Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia


Balozi wa Tanzania nchini Zambia Mhe. Luteni Generali Mathew Edward Mkingule akiwa katika picha ya pamoja na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika uwanja wa ndege wa kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA)

kabla ya wataalamu hao kuanza safari  ya  kuelekea katika hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia kwaajili ya kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto. Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel ndilo lililowezesha kufanyika kwa kambi hiyo ya upasuaji nchini Zambia.

Balozi wa Tanzania nchini Zambia Mhe. Luteni  Generali Mathew Edward Mkingule akizungumza na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) leo katika uwanja wa ndege wa kimatifa wa Julius Nyerere (JNIA) kabla ya kuanza safari yao ya kwenda katika hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia kwaajili ya kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto. Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel ndilo lililowezesha kufanyika kwa kambi hiyo ya upasuaji nchini Zambia.

Balozi wa Tanzania nchini Zambia Mhe. Luteni Generali Mathew Edward Mkingule akiagana na Mkurugenzi wa Upasuaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Angela Muhozya mara baada ya kuwaaga wataalamu wa Taasisi hiyo waliokwenda nchini Zambia kwaajili ya kufanya upasuaji wa moyo kwa watoto. Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel ndilo lililowezesha kufanyika kwa kambi hiyo ya upasuaji nchini Zambia.


Wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Wafanyakazi wa ubalozi wa Tanzania nchini Zambia na wataalamu wa Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini Zambia wakiwa katika picha ya pamoja kabla ya kuanza kwa kambi ya upasuaji wa moyo kwa watoto itakayofanyika katika hospitali hiyo kwa muda wa siku tatu. Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel ndilo lililowezesha kufanyika kwa kambi hiyo ya upasuaji nchini Zambia.

****************************************************************************************************************************************************************************************

Timu ya wataalamu tisa wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) leo tarehe 17/01/2024 wamesafiri kwenda nchini Zambia kwa jili ya kutoa huduma ya upasuaji wa moyo kwa watoto katika Hospitali ya Taifa ya Moyo ya nchini humo.

Katika kambi hiyo ya upasuaji ambayo itafanyika kuanzia tarehe 18/01/2024 hadi tarehe 20/01/2024 wataalamu wa JKCI kwa kushirikiana na wenzao wa Zambia watafanya upasuaji huo ambao utaenda sambamba na kuwajengea uwezo na ujuzi wa kazi.

Wataalamu hao ni madaktari bingwa wa watoto, upasuaji wa moyo, usingizi na wagpnjwa mahututi, maafisa uuguzi wanaohudumia wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu na wataalamu wa kuendesha mashine ya kuusaidia moyo na mapafu kufanya kazi (Heart Lung Machine).

Daktari bingwa mmoja ametangulia nchini Zambia kwaajili ya kufanya uchunguzi wa moyo kwa watoto ili kubaini watoto ambao wanahitaji kufanyiwa upasuaji katika kambi hiyo ya matibabu.

Kufanyika kwa kambi hii ya upasuaji wa moyo ni utelelezaji wa mkataba wa miaka mitatu wa makubaliano baina ya JKCI na Hospitali ya Taifa ya moyo ya nchini Zambia wa kutibu wagonjwa wa moyo pamoja na kuwajengea uwezo wataalamu wa afya wa hospitali hiyo  wa jinsi ya kuwatibu wagonjwa wa moyo uliosainiwa  tarehe 20/04/2023 jijini Dar es Salaam.

Shirika la Okoa Moyo wa Mtoto (Save a Child’s Heart – SACH) la nchini Israel ndilo lililowezesha kusainiwa kwa mkataba huo pamoja na kufanyika kwa kambi hiyo ya upasuaji nchini Zambia.

Mwaka 2015 SACH ilianza ushirikiano na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa kuwajengea uwezo wataalamu wa afya kwa kufanya kambi mbalimbali za upasuaji wa moyo kwa watoto na kutoa mafunzo nchini Israel ambapo hadi sasa JKCI imekuwa na uwezo wa kufanya upasuaji wa moyo. Kutokana na wataalamu wa JKCI kuwa na ujuzi wa kutosha katika upasuaji wa moyo kwa watoto SACH imeiunganisha JKCI na nchi ya Zambia ili waweze kuwasimamia ili nao wapate ujuzi huo na kuweza kufanya upasuaji.

“Afya ya Moyo Wako ni Jukumu Letu”.

  

 

Comments

Popular posts from this blog

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari