya zetu kwa ujumla tuwe na utaratibu wa kupima kiwango cha sukari kila siku na msukumu wa damu, pia tufanye mazoezi ya kuruka kamba na kufanya kazi za nyumbani hii itasaidia miili yetu kuwa imara na afya bora”.

Dkt. Kifai alisema wanawake watumie muda wao pia kupumzika walau masaa saba hadi nane kila siku kwani kwa kufanya hivyo kutasaidia miili yao kutokuchoka, kutumia muda wao pia kutoka kwenda kupumzika maeneo mazuri kupumzisha akili.

“Wanawake mnatakiwa kufanya vitu ambavyo hamfanyi kila siku, kujitafakari wenyewe, kwenda kwenye fukwe na hii itaboresha afya ya akili na kuifanya akili ifikiri vema na kupunguza mawazo”, alisema Dkt. Kifai

 


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari