JKCI yawahimiza Wafanyakazi kupima Afya mara kwa mara kuepuka magonjwa yasiyoambukiza


 Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge akimkabidhi zawadi ya mashine ya kupimia shinikizo la damu, joto la mwili na kiwango cha sukari Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Fedha, Lucius Mwenda mara baada ya kumaliza kutoa elimu ya kujikinga na magonjwa ya moyo wakati wa zoezi la upimaji wa afya kwa watumishi wa Wizara hiyo jijini Dodoma.


Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge akitoa elimu kuhusu magonjwa ya moyo kwa wafanyakazi wa Wizara ya Fedha wakati wa zoezi la upimaji wa afya kwa watumishi wa Wizara hiyo jijini Dodoma.


Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Fedha Lucius Mwenda akizungumza na wafanyakazi wa wizara hiyo mara baada ya kupata elimu ya kujikinga na magonjwa ya moyo wakati wa zoezi la upimaji wa afya kwa watumishi wa Wizara ya Fedha jijini Dodoma.


Mtaalamu wa Maabara wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI)Glory Mtui akimchukua sampuli ya damu Afisa Habari Mkuu wa Wizara ya Fedha Scola Malinga kwa ajili ya kupima kiwango cha mafuta kwenye damu wakati wa zoezi la upimaji wa afya ya moyo  kwa watumishi wa Wizara hiyo jijini Dodoma.

Baadhi ya wafanyakazi wa Wizara ya Fedha wakimsikiliza Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI), Dkt. Peter Kisenge wakati akitoa elimu ya kujikinga na magonjwa ya moyo katika zoezi la upimaji wa afya ya moyo kwa watumishi wa wizara hiyo jijini Dodoma.

*****************************************************************************************************************************************************************************************

Wafanyakazi wa Wizara ya Fedha wametakiwa kujenga utamaduni wa kupima afya zao angalau mara moja kwa mwaka ili kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza yakiwemo magonjwa ya moyo ambayo yamekuwa chanzo cha vifo vya ghafla.

Rai hiyo imetolewa leo na Mkurugenzi Mtendaji wa Taasisi ya Moyo Jakaya Kikwete (JKCI) Dkt. Peter Kisenge wakati akitoa elimu ya jinsi ya kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kwa wafanyakazi wa Wizara hiyo katika ukumbi wa Kambarage jijini Dodoma.

Dkt. Kisenge ambaye pia ni Daktari Bingwa wa Magonjwa ya Moyo alisema elimu hiyo imeenda sambamba na huduma za uchunguzi wa afya ya moyo kwa wafanyakazi hao ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuhamasisha jamii kujenga utamaduni wa kujali afya zao mapema.

Akizungumza na wafanyakazi hao Dkt. Kisenge alisema magonjwa yasiyoambukiza yanaongezeka kwa kasi kutokana na mabadiliko ya mtindo wa maisha, ulaji usiofaa, kutofanya mazoezi, uvutaji wa sigara, unywaji wa pombe uliopitiliza pamoja na msongo wa mawazo.

“Hivi sasa Taasisi yetu imekuja na kampeni ya ‘Jua Namba Zako’ inayolenga kuhamasisha wananchi kufahamu viwango vya afya zao ikiwemo shinikizo la damu, kiwango cha sukari kwenye damu, uzito unaolingana na urefu pamoja na kiwango cha mafuta mwilini”,  alisema Dkt. Kisenge.

Alifafanua kuwa shinikizo la damu linapaswa kuwa chini ya 120/80, kiwango cha sukari kwenye damu chini ya 5.6, uzito unaolingana na urefu (BMI) kati ya 18.5 hadi 24.9, mzunguko wa kiuno chini ya sentimita 94 kwa wanaume na sentimita 80 kwa wanawake pamoja na mapigo ya moyo kati ya 60 hadi 100 kwa dakika.

Dkt. Kisenge alisema unene kupita kiasi hususan kuongezeka kwa ukubwa wa kiuno ni moja ya vihatarishi vya magonjwa ya moyo huku akiongeza kuwa kadri umri unavyoongezeka ndivyo hatari ya kupata magonjwa yasiyoambukiza ikiwemo moyo, kisukari na saratani inavyoongezeka.

“Magonjwa yasiyoambukiza yanaathiri afya za watu pamoja na uzalishaji wa kiuchumi. Ni muhimu wananchi na wafanyakazi kuchukua hatua za mapema kwa kupima afya zao mara kwa mara na kubadili mtindo wa maisha”,  alisema.

Katika elimu hiyo wafanyakazi walihimizwa kufanya mazoezi mara kwa mara, kutumia ngazi badala ya lifti inapowezekana, kupunguza muda wa kukaa ofisini bila kufanya mazoezi, kula lishe bora, kunywa maji ya kutosha pamoja na kuepuka uvutaji wa sigara na  unywaji wa pombe kupita kiasi ikiwemo shisha.

 “Watu wanaofanya mazoezi wana nafasi kubwa ya kuishi maisha marefu na kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza. Hata mazoezi madogo madogo yanayofanyika eneo la kazi yanaweza kusaidia kuboresha afya”, alisema Dkt. Kisenge.

Alisema JKCI imeendelea kusogeza huduma karibu na wananchi kupitia matawi yake ya Kariakoo, Kawe, Oysterbay, Hospitali ya Dar Group pamoja na Arusha huku ikiwa na mpango wa kufungua tawi jipya Chato.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Fedha Lucius Mwenda aliishukuru JKCI kwa kutoa elimu na huduma za uchunguzi wa afya ya moyo kwa wafanyakazi wa wizara hiyo.

“Ili tuweze kutekeleza majukumu yetu kwa ufanisi ni lazima tuwe na afya njema. Elimu hii tuliyoipata imetukumbusha umuhimu wa kujali afya zetu na tunatarajia kuona mabadiliko chanya kwa wafanyakazi wetu”,  alisema Mwenda.

Aliongeza kuwa wafanyakazi wa wizara hiyo wamepokea elimu hiyo kwa hamasa kubwa huku akiomba huduma za uchunguzi wa afya ziendelee kutolewa mara kwa mara ili kuwasaidia wafanyakazi kutambua hali zao za afya mapema na kuchukua hatua stahiki.

JKCI inaendelea na kampeni ya kuhamasisha wananchi kujikinga na magonjwa yasiyoambukiza kupitia utoaji wa huduma za uchunguzi wa afya kwa kuwafuata wananchi mahali walipo ikiwemo kwenye maeneo yao ya kazi kwa lengo la kusaidia jamii kutambua hali zao za afya mapema na kupata ushauri wa kitaalamu.

Comments

Popular posts from this blog

Kutoka miaka 22 hadi kustaafu: Safari ya Lemmah yatoa somo kwa Watumishi wa Umma

Wanawake waaswa kulinda mioyo yao, kuepuka sukari na chumvi kupita kiasi