Tanzania na China kuendeleza ushirikiano katika matibabu ya moyo

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi tuzo ya kumshukuru kwa kazi nzuri aliyoifanya daktari kutoka Jamhuri ya Watu wa China Prof. Zhahg Hailong wakati wa kuwaaga madaktari watatu kutoka China waliokuwa wanafanya kazi JKCI kwa kipindi cha miaka miwili hivi karibuni jijini Dar es Salaam.

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi cheti cha kuthamini mchango wake daktari kutoka Jamhuri ya Watu wa China Sun Xufang wakati wa kuwaaga madaktari watatu kutoka China waliokuwa wanafanya kazi JKCI kwa kipindi cha miaka miwili hivi karibuni jijini Dar es Salaam.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi cheti cha kumshukuru kwa kazi nzuri aliyoifanya daktari kutoka Jamhuri ya Watu wa China Wang Jun wakati wa kuwaaga madaktari watatu kutoka China waliokuwa wanafanya kazi JKCI kwa kipindi cha miaka miwili hivi karibuni jijini Dar es Salaam.

Madaktari kutoka Jamhuri ya Watu wa China wakimkabidhi Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge zawadi ya kumshukuru kwa kuwa na ushirikiano mzuri kwa kipindi cha miaka miwili ya utendaji kazi wao katika Taasisi hiyo hivi karibuni wakati wa hafla fupi ya kuwaaga iliyofanyika katika ukumbi wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam.


Daktari kutoka Jamhuri ya Watu wa China Prof. Zhahg Hailong akitoa neno la shukrani kwa wafanyakazi wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwa ushirikiano waliouonyesha wakati wa hafla fupi ya kuwaaga madaktari watatu kutoka China iliyofanyika hivi karibuni katika ukumbi wa Taasisi hiyo.

Baadhi ya wataalamu wa afya wa Jamhuri ya watu wa China na wenzao wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakifuatilia wakati wa hafla fupi ya kuwaaga madaktari watatu kutoka Jamhuri wa Watu wa China baada ya kumaliza muda wao wa kutoa huduma katika Taasisi hiyo hivi karibuni jijini Dar es Salaam.

Na: JKCI

**********************************************************************************************************

Tanzania na China kuendelea kushirikiana katika sekta ya afya kwa kuwaleta madaktari bingwa kushirikiana na wenzao mabingwa wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kubadilishana uzoefu na kuboresha huduma za kibingwa nchini.

Ushirikiano huo umeleta tija katika sekta hiyo kwani unatoa fursa kwa watalamu wa afya kupata ujuzi, pamoja na kuendelea kujenga mahusiano mazuri baina ya nchi hizo mbili.

Akizungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam wakati wa kuwaaga madaktari watatu kutoka nchini China Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge aliwapongeza madaktari hao kwa kutoa huduma za matibabu ya moyo kwa watanzania kwa kipindi cha miaka miwili.

Dkt. Kisenge alisema madaktari bingwa kutoka China wamekuwa sehemu ya wataalamu wa afya wa JKCI kwa kufanya kazi kwa pamoja na kujitoa kushiriki katika shughuli zote za Taasisi hivo kuondoka kwao kunaacha pengo kutokana na ushirikiano uliokuwepo baina yao.

“Mmekuwa mkijitoa kushirikiana na wataalamu wetu tangu mlipofika hapa JKCI, tunawaomba mnavyoondoka msisite kurudi wakati wowote kwani sasa JKCI ni kama nyumbani kwenu”, alisema Dkt. Kisenge.

Kwa upande wake Daktari kutoka Jamhuri ya Watu wa China Prof. Zhahg Hailong ameushukuru uongozi wa JKCI na wafanyakazi kwa kuonyesha uaminifu kwao kwa kipindi chote walichokuwa wakifanya kazi JKCI.

Zhahg alisema kufanya kazi na wataalamu wa afya wa JKCI kumewaongezea ujuzi, na uwezo wa kufanya upasuaji wa moyo wa aina mbalimbali pamoja na kutoa huduma kwa wagonjwa wanaohitaji uangalizi maalumu.

“Sisi tunavyoondoka madaktari wengine kutoka China wanakuja kuendeleza ushirikiano na Taasisi hii, nimesikia kuna mwenzetu alishafanya kazi hapa JKCI anarejea naamini na mimi ninavyoondoka leo nitarejea tena hapa kwani tayari hapa ni nyumbani”, alisema Prof. Zhahg

Naye Mkuu wa Idara ya Upasuaji wa Moyo kwa watu wazima Dkt. Evaristi Nyawawa alisema madaktari hao kutoka Jamhuri ya Watu wa China wamekuwa wakifanya kazi mchana na usiku kuhakikisha watanzania wanapata huduma.

Dkt. Nyawawa alisema madaktari hao wameonyesha mfano mzuri wa kuiwakilisha nchi ya China vizuri kwani wameweza kuacha familia zao kwa kipindi chote hicho na kufanya kazi kwa amani.

“Tunathamini sana mchango wenu, mmeacha alama hapa JKCI kwa kufanya kazi kwa upendo na bidii, tutaendelea kushirikiana nanyi kwani lengo letu wote ni moja la kuokoa maisha ya wagonjwa wa moyo wanaotutegemea”, alisema Dkt. Nyawawa

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari