Watu 558 wafanyiwa uchunguzi wa magonjwa ya moyo

Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Mlagwa Yango akimpima kipimo cha kuangalia jinsi moyo unavyofanya kazi (Echocardiography – ECHO) mwananchi aliyepatiwa huduma katika kambi maalumu ya siku nne ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba iliyokuwa ikifanyika katika Zahanati ya Bungoni kata ya Ilala na kumalizika jana jijini Dar es Salaam. Kambi hiyo imefanywa na Hospitali ya JKCI Dar Group kwakushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu.

Daktari wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Yona Jeremia akimshauri mwananchi wa Ilala baada ya kufanya vipimo vya magonjwa ya moyo wakati wa kambi maalumu ya siku nne ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba iliyokuwa ikifanyika katika Zahanati ya Bungoni kata ya Ilala na kumalizika jana jijini Dar es Salaam. Kambi hiyo imefanywa na Hospitali ya JKCI Dar Group kwakushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu.

Afisa Uuguzi kutoka Mpango wa Taifa wa damu salama akimtoa damu mwananchi aliyejitokeza kuchangia damu wakati wa kambi maalumu ya siku nne ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba iliyokuwa ikifanyika katika Zahanati ya Bungoni kata ya Ilala na kumalizika jana jijini Dar es Salaam. Kambi hiyo imefanywa na Hospitali ya JKCI Dar Group kwakushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu.

Na: JKCI

*************************************************************************************************************************

Julma ya watu 558 wa Wilaya ya Ilala na vitongoji vyake wamefanyiwa uchunguzi na wengine kupewa matibabu ya magonjwa ya moyo katika kambi maalumu ya Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan tiba mkoba.

Kambi hiyo maalumu ya siku nne iliyomalizika jana imefanywa na wataalamu wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) katika Zahanati ya Bungoni Wilaya ya Ilala kwa kushirikiana na Ofisi ya Mbunge wa jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu.

Akizungumza wakati wa kufunga kambi hiyo Daktari bingwa wa magonjwa ya moyo kwa watoto wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Hospitali ya Dar Group Eva Wakuganda alisema asilimia 67 ya watu wote waliofanyiwa vipimo vya moyo wamekutwa na magonjwa mbalimbali ya moyo ikiwemo shinikizo la juu la damu, moyo kutanuka, moyo kushindwa kufanya kazi na kuziba kwa mishipa ya damu.

 “Katika kambi hii pia tumeweza kuwafanyia uchunguzi wa magonjwa ya moyo kwa watoto 75 ambapo kati yao watoto 12 tuliwagundua kuwa na matatizo ya matundu kwenye moyo”, alisema Dkt. Eva

Dkt. Eva alisema katika kambi hiyo watu 215 walipewa rufaa kufika JKCI kwaajili ya kuendelea na matibabu zaidi na wale waliohitaji kutumia dawa walipewa dawa bila gharama.

“Sambamba na upimaji wa magonjwa ya moyo katika kambi hii watu 400 wamepimwa kipimo cha homa ya ini na kupewa chanjo hiyo bila gharama”, alisema Dkt. Eva

Kwa upande wake Mganga mfawidhi wa Zahanati ya Bungoni Dkt. Ester Akili alimshukuru Mbunge wa Jimbo la Ilala Mhe. Mussa Azzan Zungu kwa kuwafikishia huduma za kibingwa za matibabu ya moyo wananchi wa Ilala bila gharama.

Dkt. Ester alisema mwitikio wa watu kujitokeza kupima moyo umekuwa mkubwa tofauti na walivyotarajia kwani watu kutoka Wilaya ya Ilala na wilaya za jirani waliweza kujitokeza kufanya uchunguzi wa afya.

Tunaishukuru sana JKCI kwa kutuletea wataalamu hawa mabingwa wa moyo, kupitia kambi hii watu wameweza kukitafuta kituo chetu mahali kilipo na kufika kwani kituo hiki ni kipya na watu wengi walikuwa hawakifahamu.

“Zahanati ya Bungoni ni mypa tangu ianze kutoa huduma ina miezi saba sasa, tunashukuru kupitia kambi hii zahanati yetu imetambulika katika jamii ya watu kutoka maeneo mbalimbali”, alisema Dkt. Ester

Naye mwananchi aliyepatiwa huduma katika kambi hiyo Willium Kiwazo alisema alikutwa na shida ya moyo miaka mitano iliyopita lakini baada ya kupata matibabu na kuendelea vizuri hakuweza kurudi tena hospitali kuangalia maendeleo yake.

Willium alisema kushindwa kwake kuendelea kufuatilia matibabu kumetokana na bima yake ya afya kuisha muda wake miaka miwili iliyopita na kushindwa kukata bima nyingine.

“Nilifanyiwa uchunguzi JKCI miaka mitano iliyopita na kukutwa na tatizo la moyo ambalo nilipewa dawa lakini baada ya hapo sijarudi tena hospitali kutokana na kadi yangu ya bima kuisha muda wake na kushindwa kukata bima nyingine”, alisema Willium

Willium alitoa wito kwa wananchi kujitokeza kupima afya zao pale fursa za upimaji wa magonjwa mbalimbali zinapojitokeza kupunguza gharama ya kuzifuata mahali zilipo.

 

Comments

Popular posts from this blog

Wataalamu wa JKCI kufanya upasuaji wa moyo nchini Zambia

JKCI na AICC Hospitali kutoa huduma za uchunguzi na matibabu ya moyo katika kikao kazi cha wenyeviti na watendaji wakuu wa Taasisi za Umma

JKCI yamshukuru Rais Dkt.Samia kwa kuwapa magari