JKCI yafanya upasuaji wa moyo kwa watoto saba wa Zambia



Madaktari wa Usingizi na Wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia wakimlaza mtoto kwaajili ya kufanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi ya matibabu iliyomalizika jana nchini Zambia. Kambi hiyo ya siku tatu na nusu imewezeshwa na Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel.


Wataalamu wa afya wanaofanya kazi katika chumba cha wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu (ICU) wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) na wenzao wa Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia wakijaza fomu ya maendeleo ya mtoto aliyefanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi ya matibabu iliyomalizika jana nchini Zambia. Kambi hiyo ya siku tatu na nusu imewezeshwa na Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel.

************************************************************************************************************************************************************************************************

Watoto saba wenye matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo wamefanyiwa upasuaji wa moyo katika kambi maalumu ya matibabu  iliyomalizika jana nchini Zambia.

Kambi hiyo ya upasuaji ya siku tatu na nusu imefanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kushirikiana na wenzao wa Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia.

Akizungumza kuhusu kambi hiyo Godwin Sharau ambaye ni daktari bingwa wa upasuaji wa moyo kwa watoto katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) alisema watoto waliofanyiwa upasuaji ni wale wenye matatizo ya matundu, mishipa ya damu ya moyo kutokukaa katika mpangilio wake pamoja na Valvu.

“Tunamshukuru Mungu watoto tuliowafanyia upasuaji wanaendelea vizuri na kuna ambao wametoka katika chumba cha Uangalizi Maalumu (ICU) na kwenda wodini kuendelea na matibabu”.

“Tunaishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuwezesha kufanyika kwa kambi hii ya upasuaji ambayo imesaidia kuokoa maisha ya watoto hawa saba ambao baada ya kupona wataendelea na maisha kama watoto wengine”, alisema Dkt. Sharau ambaye pia ni mkuu wa kitengo cha upasuaji wa moyo kwa watoto.

Dkt. Sharau alisema katika kambi hiyo walipata nafasi ya kubadilishana ujuzi wa kazi na wenzao wa hospitali hiyo wa namna ya  kufanya upasuaji pamoja na  jinsi ya kuwahudumia wagonjwa hao anaamini  baada ya miaka ijayo watalamu hao wa Zambia  wataweza kusimama na kufanya upasuaji kama JKCI.

Kwa upande wake Mkuu wa Utawala wa Ubalozi wa Tanzania nchini Zambia Humphrey Shangarai alisema waliwapokea wataalamu wa JKCI tarehe 18 mwezi huu ambao walikwenda kufanya uchunguzi na  upasuaji  wa moyo kwa watoto katika Hospitali ya Taifa ya  Moyo Zambia.

“Tumefurahi kwani wataalamu wetu wamefanya upasuaji vizuri na wenyeji wamekiri haijawahi kutokea ushirikiano wa aina  hii  katika nchi za Afrika na idadi ya upasuaji waliyoifanya ni kubwa pia wameamini kazi nzuri inayofanywa na JKCI na kuonesha mfano katika nchi za Afrika“, alisema Shangarai.

Kwa upande wa wazazi ambao watoto wao wamefanyiwa upasuaji katika kambi hiyo walishukuru kwa huduma waliyopatiwa watoto wao na kusema kuwa imewapunguzia gharama ya safari ya kuifuata huduma hiyo nje ya Zambia.

“Mwanagu alikuwa na tatizo la kutokupumua vizuri na kukohoa baada ya kumfanyia vipimo iligundulika anatundu kwenye moyo wakanipa rufaa ya kuja hapa na wakaniambia anatakiwa kufanyiwa upasuaji, nilipata hofu kwani sikuwa na uhakika kama hili linaweza kufanyika Zambia.

“Namshukuru Mungu amefanyiwa upasuaji na anaendelea vizuri, nawaomba wazazi wenzangu wenye watoto ambao wana matatizo kama haya wasikate tamaa ipo siku watafanyiwa upasuaji na kupona kama ilivyofanyika kwa mwanangu”, alishukuru Msopero Gwesi.

“Baada ya vipimo mwanangu aligundulika kuwa na shida ya moyo na nilikuwa nampeleka hospitali mara kwa mara kwaajili ya matibabu hivi karibuni alipata shida ya kushindwa kupumua nikapewa rufaa ya kuja hapa baada ya vipimo nikaambiwa upasuaji hauwezi kufanyika hapa Zambia.

“Wiki iliyopita nikaambiwa kuna wataalamu wanakuja kutoka Tanzania hivyo mwanangu atafanyiwa upasuaji. Upasuaji umefayika na mwanangu anaendelea vizuri nashukuru sana kwa huduma hii kwani imetusaidia wanawake ambao hatuna uwezo wa kusafiri kwenda nje ya nchi kuipata huduma hii hapa nchini”, alishukuru Achimba Mpundu.

Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH la nchini Israel ndilo lililowezesha kufanyika kwa kambi hiyo ya upasuaji wa moyo kwa watoto  nchini Zambia kwa kutoa  vifaa tiba na kuwasafirisha wataalamu wa  JKCI.

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari