Wanafunzi 965 wapimwa moyo Dar es Salaam

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali ya Shandong Provincial iliyopo nchini China ambaye pia anafanya kazi Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Zhao Lijian akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi mwanafunzi wa Shule ya Msingi Msasani wakati wa kambi maalumu ya siku mbili iliyomalizika leo jijini Dar es Salaam. Jumla ya wanafunzi 965 wa Shule za Msingi Hananasif na Msasani wamefanyiwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi. 

Daktari bingwa wa watoto wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Theophylly Ludovick akizungumza na mzazi ambaye mtoto wake amefanyiwa kipimo cha moyo wakati wa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa wanafunzi wa Shule ya Misingi Msasani leo jijini Dar es salaam. Jumla ya wanafunzi 965 wa Shule za Msingi Hananasif na Msasani wamefanyiwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi. 

Daktari kutoka Hospitali ya YUNNAN FUWAI iliyopo nchini China Zhang Shuyue akisikiliza mapigo ya moyo ya mwanafunzi wa Shule ya Msingi Msasani wakati wa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa wanafunzi wa Shule ya Misingi Msasani leo jijini Dar es salaam. Jumla ya wanafunzi 965 wa Shule za Msingi Hananasif na Msasani wamefanyiwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi.

Dakatari bingwa wa magonjwa ya moyo kutoka Hospitali ya YUNNAN FUWAI iliyopo nchini China Duo Lin akizungumza na Afisa Utafiti na Mafunzo wa Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete (JKCI) Makrina Komba pamoja na Mratibu wa Tiba na magonjwa yasiyoambukiza Wilaya ya Kinondoni  Dkt. Omary Mwangaza wakati wa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa wanafunzi wa Shule ya Misingi Msasani leo jijini Dar es salaam. Jumla ya wanafunzi 965 wa Shule za Msingi Hananasif na Msasani wamefanyiwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi.

Na: Stella Gama

*********************************************************************************************************

Wanafunzi 965 wa shule za msingi za Hananasif na Msasani za jijini Dar es Salaam wamefanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa kupimwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography – ECHO).

Wanafunzi hao wamefanyiwa kipimo hicho wakati wa kambi maalumu ya uchunguzi wa magonjwa ya moyo ya siku mbili iliyofanywa na madaktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) kwakushirikiana na wenzao kutoka Hospitali ya YUNNAN FUWAI iliyopo nchini China.

Akizungumza na waandishi wa habari wakati wa kuhitimisha kambi hiyo leo jijini Dar es Salaam kwa niaba ya Mkurungenzi Mtendaji wa JKCI Daktari bingwa wa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Theophylly Ludovick alisema watoto 743 wa shule ya msingi Hananasif na watoto 222 wa shule ya msingi Msasani wamefanyiwa kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi.

Dkt. Theophylly alisema upimaji huo uliofadhiliwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) umehusisha uchunguzi wa viashiria vya matatizo ya moyo kugundua kama kuna matatizo ya moyo ambayo hayajawahi kugundulika.

“Katika Shule ya Msingi Hananasif tumekuta watoto watatu wana matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo ambapo mmoja wao anahitaji upasuaji wa kuziba tundu lililopo katika moyo wake, mtoto huyo ameshafika katika Taasisi yetu tumemlaza na kesho atafanyiwa upasuaji wa moyo”,

“Kwa hapa shule ya Msingi Msasani pia tumewakuta watoto watatu wana matatizo ya moyo ya kuzaliwa nayo, watoto hawa tutawapanga katika ratiba zetu kwaajili ya kuwafanyia upasuaji wa kuziba matundu yaliyopo katika mioyo yao”, alisema Dkt. Theophylly

Dkt. Theophylly alisema Taasisi kwakushirikiana na Hospitali ya YUNNAN FUWAI iliyopo nchini China watatoa huduma za matibabu kwa watoto sita waliogundulika kuwa na matatizo ya moyo bila gharama.

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto kutoka Hospitali ya Shandong Provincial iliyopo nchini China ambaye pia anafanya kazi katika Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Zhao Lijian aliwapongeza wazazi kwa kuitikia wito wa kuwafikisha watoto katika kambi hiyo kwaajili ya kufanyiwa uchunguzi.

Dkt. Zhao alisema kambi hiyo imefanyika kama sehemu ya mafanikio ya miaka 60 ya ushirikiano kati ya Tanzania na China katika sekta ya afya kuendelea kutoa huduma za afya hasa kwa watoto.

“Huu ni mwanzo wa progamu hii ya kuwafuata watoto mashuleni kuwafanyia uchunguzi wa magonjwa ya moyo, zoezi hili litaendelea tena kwa awamu nyingine ili tuweze kuwagundua watoto wenye matatizo ya moyo mapema na kuwapatia matibabu kwa wakati”, alisema Dkt. Zhao

Kwa upande wa wazazi ambao watoto wao walipata huduma hiyo walizishukuru Serikali za Tanzania na China kwa kuwa na wazo la kuwapima wanafunzi waliopo mashuleni na kuomba zoezi hilo liendelee na kwa watoto wengine.

Mzazi wa mtoto aliyegundulika kuwa na tundu kwenye moyo Iptsam Anwary alisema tangu ajifungue mtoto huyo hajawahi kuwa na dalili zozote zinazoendana na magonjwa ya moyo hadi jana alipopimwa akiwa shuleni Hananasif.

“Naishukuru sana Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali ya watu wa China kuanzisha progamu hii ya kuwafanyia uchunguzi wa magonjwa ya moyo watoto waliopo mashuleni kwani bila hivyo nisigejua kama mtoto wangu ana tundu kwenye moyo”,

“Sikuwa na wazo la kwenda kumpima mtoto wangu moyo wala sikuwahi kuhisi kama mtoto wangu ana tatizo la moyo lakini baada ya kufanyiwa kipimo na kukutwa na tatizo hili daktari kaniambia tatizo alilonalo linaweza kutibika”, alisema Iptsam

Naye Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Msasani Edward Mollel ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuifikiria jamii na kuiwezesha kupata huduma muhimu za uchunguzi wa afya.

Mollel alisema jamii bado haijapata elimu ya kutosha kuhusu uchunguzi wa afya na hiyo imejidhihirisha kwa watoto wengi wa shule ya msingi Msasani kufanyiwa kipimo cha kuchunguza moyo unavyofanya kazi kwa mara ya kwanza.

“Nilikuwa najua tatizo la moyo kwa watoto sio kubwa lakini leo nimethibitisha kupitia watoto wetu waliopimwa hapa kwani watoto hawa uwezi kuwafikiria kama wana matatizo ya moyo”, alisema Mollel


Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari