JKCI yaandaa mkutano wa kimataifa wa moyo

Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akizungumza na wadau leo wakati wa uzinduzi wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo (Cardiotan Africa) utakaofanyika mwezi Aprili 2025 katika Hoteli ya Sea Cliff iliyopo mjini Zanzibar.

Mwenyekiti wa kamati ya maandalizi ya mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo (Cardiotan Africa) utakaofanyika mwezi Aprili 2025 katika Hoteli ya Sea Cliff iliyopo mjini Zanzibar Dkt. Delilah Kimambo akielezea malengo ya mkutano huo leo wakati wa uzinduzi wa mkutano huo jijini Dar es Salaam.

Baadhi ya wafanyakazi na wadau wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) wakifuatilia wakati wa uzinduzi wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo (Cardiotan Africa) uliokuwa ukifanyika leo katika ukumbi wa Taasisi hiyo iliyopo jijini Dar es Salaam


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge akiwa katika picha ya pamoja na wadau wa Taasisi hiyo mara baada ya uzinduzi wa mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo (Cardiotan Africa) utakaofanyika mwezi Aprili 2025 mjini Zanzibar kumalizika.

Na: Stella Gama

*************************************************************************************************************************************************

Zaidi ya washiriki 1000 kutoka nchi 40 wanatarajiwa kushiriki katika mkutano wa tatu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo unaoandaliwa na Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI).

Mkutano huo utafanyika mwezi Aprili mwakani katika Hoteli ya Sea cliff & Spa, visiwani Zanzibar.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es Salaam katika mkutano wa kutambulisha mkutano huo Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge alisema kupitia mkutano huo wataalamu wa afya watafundishwa kutumia teknolojia mpya ya kutibu magonjwa ya moyo kwa kutumia njia za kisasa kama vile akili mnemba.

“Mkutano wa Cardiotan 2025 utaelekeza namna ya kutibu matatizo ya magonjwa ya moyo, madaktari kutoka nchi za Afrika ni wakati wetu sasa kupitia mkutano huu kujifunza mbinu mbalimbali za kutibu wagonjwa wa moyo”, alisema Dkt. Kisenge.

Kwa upande wake mwenyekiti wa maandalizi ya mkutano huo Dkt. Delilah Kimambo alisema lengo kubwa la mkutano huo ni pamoja na kukusanya wataalamu wa afya ambao wanamchango mkubwa katika sekta ya matibabu ya moyo kujadili mada zitakazohusiana na kinga, lishe na matibabu ya moyo.

Dkt. Delilah alisema kupitia mkutano huo kwa mara ya kwanza JKCI inaenda kushirikiana na Wizara ya Utalii na Mambo ya Kale Zanzibar kuwafundisha watu ambao sio wataalamu wa afya jinsi ya kutoa huduma ya kwanza kwa mgonjwa anayehitaji huduma ya kwanza na kuwaleta watu pamoja.

“Kupitia mkutano wetu wa kimataifa wa magonjwa ya moyo tunaenda kujadili na kuona jinsi gani tunaweza kuisaidia Afrika kwa njia rahisi kabisa ili matibabu ya moyo yaweze kupatikana kwa urahisi”, alisema Dkt. Delilah.

Naye Kaimu Katibu Mtendaji wa Kamisheni ya Utalii Zanzibar Aziwa Issa Makame alisema kupitia mkutano huo utaenda kuisaidia Zanzibar kuongeza idadi ya watalii wanaoingia nchini na wale wanaoongoza watalii wataweza kupatiwa mafunzo ambayo yataweza kuwasaidia wageni wao pale wanapopata changamoto za kiafya.

Aziwa aliishukuru JKCI kwa kuwa na wazo la kupeleka mkutano huo Zanzibar na kuichagua sekta ya utalii kuwa miongoni mwa sekta zitakazopatiwa mafunzo kwani mafunzo hayo ni muhimu kuifikia jamii.

“Nachukua nafasi hii kuwahimiza wadau wote wa utalii kujiandikisha kwaajili ya kupatiwa mafunzo ya namna ya kumsaidia mtu anayehitaji huduma ya kwanza ili kulinda afya za watalii wetu”, alisema Aziwa.

Mkutano wa kimataifa wa magonjwa ya moyo  wa mwaka 2025 wenye kaulimbiu “Kuimarisha huduma za moyo barani Afrika kupitia jitihada za pamoja” utakuwa mkutano wa tatu tangu kuanzishwa mkutano huo mwaka 2023 ambapo mkutano wa pili wa mwaka 2024 ulikuwa wa mafanikio makubwa ambayo uliwakutanisha wataalamu wa afya zaidi ya 500 kutoka mataifa mbalimbali duniani.


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari