China kuleta vifaa tiba nchini


Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel akimkaribisha Naibu Waziri Mkuu wa Serikali ya Watu wa China Mhe. Liu Guozhong alipofanya ziara katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) leo kuona huduma zinazotolewa. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimuelezea mafanikio ya Taasisi hiyo tangu kuanzishwa kwake Naibu Waziri Mkuu wa Serikali ya Watu wa China Mhe. Liu Guozhong alipofanya ziara katika Taasisi hiyo leo kuona huduma zinazotolewa.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimuelezea huduma zinazotolewa katika chumba cha upasuaji wa tundu dogo (CathLab) Naibu Waziri Mkuu wa Serikali ya Watu wa China Mhe. Liu Guozhong alipofanya ziara katika Taasisi hiyo leo kuona huduma zinazotolewa.

Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel akiwa katika picha ya pamoja na Naibu Waziri Mkuu wa Serikali ya Watu wa China Mhe. Liu Guozhong na viongozi wengine wa Serikali mara baada ya ziara ya Naibu Waziri Mkuu huyo kutembelea Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) leo kuona huduma zinazotolewa.

Na: JKCI

****************************************************************************************************

Tanzania na China zakubaliana kuanzisha mfumo wa upatikanaji wa vifaa tiba vinavyotumika kutoa huduma za matibabu ya moyo kutoka nchini China kuendeleza ushirikiano uliopo baina ya nchi hizo.

Ushirikiano huo unatarajiwa kurahisisha upatikanaji wa vifaa vinavyotumika kutoa huduma za matibabu ya moyo na matibabu mengine yanayohitaji vifaa tiba kupunguza rasimu ya upatikanaji wa vifaa tiba.

Akizungumza leo jijini Dar es Salaam wakati wa ziara ya Naibu Waziri Mkuu kutoka Serikali ya watu wa China Mhe. Liu Guozhong Naibu Waziri wa Afya Mhe. Dkt. Godwin Mollel alisema katika majadiliano na Naibu waziri huyo China imekubali kutoa msaada wa vifaa tiba nchini pamoja na kuanza kwa ushirikiano wa kuagiza vifaa tiba nchini China.

“Tumekubaliana kupitia Bohari ya Dawa (MSD) tutaenda kushirikiana na Serikali ya Watu wa China kupata vifaa tiba ambavyo mara nyingi tumekuwa tukiviagiza katika mataifa ya mbali na kuchukua muda mrefu kutufikia”, alisema Dkt. Mollel

Dkt.  Mollel alisema Tanzania imejipanga kuhakikisha kuwa Bohari ya Dawa (MSD) inaenda moja kwa moja katika viwanda vilivyopo nchini China kununua vifaa tiba hivyo kupunguza gharama za matibabu.

“Tanzania tayari tuna sayansi kubwa, lakini vifaa mbalimbali vinavyotumika kila siku katika kutoa huduma za matibabu havipatikani hapa nchini kwasababu hatuna viwanda vinavyozalisha vifaa hivyo”,

“Haya ni matunda ya Rais wetu Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwani tunapomuona akitembelea nchi mbalimbali duniani anafanya mambo makubwa ya ushirikiano na mataifa anayoyatembelea yaliyokuwa kisayansi na kiteknolojia ili kwapamoja tujifunze na kutumia fursa zilizopo kuendeleza sekta yetu ya afya”, alisema Dkt. Mollel

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema JKCI imekuwa moja ya Taasisi kubwa zinazotoa huduma za matibabu ya mogonjwa ya moyo barani Afrika, na kuwa yakwanza kufanya upasuaji mkubwa wa moyo na upasuaji wa moyo kwa watoto nchini yote hayo yakiwa ni matunda ya ushirikiano wa nchi ya Tanzania na China.

Dkt. Kisenge alisema leo Naibu Waziri Mkuu kutoka Serikali ya Watu wa China amefika JKCI kujionea vifaa vilivyowekezwa vyenye teknolojia ya kisasa duniani pamoja na kuwasalimia wataalamu wa afya waliopo nchini kutoka Serikali ya watu wa China ambao wamekuwa wakibadilishana nao uzoefu.

“Tumepata ugeni wa Naibu Waziri Mkuu kutoka Serikali ya Watu wa China aliyetembelea Taasisi yetu kutokana na uhusiano mzuri uliopo kati ya Tanzania na china, Namshukuru sana Mhe. Dkt Samia Suluhu Hassan kwakutusaidia katika rasilimali watu kwani sasa tuna madaktari bingwa wa hali ya juu, pamoja na vifaa tiba vya kutosha hivyo kuifanya taasisi yetu kuwa sehemu ya utalii tiba hapa nchini”, alisema Dkt. Kisenge

Dkt. Kisenge alisema Naibu Waziri Mkuu kutoka Serikali ya Watu wa China amefika JKCI kuona jengo ambalo lilijengwa na Serikali hiyo, kwani msaada walioutoa umekuwa mkubwa na sasa unawasaidia watu kutoka nchi zaidi ya 20 zilizopo Afrika na mataifa mengine kupata huduma za matibabu ya moyo.  


 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari